PHPWord

 

 

رِسَالَةٌ فِي الدِّمَاءِ الطَّبِيعِيَّةِ لِلنِّسَاءِ

 

Makala kuhusu damu za asili za wanawake

 

بِقَلَمِ فَضِيلَةِ الشَّيْخِ العَلَّامَةِ

مُحَمَّدِ بْنِ صَالِحٍ العُثَيْمِينِ

غَفَرَ اللَّهُ لَهُ وَلِوَالِدَيْهِ وَلِلمُسْلِمِينَ

 

Kimeandikwa na Mheshimiwa, Sheikh, Mwanachuoni

Muhammad Bin Swaleh Al-Uthaimiin

Mwenyezi Mungu amsamehe yeye, wazazi wake, na Waislamu wote.

 


بِسْمِ اللهِ الرَّحمَنِ الرَّحِيمِ

Makala kuhusu damu za asili za wanawake

 

Kwa jina la Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema mwenye kurehemu

Kila sifa njema zinamstahikia Mwenyezi Mungu, tunamsifu na tunamtaka msaada, na tunamuomba msamaha, na kutubia kwake, na tunajilinda kwa Mwenyezi Mungu kutokana na shari za nafsi zetu na matendo yetu mabaya. Mwenye kuongozwa na Mwenyezi Mungu hakuna wa kumpoteza, na mwenye kupotezwa na Mwenyezi Mungu hakuna wa kumuongoza, na nina shuhudia kuwa hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu peke yake, hana mshirika. Na nina shuhudia kuwa Muhamad ni mja wake na ni mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake na watu wake na Maswahaba zake, na wote wanaowafuata kwa wema mpaka Siku ya Malipo, na zimfikie amani na salamu nyingi.

Ama baada ya hayo: Kwa hakika damu zinazompata mwanamke; nazo ni Hedhi, Damu ya ugonjwa, na Nifasi, ni miongoni mwa mambo muhimu yanayohitaji kubainishwa na kufahamika hukumu zake, na kutofautishwa kati ya kauli isiyo sahihi na kauli sahihi katika kauli za Wanazuoni kuhusu hayo. Na tegemeo liwe katika yale yaliyotiwa nguvu au kudhoofishwa, kupitia mwangaza wa yaliyokuja katika Qur'ani na sunna.

1- Kwa kuwa Qur'ani na sunna ndio vyanzo viwili vya msingi vinavyojengewa hukumu za Mwenyezi Mungu Mtukufu alizowaamrisha waja wake wamuabudu kwa kuzitekeleza na akawawajibisha nazo.

2- Na kwa kuwa kutegemea Kitabu na Sunna kunaleta utulivu wa moyo, na kukunjuka kwa kifua, raha ya nafsi, na kuondokana na dhima.

3- Na kwa sababu visivyokuwa hivi viwili, huletwa dalili kwa ajili yake, wala havitumiki kuwa dalili yenyewe.

Hakika hakuna hoja ila katika maneno ya Mwenyezi Mungu Mtukufu na maneno ya Mtume Wake, rehema na amani zimshukie; na vilevile maneno ya wenye elimu miongoni mwa Maswahaba, kwa mujibu wa kauli yenye nguvu, kwa sharti kwamba pasiwepo katika Kitabu na Sunna kinachopingana nacho. Na kwamba isipingane kauli yake na kauli ya Swahaba mwingine; na ikiwa katika Qur'ani na Sunna kipo kinachokwenda kinyume na kauli yake, basi ni lazima kuchukua yaliyoko katika Qur'ani na Sunna. Na iwapo itapingwa na kauli ya Swahaba mwingine, hutazamwa kauli yenye nguvu zaidi kati ya kauli mbili hizo, na huchukuliwa ile yenye nguvu miongoni mwazo; kwa kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

﴿...فَإِن تَنَٰزَعۡتُمۡ فِي شَيۡءٖ فَرُدُّوهُ إِلَى ٱللَّهِ وَٱلرَّسُولِ إِن كُنتُمۡ تُؤۡمِنُونَ بِٱللَّهِ وَٱلۡيَوۡمِ ٱلۡأٓخِرِۚ ذَٰلِكَ خَيۡرٞ وَأَحۡسَنُ تَأۡوِيلًا﴾

"...na mkizozana katika jambo basi lirudisheni kwa Mwenyezi Mungu na Mtume, ikiwa mnamuamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho. Hayo ndiyo bora zaidi na ndiyo yenye mwisho mwema." [An-Nisaa: 59].

Huu ni ujumbe mfupi katika yale yanayohitaji kubainishwa kuhusu damu hizi na hukumu zake, nao unajumuisha sehemu zifuatazo:

Sura ya kwanza: Katika maana ya Hedhi, na hekima yake.

Sura ya Pili: Kuhusu Muda wa Hedhi na Urefu Wake.

Sura ya Tatu: Kuhuhusu Matukio ya Dharura yanayoweza kujitokeza katika Hedhi.

Sura ya Nne: Kuhuhusu Hukumu za Hedhi.

Sura ya Tano: Kuhusu Damu ya Ugonjwa na hukumu zake.

Sura ya Sita: Kuhusu nifasi na hukumu zake.

Sura ya Saba: Kuhusu matumizi ya vitu vinavyozuia Hedhi au kuileta, na yanayozuia mimba au kuiondosha.

Sura ya Kwanza: Kuhusu maana ya Hedhi, na hekima yake.

Hedhi katika lugha ya Kiarabu: Ni kutiririka kwa kitu na kukimbia wake.

Kisheria: Hedhi ni damu ya maumbile ambayo hutolewa na mfuko wa uzazi kupitia tupu ya mwanamke aliyevunja ungo kama sehemu ya afya, bila ya sababu, katika siku maalumu; Hivyo ni damu ya maumbile isiyotokana na ugonjwa, jeraha, kuanguka au kuzaa. Na kwa kuwa ni damu ya maumbile, hutofautiana kulingana na hali ya mwanamke, mazingira yake na hali ya hewa; kwa hivyo wanawake hutofautiana ndani yake kwa tofauti zinazoonekana wazi.

Na hekima ndani ya hilo ni kwamba: Kwa kuwa mtoto aliye tumboni mwa mama yake hawezi kupata lishe kama jinsi anavyopata yule aliye nje ya tumbo, wala haiwezekani, hata mama yake ambaye ndiye mwenye huruma kuliko wote kwake, kumfikishia chochote katika chakula; hapo ndipo Mwenyezi Mungu -Mtukufu- akaweka kwa mwanamke majimaji ya damu ambayo mtoto aliye tumboni hutumia kama lishe kwayo bila kuhitaji kula na kumeng'enya. Majimaji hayo huingia mwilini mwake kupitia kitovu, ambapo damu huenea katika mishipa yake, naye hupata lishe kwayo. Basi ametukuka mno Mwenyezi Mungu, Mbora wa waumbaji.

Hii ndiyo hekima ya hedhi; na kwa sababu hiyo, mwanamke anapobeba mimba hedhi hukatika kwake, hivyo hatokwi na damu ya hedhi ila mara chache; na vivyo hivyo wanawake wanaonyonyesha huwa wachache miongoni mwao wanaopata hedhi, hususani mwanzoni mwa kipindi cha kunyonyesha.

Sura ya Pili: Kuhusu Muda wa Hedhi na Kipindi Chake.

Maelezo katika sura hii yako katika sehemu mbili:

Sehemu ya kwanza: Kuhusu umri ambao hedhi huja.

Sehemu ya pili: Kuhusu muda wa hedhi.

Ama sehemu ya kwanza: Umri ambao kwa kawaida hutokea Hedhi ni kati ya miaka kumi na mbili hadi miaka hamsini, na huenda mwanamke akapata Hedhi kabla ya hapo au baada yake, kulingana na hali yake, mazingira yake na hali ya hewa ya mahali alipo.

Na wanachuoni, Mwenyezi Mungu awarehemu, wametofautiana: Je, kuna kikomo maalumu cha umri ambapo hutokea hedhi, kiasi kwamba mwanamke hapati hedhi kabla yake wala baada yake, na kwamba atakachokiona kabla yake au baada yake ni damu ya ugonjwa si hedhi?

Wanachuoni walitofautiana katika hilo; Ad-Darimi -baada ya kutaja tofauti hizo- akasema: Haya yote, kwa mtazamo wangu, si sahihi! Kwa kuwa marejeo katika yote hayo ni kwenye kuwepo; hivyo kiasi chochote kitakachopatikana katika hali yoyote na umri wowote, ni lazima kihesabiwe kuwa ni hedhi. Na Mwenyezi Mungu ndiye Ajuaye zaidi1.

Na hili alilolisema Ad-Daarimi ndilo sahihi, nalo ndilo alilolichagua Sheikhul-Islam Ibn Taymiyyah2, hivyo mwanamke atakapoona damu ya hedhi, atakauwa na hedhi, hata akiwa chini ya miaka tisa au juu ya miaka hamsini. Na hilo ni kwa sababu hukumu za hedhi Mwenyezi Mungu Mtukufu na Mtume wake -rehema na amani ziwe juu yake- wamezifungamanisha na kuwepo kwake; na Mwenyezi Mungu na Mtume wake -rehema na amani ziwe juu yake- hawakuweka umri maalumu. Hivyo inawajibika kurejea katika kuwepo huko ambako hukumu zimefungamanishwa, na kuweka umri maalumu kunahitaji dalili kutoka katika Qur'an Tukufu au Sunna, na hakuna dalili katika hilo.

Ama jambo la pili nalo ni muda wa hedhi, yaani kiasi cha muda wake.

Hakika wanachuoni wamehitilafiana (mitazamo) katika jambo hili hitilafu kubwa, kiasi cha kufikia kauli sita au saba. Akasema Ibnul-Mundhir (Mwenyezi Mungu amrehemu): Na baadhi ya wanachuoni wamesema: Hakuna kikomo kwa siku wala uchache wa kutoka damu ya hedhi wala kwa wingi wake.3

Nimesema: Na kauli hii ni kama kauli ya Darami iliyotangulia, nayo ndiyo chaguo la Sheikhul-Islaam ibnu Taimiyya, na hiyo ndiyo sahihi; kwa kuwa juu yake zipo dalili kutoka katika Kitabu na Sunna na mazingatio.

Na ushahidi wa kwanza ni kauli yake Mtukufu:

﴿وَيَسۡـَٔلُونَكَ عَنِ ٱلۡمَحِيضِۖ قُلۡ هُوَ أَذٗى فَٱعۡتَزِلُواْ ٱلنِّسَآءَ فِي ٱلۡمَحِيضِ وَلَا تَقۡرَبُوهُنَّ حَتَّىٰ يَطۡهُرۡنَۖ...﴾

"Na wanakuuliza juu ya hedhi. Waambie, huo ni uchafu. Basi jitengeni na wanawake wakati wa hedhi. Wala msiwaingilie mpaka watwaharike (wawe safi)..." [Al-Baqara: 222] Mwenyezi Mungu ameufanya ukomo wa zuio kuwa ni kutwaharika, wala hakuufanya ukomo huo kuwa ni kupita kwa siku moja na usiku mmoja, wala siku tatu, wala siku kumi na tano; hivyo jambo hili linabainisha kwamba sababu ya hukumu ni hedhi, kuwepo kwake au kukosekana kwake. Muda wowote hedhi ikiwepo basi hukumu huthibiti; na anapotwaharika kutokana nayo, hukumu zake huondoka.

Ushahidi wa Pili: Ni yale yaliyothibiti katika Sahihi Muslim, kwamba Mtume rehema na amani ziwe juu yake alimwambia Aisha pindi alipopata hedhi na alikuwa amehirimia Umra: "Fanya kama anavyofanya hujaji isipokuwa usizunguke Nyumba (Al-Ka'aba) mpaka utwaharike." Akasema: Ilipofika siku ya Nahr (kuchinja) akatwaharika, akatekeleza Twawaf al-Ifadha." Hadi mwisho wa Hadithi4.

Na katika Sahihi mbili ya kwamba Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake akamwambia: "Subiri; utakapokuwa safi, kisha toka uende Tan'iim (ni eneo liko nje kidogo ya Makka)."5 Hivyo Mtume -rehema na amani ziwe juu yake- akaweka ukomo wa katazo kuwa ni twahara, wala hakuufanya ukomo huo kuwa muda maalumu; na hili linaonyesha kwamba hukumu inahusishwa na hedhi kwa kuwepo kwake au kutokuwepo kwake.

Ushahidi wa tatu: Kwamba makadirio na ufafanuzi huu uliyotajwa na baadhi ya wanazuoni wa fiqhi katika suala hili halipo katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu wala katika Sunna za Mtume wa Mwenyezi Mungu -rehema na amani ziwe juu yake-, pamoja na kwamba haja, bali dharura, inasukuma kubainishwa kwake. Basi lau ingelikuwa miongoni mwa yale yanayowajibika kwa waja kuyaelewa na kumuabudu Mwenyezi Mungu kwayo, basi Mwenyezi Mungu na Mtume wake -rehema na amani ziwe juu yake- wangelibainisha kwa ubainifu ulio wazi kwa kila mmoja; kwa sababu ya umuhimu wa hukumu zinazotokana na hilo, kama vile Swala, Funga, Ndoa, Talaka, Urithi, na hukumu nyinginezo. Kama ambavyo Mwenyezi Mungu Mtukufu na Mtume wake -rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake- wamebainisha idadi ya swala, nyakati zake, rukuu zake na sujudi zake. Na Zaka: Mali zake, viwango vyake, kiasi chake, na walengwa wake wanaostahiki; na Swaumu: Muda wake na wakati wake; na Hija na mengineyo, Hata maadili ya kisheria ya kula na kunywa, na kulala, na tendo la ndoa, na kukaa, na kuingia nyumbani na kutoka humo, na maadili ya kisheria ya kwenda haja, hadi idadi ya mapanguso ya kujisafisha haja kwa mawe, na mengineyo miongoni mwa mambo madogo na makubwa; yote hayo ni miongoni mwa yale ambayo Mwenyezi Mungu amekamilisha nayo Dini, na akatimiza nayo neema Yake juu ya Waumini, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu:

﴿...وَنَزَّلۡنَا عَلَيۡكَ ٱلۡكِتَٰبَ تِبۡيَٰنٗا لِّكُلِّ شَيۡءٖ...﴾

"...na tumekuteremshia Kitabu hiki kinacho bainisha kila kitu..." [An-Nahl: 89] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:

﴿...مَا كَانَ حَدِيثًا يُفْتَرَى وَلَـكِن تَصْدِيقَ الَّذِي بَيْنَ يَدَيْهِ وَتَفْصِيلَ كُلَّ شَيْءٍ...﴾

"...hayakuwa ni maneno yaliyo zuliwa, bali ni ya kusadikisha yaliyo kabla yake, na ufafanuzi wa kila kitu..." [Surat Yusuf: 111]

Kwa kuwa makadirio haya na tafsiri hizi hazikupatikana katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu Mtukufu wala katika Sunna ya Mtume -rehema na amani ziwe juu yake-, imebainika kuwa hayastahiki kutegemewa; bali kinachotegemewa ni kile kinachoitwa hedhi, kitu ambacho hukumu za kisheria zimefungamanishwa nacho katika kuwapo kwake na kutokuwapo kwake. Na dalili hii — Yaani: Kwamba kutotajwa kwa hukumu katika Kitabu na Sunna ni dalili ya kutozingatiwa kwake — itakunufaisha katika suala hili na mengineyo miongoni mwa masuala ya kielimu; kuwa hukumu za kisheria hazithibiti isipokuwa kwa dalili za kisheria; kutoka katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu, au sunna za Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, au makubaliano ya wanachuoni yanayojulikana, au upimaji sahihi wa mambo (Qiyas). Amesema Shaikhul-Islam Ibn Taymiyyah katika kanuni yake moja: “Na miongoni mwa hayo ni kwamba jina la hedhi Mwenyezi Mungu -Mtukufu- amelihusisha nalo hukumu nyingi katika Kitabu na sunna, wala hakuweka ukomo maalumu wa kiwango chake cha chini wala cha juu, wala (ukomo wa) twahara baina ya hedhi mbili, pamoja na kuwa hilo ni jambo lililoenea kwa Umma na wanalihitajia; na lugha haitofautishi kati ya kiwango na kiwango. Basi atakayeweka mpaka katika hilo amekwenda kinyume na Kitabu na sunna.”6. Mwisho wa maneno yake.

Dalili ya nne: Mazingatio, yaani: Qiyaas (upimaji) sahihi ulio thabiti na unaoendelea; ni kwamba Mwenyezi Mungu Aliyetukuka amebainisha kuwa hedhi ni maudhi. Hivyo, wakati wowote hedhi inapokuwepo basi maudhi yapo; hakuna tofauti kati ya siku ya pili na ya kwanza, wala kati ya nne na ya tatu. Wala hakuna tofauti baina ya siku ya kumi na sita na siku ya kumi na tano, wala baina ya siku ya kumi na nane na siku ya kumi na saba. Hivyo Hedhi ni Hedhi, na Maudhi ni Maudhi; Sababu ipo katika siku hizo mbili kwa kiwango sawa sawa, basi vipi itakuwa sahihi kutofautisha Hukumu kati ya siku hizo mbili ilhali zimefanana katika Sababu? Je, hili si ni kinyume na upimaji sahihi wa mambo (Qiyasi)? Na je, hivi upimaji sahihi siyo kuwa sawa siku mbili hizo katika hukumu kwa kuwa zimewiana katika sababu ya hukumu?

Dalili ya tano: Hitilafu za kauli za wanaobainisha mipaka na kupingana kwa kauli hizo; kwani hilo linaonyesha kuwa hakuna dalili katika suala hili inayolazimu kurejelewa, bali ni hukumu za jitihada zinazoweza kukosea au kupatia, wala hakuna moja kati ya kauli hizo yenye haki zaidi ya kufuatwa kuliko nyingine; na wakati wa mzozo ni lazima kurejea katika Kitabu (Qur'ani) na Sunna za Mtume -rehema na amani ziwe juu yake-.

Ikidhihirika nguvu ya kauli kwamba hakuna idadi ya uchache wala wala wingi masiku ya hedhi, na kwamba hiyo ndiyo kauli yenye nguvu; basi fahamu kwamba damu yote ya maumbile atakayoiona mwanamke ambayo haina sababu ya kidonda na mfano wake, hiyo ni damu ya hedhi bila kuuwekea ukomo wa muda wala umri; isipokuwa ikiwa itaendelea kumtoka mwanamke bila kukatika jumla, au ikakatika kwa muda mfupi kama siku moja au mbili katika mwezi, basi hiyo huwa ni damu ya ugonjwa. Na utakuja ufafanuzi wa damu ya ugonjwa na hukumu yake, Mwenyezi Mungu akipenda.

Amesema Sheikhul-Islaam ibnu Taimiyya - Mwenyezi Mungu amrehemu-: Asili katika kila kinachotoka katika mfuko wa uzazi huwa ni hedhi, mpaka ithibiti dalili kwamba ni damu ya ugonjwa.7

Na akasema pia: Basi damu yoyote itakayoonekana ni hedhi, endapo haitajulikana kuwa ni damu ya mshipa au jeraha.8 Mwisho.

Na kauli hii, pamoja na kuwa ndiyo yenye nguvu zaidi kwa upande wa dalili, pia iko karibu zaidi kufahamika na kueleweka, na ni rahisi zaidi kwa utekelezaji kwa vitendo kuliko walivyotaja walioweka mipaka; na chenye kuwa hivyo ndicho chenye stahiki zaidi ya kukubaliwa kwa kuwa kinaafikiana na madhumuni ya dini ya Uislamu na kanuni yake ya msingi, nayo ni urahisi na wepesi, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:

﴿...وَمَا جَعَلَ عَلَيۡكُمۡ فِي ٱلدِّينِ مِنۡ حَرَجٖ...﴾

"Wala hakuweka juu yenu mambo mazito katika Dini." [Al-Hajj: 78], Na amesema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Hakika dini ni nyepesi, na hatoifanyia mkazo dini yeyote ila itamshinda, basi shikamaneni na mfanye kadiri ya uwezo yanayoweza kukuwekeni karibu, na toeni bishara." Imepokelewa na Bukhari9.

Na miongoni mwa tabia zake rehema na amani ziwe juu yake "Kwamba hakuwahi kupewa hiyari Mtume rehema na amani ziwe juu yake baina ya mambo mawili isipokuwa atachukua jepesi lake, madamu si dhambi."10.

Hedhi ya mjamzito:

Mara nyingi sana mwanamke anapopata ujauzito hukatika damu ya hedhi, kama anavyosema Imam Ahmad: Wanawake wengi hujua ujauzito kwa kukatika hedhi.11

Basi mjamzito atakapoiona damu, ikiwa ni kabla ya kujifungua kwa muda mfupi kama siku mbili au tatu, huku akiwa na uchungu wa kujifungua, basi damu hiyo ni damu ya uzazi (Nifasi), na ikiwa damu hiyo itakuwa kabla ya kujifungua kwa muda mrefu au kwa muda mfupi, isipoambatana na uchungu wa kujifungua, basi si damu ya uzazi (nifasi); lakini je, itakuwa ni hedhi ambayo zinathibiti kwake hukumu za hedhi, au ni damu iliyoharibika ambayo haipati hukumu za hedhi?

Katika jambo hili kuna mitazamo tofauti miongoni mwa Wanachuoni, na yaliyo sahihi ni kwamba hiyo ni hedhi iwapo iko katika hali ya kawaida ya hedhi yake; kwa sababu asili katika damu inayompata mwanamke ni kuwa ni hedhi, iwapo hakuna sababu inayozuia kuhesabiwa kwake kuwa ni hedhi, na wala hakuna katika Kitabu na Sunna kinachozuia hedhi ya mjamzito.

Haya ndio madhehebu ya Maliki12 na Shaafiy13, na ndio lililochaguliwa na Sheikh al-Islam Ibn Taymiyyah; akasema katika Al-Ikhtiyaaraat (ukurasa wa 30): Na Al-Baihaqiy amelisimulia hivyo kama riwaya kutoka kwa Ahmad, bali ametaja kwamba Ahmad alirejea kwake.

Na kwa msingi huu, hedhi ya mjamzito inathibiti kwake hukumu zile zile zinazothibiti kwa hedhi ya mwanamke asiyemjamzito, isipokuwa katika mambo mawili:

Jambo la kwanza: Talaka. Ni haramu kumtaliki mwanamke anayelazimika kukaa eda akiwa katika hedhi ikiwa si mjamzito; na si haramu kumtaliki mjamzito. Kwa sababu talaka wakati wa hedhi kwa mwanamke asiye mjamzito ni kinyume na kauli yake Mwenyezi mungu mtukufu

﴿...فَطَلِّقُوهُنَّ لِعِدَّتِهِنَّ...﴾

"...wapeni talaka katika wakati wa eda zao..." [At-Talaq: 1] Ama talaka ya mwanamke mwenye mimba akiwa katika hedhi, hilo halipingani; kwa sababu anayempa talaka mwanamke mwenye mimba basi amempa talaka kwa ajili ya eda yake, iwe yuko katika hedhi au yuko twahara; kwa sababu eda yake ni kwa ujauzito. Kwa hiyo si haramu kwake kumtaliki baada ya kujamiiana, tofauti na wengine.

Jambo la pili: Hedhi ya mjamzito haimalizi muda wa eda, tofauti na hedhi ya mwanamke asiyemjamzito. Kwa sababu eda ya mjamzito haikomi ila kwa kujifungua, iwe anatokwa na damu ya hedhi au la. Kwa kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu:

﴿...وَأُوْلَاتُ الأَحْمَالِ أَجَلُهُنَّ أَن يَضَعْنَ حَمْلَهُنَّ...﴾

"Na wenye mimba eda yao mpaka watakapo zaa." [Attwalaaq: 4].

Sura ya tatu: Kuhusu Matukio ya dharura yanayoathiri Hedhi

Na matukio ya dharura yanayohusiana na hedhi yako katika aina kadhaa:

Aina ya Kwanza: Kuongezeka au Kupungua; mfano wake ni kuwa mzunguko wa mwanamke ukiwa siku sita, kisha damu ya hedhi ikaendelea hadi siku saba; au mzunguko wake ukiwa siku saba, kisha atwaharike katika siku ya sita.

Na aina ya pili: Kutangulia au kuchelewa; mfano: ada yake ya hedhi huwa mwishoni mwa mwezi, kisha akaona hedhi mwanzoni mwake, au ada yake huwa mwanzoni mwa mwezi, kisha akaiona mwishoni mwake.

Na wanachuoni wametofautiana katika hukumu ya aina hizi mbili, na lililo sahihi ni kwamba: Mwanamke atakapoona damu basi hiyo ni hedhi, na wakati wowote akitwaharika kutokana nayo basi ametwaharika, iwe zimezidi siku zake za kawaida au zimepungua, na iwe zimetangulia au zimechelewa. Na dalili ya hilo imetangulia kutajwa katika sehemu iliyotangulia, ambapo sheria imeambatanisha hukumu za hedhi na kuwapo kwake.

Huu ndio msimamo wa Madhehebu ya Kishaafiy, na ndio chaguo la Sheikhul-Islam Ibnu Taymiyyah, na ameuimarisha na kuutetea Mwandishi wa Al-Mughni, akasema: Lau ada ingelizingatiwa kwa namna iliyotajwa katika madhehebu, basi Mtume rehema na amani zimshukie angeliubainisha kwa Umma wake, na isingelikuwa halali kwake kuchelewesha ufafanuzi wake.1415 Kwa sababu haifai kuchelewesha kubainisha mpaka ukaisha muda wake wakubainisha, na wake zake na wengineo miongoni mwa wanawake wanahitaji kubainishiwa hilo kila wakati, basi hakuwa wa kulipuuzia kulibainisha hilo. Wala hakuna kilichopokelewa kutoka kwa Mtume -rehema na amani ziwe juu yake- cha kutaja ada ya hedhi wala kuibainisha, isipokuwa katika hukumu ya mwanamke mwenye istihaadha tu.16. Mwisho wa kunukuu.

Aina ya tatu: Maji maji ya njano au ya kahawia; kwa namna ambayo huonekana damu ikiwa ya njano kama maji ya vidonda, au iliyochanyika kati ya rangi ya njano na nyeusi. Basi haya yakitokea wakati wa hedhi, au yakaungana nayo kabla ya kutwaharika, yanazingatiwa kuwa ni hedhi; tunayathibitishia hukumu za hedhi. Na yakitokea baada ya kutwaharika si hedhi; kwa kauli ya Ummu Atwiya -radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake-: "Tulikuwa hatuchukulii maji maji ya kahawia na njano baada ya twahara kuwa ni chochote" Imepokelewa na Abu Daudi kwa mlolongo mzuri wa wasimulizi17, Na pia ameipokea Bukhari bila ya kuzidisha (baada ya kutwaharika), lakini ametunga mlango kwa kauli yake: “Mlango wa maji maji ya njano na kahawia katika siku zisizo za hedhi”18.

Amesema katika sherehe (ufafanuzi) wake Fat-hul-Baari: Anaashiria kwa hilo kuleta muafaka kati ya hadithi ya Aisha iliyotangulia katika kauli yake: "mpaka uone ute mweupe." Na imebainisha hadithi ya Ummu Atwiya -radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake- iliyotajwa katika mlango, kwamba hilo — yaani hadithi ya mama Aisha -radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake- — limechukuliwa kuwa linahusu pale mwanamke anapoona maji maji ya kahawia na njano katika siku za hedhi; ama nje ya siku hizo, basi (hukumu ni) kama alivyosema Ummu Atwiya -radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake-.19 Mwisho wa kunukuu.

Na hadithi ya Aisha aliyoiashiria, ni lile alilolitaja Bukhari kwa yakini kabla ya mlango huu20, kwamba wanawake walikuwa wakiagiza kipande cha kitambaa, yaani; kitu ambacho mwanamke hujitia ili ajue kama bado imebaki athari ya hedhi au la, ili iende kwa mama wa waumini Aisha radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake; ndani yake kuna Kursuf yaani; pamba, ikiwa na rangi ya njano, alikuwa akisema: "Msifanye haraka mpaka muione alama nyeupe."21

Na ute mweupe ni maji meupe yanayotoka katika mfuko wa uzazi wakati hedhi inapokatika.

Na aina ya nne: Ni kukatika katika kwa hedhi, kwa namna kwamba mwanamke huona siku moja damu, na siku nyingine akawa yuko twahara na mfano wake, basi hizi ni hali mbili:

Hali ya kwanza: Kuwa jambo hili liwe pamoja na mwanamke daima, muda wake wote; basi hiyo ni damu ya ugonjwa, na huthibiti kwa anayepatwa nayo, hukumu ya mwanamke mwenye damu ya ugonjwa.

Hali ya pili: isiwe inatokea kwa mfululizo kwa mwanamke, bali humjia baadhi ya nyakati, na anakuwa na wakati wa twahara ulio sahihi. Basi wanachuoni - Mwenyezi Mungu awarehemu - wametofautiana kuhusu ukavu huu: je, unahesabiwa kuwa twahara au unaingia chini ya hukumu za hedhi?

Basi madhehebu ya Shafi'i katika kauli zake mbili iliyo sahihi zaidi ni kwamba hukumu za hedhi zinamhusu, hivyo huhesabiwa kuwa hedhi22, na hilo ndiyo chaguo la Sheikhul-Islam Ibn Taimiyya na mwandishi wa al-Fa'iq23, na ni madhehebu ya Abu Hanifa pia24, Na hilo ni kwa sababu maji maji meupe wanayajua wanawake hayaonekani katika hali hiyo; na kwa kuwa lau kingehesabiwa kuwa ni kutwaharika, basi yaliyo kabla yake yangekuwa hedhi moja, na yaliyo baada yake yangekuwa hedhi moja, na hakuna mwenye kauli hiyo; la sivyo, eda inayohesabiwa kwa mizunguko ya hedhi ingemalizika kwa siku tano. Na kwa kuwa lau kama lingewekwa kuwa ni twahara, lingesababisha tabu na ugumu wa kuoga na mengineyo kila baada ya siku mbili; na dhiki imeondoshwa katika Sheria hii, na sifa njema ni za Mwenyezi Mungu.

Na kilicho mashuhuri katika madhehebu ya Hanbali ni kwamba: Damu ni hedhi, na usafi ni twahara, isipokuwa endapo jumla ya vyote viwili itazidi kiwango cha juu cha hedhi; basi damu inayozidi huwa ni damu ya ugonjwa (Istihadhwa).25

Na amesema katika Al-Mughni: Inaelekea kwamba kukoma kwa damu kunapokuwa chini ya siku moja si twahara, kwa mujibu wa riwaya tuliyoitaja katika nifasi kwamba haizingatii kilicho chini ya siku moja; na hilo ndio sahihi -Mwenyezi Mungu akipenda-, kwani damu wakati mwingine hushuka na wakati mwingine hukoma. Na kuwajibisha kuoga kwa anayetwaharika saa baada ya saa ni tabu inayoondolewa; kwa kauli Yake Mtukufu:

﴿...وَمَا جَعَلَ عَلَيۡكُمۡ فِي ٱلدِّينِ مِنۡ حَرَجٖۚ...﴾

"Wala hakuweka juu yenu mambo mazito katika Dini." [Al-Hajj: 78], Akasema: Kwa msingi huu, kukatika kwa damu hakutakuwa chini ya siku moja ya twahara, isipokuwa aone kinachoashiria hilo, kama vile kukatika huko kukawa mwishoni mwa kawaida yake ya hedhi, au aone maji maji meupe.26 Mwisho wa kunukuu.

Hivyo, kauli hii ya Mwandishi wa al-Mughni iko katikati ya kauli mbili, na Mwenyezi Mungu ndiye Mjuzi zaidi wa lililo sahihi.

Aina ya tano: Ukavu wa damu kiasi kwamba mwanamke anaona unyevu tu. Hali hii ikiwa katika wakati wa hedhi au ikiambatana nayo kabla ya kutwaharika, basi ni hedhi; na ikiwa baada ya kutwaharika, si hedhi. Kwa sababu upeo wa hali yake ni kuhusishwa na maji ya njano na kahawia, na hii ndiyo hukumu yake.

 

Sura ya nne: Kuhusu Hukumu za Hedhi

Hukumu za Hedhi ni nyingi, zinazozidi ishirini; tutataja miongoni mwazo zile tunazoona kuwa zina umuhimu mkubwa; miongoni mwa hizo:

Kwanza: Swala: Basi haifai kwa mwenye hedhi kuswali, iwe ni faradhi au sunna, na swala hiyo haikubaliki kwake. Na vivyo hivyo swala si wajibu kwake isipokuwa akipata ndani ya wakati wake kiasi cha rakaa moja kamili; basi wakati huo inawajibika kwake swala, iwe ameipata hiyo mwanzoni mwa wakati au mwishoni mwake.

Mfano wa hilo mwanzoni mwake: Mwanamke akafikwa na hedhi baada ya kuzama jua kwa kiasi cha rakaa moja, basi itamuwajibikia akitwaharika kulipa swala ya Magharibi, kwa sababu aliupata muda wa swala hiyo kiasi cha rakaa moja kabla ya kuingiwa na hedhi.

Na mfano wa hilo kwa mwisho wakati wake: Mwanamke aliyetwaharika kutokana na hedhi kabla ya jua kuchomoza kwa kiasi cha rakaa moja, basi itamuwajibikia kulipa swala ya Alfajiri; kwa sababu ameupata wakati katika muda wake kiasi cha rakaa moja.

Ama ikiwa mwanamke ataupata muda wa swala kwa kiasi kisichotosheleza rakaa moja kamili, kama vile akaingia katika hedhi katika mfano wa kwanza muda mfupi tu baada ya kuzama jua, au atatwaharika katika mfano wa pili muda mfupi tu kabla ya kuchomoza jua, basi swala si wajibu juu yake; kwa mujibu wa kauli ya Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Atakaye idiriki rakaa katika swala basi amediriki swala." Wamekubaliana Bukhari na Muslim27, Maana yake ni kwamba mwenye kuipata chini ya rakaa moja ya swala hatakuwa amediriki swala.

Na ikiwa mwanamke atapata rakaa moja katika wakati wa swala ya Alasiri, je, inakuwa wajibu juu yake kuswali swala ya Adhuhuri pamoja na Alasiri? Au akipata rakaa moja katika wakati wa swala ya Ishaa, je, inakuwa wajibu juu yake kuswali swala ya Magharibi pamoja na Ishaa?

Katika hili kuna tofauti baina ya wanachuoni, na yaliyo sahihi nikwamba halazimiki isipokuwa swala alizozipata katika wakati wake; nazo ni swala ya Alasiri na Ishaa ambayo ni ya mwisho pekee; kwa kauli yake Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Mwenye kupata rakaa moja katika swala ya Alasiri kabla jua halijazama, basi kwa hakika atakuwa ameipata swala ya Alasiri". Wamekubaliana Bukhari na Muslim28, Hakusema Mtume -rehema na amani ziwe juu yake-: “Basi amediriki Adhuhuri na Alasiri.”

Na hakutaja ulazima wa swala ya Adhuhuri juu yake, na asili ni kutokuwa na dhima ya jambo, na huo ndio msimamo wa Abu Hanifa na Maliki, na hilo limetajwa kutoka kwao katika Sharh al-Muhadhdhab29.

Na ama dhikiri na takbira na tasbihi na tahmidi, na kutaja jina la Mwenyezi Mungu wakati wa kula na vinginevyo, na kusoma hadithi za Mtume na fiqhi, na dua na kuitikia dua kwa kusema Aamiin, na kusikiliza Qur’ani, basi si haramu kwake chochote miongoni mwa hayo, kwani imethibiti katika Sahihi mbili na vinginevyo. "Kwamba Mtume -rehema na amani ziwe juu yake- alikuwa akiegemea pajani kwa Aisha -radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake- naye akiwa katika hedhi, anasoma Qur'ani"30.

Na katika Sahihi mbili pia imekuja kwamba Ummu Atwiya, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alimsikia Mtume rehema na amani ziwe juu yake akisema: "Watoke wanawake walioachwa huru kutokana na utumwa, na mabinti wanaotawishwa, na wanawake wenye hedhi (yaani: kwenda katika swala za Iddi mbili), na wahudhurie kheri na dua ya Waumini, na wenye hedhi wajitenge na mahala pa kuswalia."31

Ama kusoma Qur'ani kwa mwanamke aliye katika hedhi yeye mwenyewe, ikiwa ni kwa kuitazama kwa macho au kutafakari kwa moyo bila kutamka kwa ulimi, basi hakuna tatizo katika hilo; kama vile kuwekwa Msahafu au ubao, kisha akatazama aya na akazisoma kwa moyo wake. Amesema Nawawi katika Sharh Al-Muhadhdhab: “Inajuzu pasina tofauti yoyote.”32.

Ama ikiwa kusoma kwake Qur'ani ni kwa kutamka kwa ulimi, basi wanazuoni wengi wanaona kuwa hilo limekatazwa na halijuzu kisheria. Na Bukhari33, Ibn Jarir at-Tabari34, na Ibnul-Mundhir35 wamesema: Inafaa.

Imenukuliwa kutoka kwa Maliki, na kutoka kwa Imamu Shafi katika kauli yake ya zamani36, na imenukuliwa hivyo kutoka kwao katika "Fath Al-Baari"37.

Na Bukhari ametaja kwa mu'allaq kutoka kwa Ibrahim an-Nakha'i: Hakuna ubaya kusoma aya38.

Na amesema Sheikhul-Islam Ibn Taimiyyah katika Fataawa, Majmuu'at Ibn Qasim: "Hakuna kabisa sunnah katika Qur’ani, inayomzuia kusoma,na kauli yake aliposema: “Mwenye hedhi wala mwenye janaba asisome chochote katika Qur’ani”39 Wanachuoni wa hadithi wamekubaliana kwamba hadithi hii ni dhaifu.40

Na wanawake walikuwa wakipata hedhi katika zama za Mtume -rehema na amani ziwe juu yake-; basi lau kama kusoma Qur'ani kungelikuwa ni haramu kwao kama swala, hilo lingelikuwa miongoni mwa mambo ambayo Mtume -rehema na amani ziwe juu yake- alioubanishia Umma wake, na Mama wa Waumini wangelijifunza hilo, na lingelikuwa miongoni mwa mambo waliyoyaeneza miongoni mwa watu. Basi kwa kuwa halikupokelewa kutoka kwa Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, katika hilo katazo, haijuzu kulifanya kuwa haramu pamoja na kujua kwamba hakulikataza; na kwa kuwa hakulikataza pamoja na wingi wa wenyekupatwa na hedhi katika zama zake, ikajulikana kuwa hilo si haramu.41 Mwisho wa nukuu.

Na lililo bora, baada ya kujua tofauti ya mitazamo ya wanachuoni, ni kusemwa: lililo bora kwa mwanamke mwenye hedhi ni asisome Qur'ani kwa kutamka kwa ulimi, isipokuwa pale panapokuwa na hitajio hilo, kama vile akiwa ni mwalimu wa kike akahitaji kuwasomesha wanafunzi wa kike, au katika hali ya mtihani ambapo mwanafunzi wa kike atahitaji kusoma kwa ajili ya mtihani wake, au mfano wa hayo.

Jambo la pili: Swaumu: Basi ni haramu kwa mwenye hedhi kufunga, iwe ya faradhi au ya sunna, na siyo sahihi akifunga katika hali hiyo; lakini analazimika kulipa swaumu ya faradhi miongoni mwa hizo; kwa ushahidi wa maneno ya Aisha - radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Tulikuwa tukipatwa na hilo - yaani: hedhi -, basi tunaamrishwa kulipa swaumu, na wala hatuamrishwi kulipa swala." Wamekubaliana Bukhari na Muslim42.

Akipata hedhi akiwa amefunga, basi swaumu yake itabatilika, hata ikiwa hilo limetokea kabla ya kuzama kwa jua kwa muda mfupi tu, na itamlazimu kuilipa siku hiyo ikiwa ni swaumu ya lazima. Ama akihisi kuja kwa damu ya hedhi kabla ya Magharibi lakini haikutoka isipokuwa baada ya Magharibi, basi funga yake imetimia na haibatiliki kwa kauli iliyo sahihi; kwa sababu damu iliyo ndani ya mwili haina hukumu ya kisheria.

Na kwa kuwa Mtume -rehema na amani ziwe juu yake- alipoulizwa kuhusu mwanamke anayeona katika ndoto yake kama aonavyo mwanaume: Je, inamlazimu kuoga? Akasema: "Ndio, iwapo mwanamke ataona maji".43 Akaifungamanisha hukumu kwa kuonekana kwa manii, si kwa kuhama kwake; vivyo hivyo hedhi, hathibiti hukumu zake isipokuwa kwa kuiona damu ya hedhi imetoka nje, si kwa kuhama kwake.

Alfajiri itakapochomoza akiwa katika hedhi, basi swaumu ya siku hiyo si sahihi kwake, hata kama atatwaharika mara tu baada ya Alfajiri.

Mwanamke akitwaharika kabla kidogo ya Alfajiri kisha akafunga, swaumu yake ni sahihi, hata kama hakuoga josho kubwa ila baada ya Alfajiri; kama aliyepatwa na janaba aliponuia kufunga akiwa na janaba, na hakuoga ila baada ya kuchomoza Alfajiri, basi swaumu yake ni sahihi. Katika hadithi ya Aisha -radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake- amesema: "Alikuwa Mtume rehema na amani ziwe juu yake anapoingia asubuhi akiwa na janaba lililotokana na tendo la ndoa si kwa ndoto, kisha anafunga katika Ramadhani. Wamekubaliana Bukhari na Muslim44.

Hukumu ya tatu: Kuizunguka Al-Ka'aba: Basi ni haramu kwake kuizunguka Al-Ka'aba, iwe ya faradhi au ya hiyari, na haisihi kwake. Ama yale yaliyosalia katika matendo kama Sa’ayi -kukimbia- baina ya Mlima Swafaa na Mar-waa, na kusimama Arafa, na kulala Muzdalifah na Mina, na kuipiga Jamarat kwa vijiwe, na mengineyo miongoni mwa matendo ya Hija na Umra, basi si haramu kwake. Kwa kauli ya Mtume rehema na amani ziwe juu yake kumwambia Aisha radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake alipoingia katika hedhi: "Fanya kama anavyofanya hujaji isipokuwa usizunguke Nyumba (Al-Ka'aba) hadi utakapokuwa safi."45.

Na juu ya hili, iwapo mwanamke atazunguka Kaaba hali ya kuwa ametwaharika, kisha ikamjia hedhi mara tu baada ya kumaliza kuzunguka Kaaba, au akiwa katika mzunguko wa Swafa na Marwa, basi hapana ubaya wowote juu ya hilo.

Hukumu ya nne: Anaondokewa na wajibu wa Tawafu ya kuaga: Iwapo mwanamke atakuwa amekamilisha ibada za Hija na Umra, kisha akapata hedhi kabla ya kuondoka kurejea kwao, na hedhi ikaendelea hadi wakati wa kuondoka kwake, basi atatoka bila Tawafu ya kuaga; Imepokelewa katika hadithi ya Bin Abbas -radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yao- amesema: "Watu waliamrishwa kwamba jambo lao la mwisho Makka liwe ni kuzunguka Nyumba tukufu, isipokuwa wanawake wenye hedhi walirahisishiwa katika hilo. (Hadithi hii wamekubaliana juu yake Bukhari na Muslim)46.

Haipendekezwi kwa mwenye hedhi wakati wa kuaga kuja katika mlango wa Msikiti Mtukufu na kuomba dua; kwa sababu hilo halikunukuliwa kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, na ibada zimejengeka juu ya yaliyonukuliwa. Bali yaliyopokelewa kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, yanathibitisha kinyume cha hilo; kwani katika kisa cha Safia -radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake- alipopata hedhi baada ya Tawaful-Ifadhwa, Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alimwambia: "Basi ondoka." Wamekubaliana Bukhari na Muslim47.

Wala hakuamrisha kuhudhuria mlangoni mwa msikiti; na lau hilo lingekuwa limewekwa kisheria angelibainisha hilo. Ama kuzunguka Kaaba kwa ajili ya Hija na Umra haliondoki kwake, bali atazunguka Kaaba atwaharikapo.

Hukumu ya tano: Kukaa ndani ya msikiti: Basi ni haramu kwa mwanamke mwenye hedhi kukaa ndani ya msikiti, hata eneo la kuswalia Idd ni haramu kwake kukaa humo. Katika hadithi ya Ummu Atwiya -radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake-: kwamba alimsikia Mtume -rehema na amani ziwe juu yake- akisema: "Watoke wasichana waliobalehe, walioko majumbani, na wenye hedhi."

Na katika riwaya hiyo: "Wenye hedhi wajitenge mbali na mahali pa kuswalia. Wamekubaliana Bukhari na Muslim48.

Hukumu ya sita: Kujamiiana: Basi ni haramu kwa mume wake kujamiiana naye, na ni haramu kwake kumruhusu afanye hivyo; kwa sababu ya kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu:

﴿وَيَسۡـَٔلُونَكَ عَنِ ٱلۡمَحِيضِۖ قُلۡ هُوَ أَذٗى فَٱعۡتَزِلُواْ ٱلنِّسَآءَ فِي ٱلۡمَحِيضِ وَلَا تَقۡرَبُوهُنَّ حَتَّىٰ يَطۡهُرۡنَۖ...﴾

"Na wanakuuliza juu ya hedhi. Waambie, huo ni uchafu. Basi jitengeni na wanawake wakati wa hedhi. Wala msiwaingilie mpaka wat'ahirike..." [Al-Baqara: 222] Na makusudio ya Hedhi: Ni muda wa hedhi na mahali pake, na mahali hapo ni tupu ya mwanamke. Na kwa kauli ya Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Fanyeni kila kitu isipokuwa tendo la ndoa."

Yaani: Jimai. Imepokelewa na Muslim49; Na kwa sababu waislamu wamekubaliana ya kuwa kumwingilia mwenye hedhi katika tupu yake ni haramu.

Si halali kwa mtu anayemuamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho kulifanya jambo hili ovu ambalo kukatazwa kwake kumethibitishwa na Qur’ani Tukufu na Sunna ya Mtume wake, rehema na amani ziwe juu yake, na makubaliano ya Waislamu; basi atakuwa miongoni mwa waliompinga Mwenyezi Mungu na Mtume wake, rehema na amani ziwe juu yake, na akafuata njia isiyokuwa ya Waumini. Amesema katika Al-Majmuu’ Sharhi Al-Muhadh-dhab (uk. 374, Juz. 2): Na amesema Imamu Shafy, Mwenyezi Mungu amrehemu: “Yeyote atakayefanya hivyo basi amefanya dhambi kubwa.” Wamesema wenzetu na wengine: “Atakayehalalisha kujamiiana na mwanamke mwenye hedhi uhukumiwa kuwa kafiri.” Mwisho wa maneno ya An-Nawawiy.

Imeruhusiwa kwake -na sifa njema ni za Mwenyezi Mungu- kufanya yanayoweza kupunguza matamanio yake bila ya tendo la ndoa, kama vile kumbusu, kumkumbatia na kumpapasa mwanamke katika sehemu zisizokuwa tupu; lakini lililo bora asimpapase katika sehemu za kuanzia kitovuni mpaka magotini isipokuwa akiwa nyuma ya kizuizi. Kwa kauli ya Aisha -radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake-: "Alikuwa Mjumbe wa Mwenyezi Mungu -rehema na amani ziwe juu yake- akiniamrisha najifunga kikoi, ananigusa na mimi nikiwa katika hedhi." Wamekubaliana Bukhari na Muslim50.

Hukumu ya saba: Talaka: Ni haramu kwa mume kumtaliki mwanamke mwenye hedhi katika kipindi cha hedhi yake; kwa kauli Yake Aliyetukuka:

﴿يَاأَيُّهَا النَّبِيُّ إِذَا طَلَّقْتُمُ النِّسَاء فَطَلِّقُوهُنَّ لِعِدَّتِهِنَّ...﴾

"Ewe Nabii! Mtakapo wapa talaka wanawake, basi wapeni talaka katika wakati wa eda zao..." [Attwalaaq: 1] Yaani: Katika hali watakayoianza kukaa eda inayohesabika wakati wa talaka, na hilo halitokei ila iwapo atamtaliki akiwa mjamzito au akiwa katika twahara isiyofuatana na kujamiiana. Kwa sababu akipewa talaka katika hali ya hedhi, haanzi kuhesabu eda; kwa kuwa hedhi ambayo alipewa talaka ndani yake haihesabiwi katika eda. Na akipewa talaka akiwa katika twahara baada ya kujamiiana, eda atakayoianza haijulikani; kwa kuwa haijulikani iwapo amepata mimba kutokana na kujamiiana huko, basi atakaa eda ya mimba, au kama hakupata mimba, atakaa eda ya hedhi. Basi ilipokosekana yakini kuhusu aina ya eda, ikawa ni haramu kwake kutoa talaka mpaka jambo libainike.

Basi kumtaliki mwenye hedhi wakati wa hedhi yake ni haramu kwa sababu ya Aya iliyotangulia. Na kwa yale yaliyothibiti katika Sahihi mbili (Bukhari na Muslim) na nyinginezo, kutokana na hadithi ya bin Omari, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba akamtaliki mkewe akiwa katika hedhi; basi Omari, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, akamtajia hilo Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, ndipo Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akaghadhibika juu ya hilo, akasema: "Mwambie amrejee, kisha abaki naye hadi atwaharike, kisha apate hedhi, kisha atwaharike; kisha akitaka amshikilie baada ya hapo, na akitaka amtaliki kabla hajamwingilia. Basi hiyo ndiyo eda ambayo Mwenyezi Mungu ameamuru wanawake wapewe talaka ndani yake."51

Na iwapo mume atamtaliki mkewe akiwa katika hedhi, basi amefanya dhambi, na inampasa atubu kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu, na amrudishe mkewe katika kifungo cha ndoa yake ili amtaliki kwa talaka ya kisheria inayoafikiana na amri ya Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Kisha baada ya kumrudisha, amwache hadi atakapopata twahara kutokana na hedhi ile aliyomtaliki ndani yake, kisha apate hedhi mara nyingine, kisha akitwaharika, akitaka abaki naye, na akitaka amtaliki kabla ya kumjamii.

Na vinavyotolewa nje ya katazo la kutoa talaka wakati wa hedhi ni masuala matatu:

Kwanza: Ikiwa talaka imetolewa kabla ya kumuingilia au kabla ya kujamiiana naye, basi hakuna ubaya kumtaliki akiwa katika hedhi. Kwa sababu wakati huo halazimiki kukaa eda, basi talaka yake haitakuwa kinyume; kwa sababu ya kauli yake:

﴿...فَطَلِّقُوهُنَّ لِعِدَّتِهِنَّ...﴾

"...wapeni talaka katika wakati wa eda zao..." [Attwalaaq: 1].

Jambo la pili: Ikiwa hedhi itakuwa wakati wa mimba, na sababu yake imekwishabainishwa.

Jambo la tatu: Ikiwa talaka ni kwa fidia, basi hakuna ubaya kumtaliki akiwa katika hedhi.

Mfano wa hilo ni pale panapokuwapo mgogoro na uhusiano mbovu baina ya mke na mume, kisha mume akachukua fidia kwa ajili ya kumtaliki; basi inaruhusiwa hata akiwa katika hedhi. Kutoka kwa bin Abbas radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yao kuwa mke wa Thabiti bin Kaisi bin Shamasi alimuendea Mtume rehema na amani ziwe juu yake, akasema: "Ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu, hakika mimi sina la kumlaumu juu yake katika tabia wala katika dini, lakini nachukia ukafiri katika Uislamu." Akasema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: “Je, utamrudishia Bustani yake?” Akasema: Ndiyo. Akasema Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Kubali Bustani na mpe talaka moja." Imepokelewa na Bukhari52.

Wala Mtume -rehema na amani ziwe juu yake- hakuuliza: Je, alikuwa katika hedhi au katika twahara? Na kwa kuwa talaka hii ni mke kuinunua nafsi yake, ikaruhusiwa inapohitajika iwe katika hali yoyote ile.

Amesema katika al-Mughni, akieleza sababu ya kujuzu kwa khul'u wakati wa hedhi (uk. 52, juzuu ya 7, toleo la Misri): “Kwa sababu kukatazwa talaka wakati wa hedhi ni kwa ajili ya madhara yanayompata kwa kurefuka eda; na khuluu (kujikomboa/kujivua) ni kwa ajili ya kuondoa madhara yanayompata kutokana na ubaya wa maisha ya ndoa na kuendelea kukaa na yule asiyempenda na kumchukia; na hilo ni kubwa zaidi kuliko madhara ya kurefuka kwa eda. Basi ikawa inaruhusiwa kuondoa madhara makubwa kwa kuvumilia lililo dogo; na kwa ajili hiyo Mtume rehema na amani ziwe juu yake hakumuuliza mwanamke aliyefanya khulu kuhusu hali yake.” Mwisho wa maneno yake.

Na ama kufunga ndoa na mwanamke aliye katika hedhi, hakuna ubaya katika hilo; kwa kuwa asili ni uhalali, na hakuna dalili ya kuzuia hilo. Lakini mumewe kuingiia kwake akiwa katika hedhi kunaangaliwa kwanza: Ikiwa kuna uhakika kwamba hatamuingilia, basi hakuna ubaya; vinginevyo, basi mume asiingie kwake hadi atwaharike kwa kuogopa kuangukia katika lile lililokatazwa.

Hukumu ya nane: Kuzingatia eda ya talaka ni kwa hilo — yaani hedhi-. Hivyo, akimtaliki mwanamume mkewe baada ya kujamiiana naye au kukaa naye faragha, basi mke huyo atalazimika kukaa eda ya hedhi tatu kamili, ikiwa ni miongoni mwa wanaopata hedhi, na wala si mwenye mimba; kwa kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

﴿وَٱلۡمُطَلَّقَٰتُ يَتَرَبَّصۡنَ بِأَنفُسِهِنَّ ثَلَٰثَةَ قُرُوٓءٖۚ...﴾

"Na wanawake walio achwa wangoje peke yao mpaka twahara (au hedhi) tatu zipite." [Al-Baqara: 228] Yaani: Hedhi tatu. Ikiwa ni mjamzito, basi eda yake ni hadi atakapojifungua, iwe muda huo ni mrefu au mfupi; kwa kauli Yake Aliyetukuka:

﴿...وَأُوْلَاتُ الأَحْمَالِ أَجَلُهُنَّ أَن يَضَعْنَ حَمْلَهُنَّ...﴾

"Na wenye mimba eda yao mpaka watakapo zaa." [At-Talaq: 4] Na iwapo atakuwa miongoni mwa wasioingia hedhi, kama msichana mdogo ambaye hajaingia katika hedhi, na yule ambaye damu yake ya hedhi imekatika kwa utu uzima, au kwa operesheni iliyoondoa mfuko wa uzazi, au kwa jambo jingine lolote ambalo halimpi tumaini la kurejea kwa hedhi, basi, eda yake ni miezi mitatu; kwa kauli Yake Aliyetukuka:

﴿وَاللَّائِي يَئِسْنَ مِنَ الْمَحِيضِ مِن نِّسَائِكُمْ إِنِ ارْتَبْتُمْ فَعِدَّتُهُنَّ ثَلَاثَةُ أَشْهُرٍ وَاللَّائِي لَمْ يَحِضْنَ...﴾

"Na wale waliokata tamaa kupata hedhi miongoni mwa wanawake wenu, ikiwa mnayo shaka, basi muda wa eda yao ni miezi mitatu, pamoja na ambao hawapati hedhi..." [At-Talaq: 4] Ikiwa ni miongoni mwa wanawake wenye hedhi, lakini hedhi yake imekatika kwa sababu inayojulikana kama ugonjwa au kunyonyesha, basi atabaki katika eda hata kama muda utarefuka mpaka hedhi irejee, na ataihesabu eda yake kwa hiyo hedhi. Ikiwa sababu imeondoka na hedhi haijarudi, kwa mfano amepona ugonjwa au amemaliza kunyonyesha, na hedhi ikaendelea kutokuwapo, basi atakaa eda ya mwaka mzima tangu kuondoka kwa sababu hiyo. Na kauli hii ndiyo sahihi, inayoafikiana na misingi ya sheria, Ikiwa sababu imeondoka na hedhi haijarejea, atakuwa kama yule ambaye hedhi yake imekatika bila sababu inayojulikana; na ikiwa hedhi yake imekatika bila sababu inayojulikana, basi atakaa eda mwaka mzima: Miezi tisa kwa ajili ya mimba kwa tahadhari, kwa sababu kawaida ya mimba ni miezi tisa, na miezi mitatu ya eda.

Ama ikiwa talaka imetolewa baada ya kufunga ndoa na kabla ya kujamiiana na kukaa faragha, basi halazimiki kukaa eda kabisa, si kwa hedhi wala kwa kinginecho; kwa sababu ya kauli yake:

﴿يَاأَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِذَا نَكَحْتُمُ الْمُؤْمِنَاتِ ثُمَّ طَلَّقْتُمُوهُنَّ مِن قَبْلِ أَن تَمَسُّوهُنَّ فَمَا لَكُمْ عَلَيْهِنَّ مِنْ عِدَّةٍ تَعْتَدُّونَهَا...﴾

"Enyi mlio amini! Mkiwaoa wanawake, Waumini, kisha mkawapa talaka kabla ya kuwagusa, basi hamna eda juu yao mtakayo ihesabu..." [Al Ahzaab: 49].

Hukumu ya tisa: Hukumu ya kubainika kwa tumbo la uzazi, yaani kuwa halina mimba. Hili huhitajika kila mara panapohitajika hukumu ya kubainika kwa tumbo la uzazi kuwa halina mimba, nalo lina masuala kadhaa:

Miongoni mwa hayo: Ikiwa mtu atakufa na akaacha mwanamke ambaye mtoto aliye tumboni mwake atamrithi, naye ana mume, basi mumewe hairuhusiwi kumwingilia mpaka apate hedhi, au kubainike kuwa ana mimba. Iwapo itabainika kuwa ana mimba, tunahukumu kwamba mtoto aliye tumboni atarithi, kwa kuwa tunahukumu kuwepo kwake wakati wa kufa kwa aliyemuachia urithi. Na akipata hedhi, tunahukumu kwamba hatarithi, kwa kuwa tunahukumu kuwa tumbo la uzazi halina mimba kwa hedhi.

La kumi ni uwajibu wa kuoga: Inawajibika kwa mwanamke mwenye hedhi akitwaharika aoge kwa kuuosha mwili wote; Kwa kauli ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, aliyoisema kwa Fatma bint Abii Qubaishi: "Inapokuja hedhi basi acha swala, na inapokwisha basi oga na swali." Imepokelewa na Bukhari53.

Na kiwango cha chini cha wajibu katika kuoga ni kuosha mwili wake wote hata kilicho chini ya nywele, na lililo bora nikuwa lifanyike kwa namna ilivyokuja katika hadithi. Imepokelewa kutoka kwa Mtume -rehema na amani ziwe juu yake- kwamba Asmaa binti Shakal alimuuliza kuhusu kuoga baada ya hedhi, akasema -rehema na amani ziwe juu yake-: “Mmoja wenu achukue maji yake na mkunazi wake, ajitwaharishe na aikamilishe twahara yake vyema, kisha ajimwagie maji kichwani na akisugue kichwa chake msuguo wa nguvu mpaka atakapohisi kuwa maji yamefika katika maoteo ya nywele za kichwa chake, kisha ajimwagie maji juu ya mwili wake, kisha achukue kipande cha kitambaa chenye misk, ajitwaharisha nacho.” Basi akasema Asmaa: Ni vipi atajitwaharisha kwayo? Basi akasema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Sub-haana llaah!" Ametakasika Mwenyezi Mungu. Aisha akasema kumwambia: Fuatilia athari ya damu. [Imepokelewa na Muslim]54.

Si wajibu kufumua nywele za kichwa, isipokuwa ikiwa zimefungwa kwa nguvu kiasi cha kuhofiwa kwamba maji hayatafika kwenye mizizi ya nywele. Kwa yaliyomo katika Sahihi Muslim, kutoka kwa hadithi ya Ummu Salama radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake kwamba alimwuliza Mtume Rehema na amani ziwe juu yake, akasema: “Mimi ni mwanamke ninasokota nywele za kichwa changu kwa kuzibana; je, nizifungue kwa ajili ya Ghuslu ya janaba?” Na katika riwaya nyingine: “kwa ajili ya hedhi na janaba?” Akasema: "Hapana, inakutosha tu uchote maji kwa viganja vyako mara tatu uyamimine juu ya kichwa chako, kisha ujimwagie maji katika mwili wako nawe utakuwa msafi."55

Atakapotwaharika mwenye hedhi katikati ya wakati wa swala, inawajibika kwake aharakishe kuoga josho kubwa ili apate kuiswali katika wakati wake. Basi ikiwa yuko katika safari na hana maji, au akawa ana maji lakini anahofia madhara kwa kuyatumia, au akawa ni mgonjwa anayedhurika kwa maji, basi atatayamamu badala ya kuoga josho kubwa mpaka kizuizi kiondoke, kisha aoge josho kubwa.

Na baadhi ya wanawake hutwaharika ndani ya wakati wa swala, na huchelewesha kujitwaharisha kwa kuoga hadi muda mwingine, wakisema: Haiwezekani kwao kukamilisha kule kutwaharika kunakotakiwa katika wakati huu; lakini hilo si hoja wala udhuru. Kwa sababu mwanamke anaweza kujitosheleza na kile cha wajibu tu katika kuoga, na aswali swala ya faradhi katika wakati wake, kisha atakapopata wasaa aoge kwa ukamilifu.

Sura ya tano: Katika Damu ya Ugonjwa, na hukumu zake.

Damu ya ugonjwa ni: Mwanamke kuendelea kutoka damu kiasi kwamba haikomi kabisa, au hukatika kwa muda mfupi kama siku moja au siku mbili ndani ya mwezi.

Basi dalili ya hali ya kwanza ambayo damu haikatiki kabisa ni yaliyothibiti katika Sahihi Bukhari kutoka kwa Aisha, Mwenyezi Mungu amridhie, amesema: Fatma binti Abii Qubaishi alimwambia Mtume -rehema na amani ziwe juu yake-: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, hakika mimi sipati twahara". Na katika riwaya nyingine: "Ninapata damu ya istihadha, hivyo siwi safi."56

Na dalili ya hali ya pili ambayo damu haikatiki isipokuwa kidogo ni hadithi ya Hamnah bint Jah'shi -radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake- ambapo alikuja kwa Mtume -rehema na amani ziwe juu yake- akasema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu -rehema na amani ziwe juu yake-, hakika mimi hupatwa na hedhi ya ugonjwa kwa wingi tena kali. [Hadithi hii... Ameipokea Ahmad, Abuu Daud na Tirmidhiy57; na Tirmidhiy akaisahihisha, na imenukuliwa kutoka kwa Imamu Ahmad kuwa aliisahihisha, na kutoka kwa Bukhariy kuwa aliihukumia kuwa hasan58.]

Hali za damu ya ugonjwa:

Kwa mwanamke mwenye damu ya ugonjwa zipo hali tatu:

Hali ya kwanza: Awe na hedhi inayojulikana kabla ya kuanza kwa damu ya ugonjwa; basi huyu atarejea kwenye muda wa hedhi yake uliokuwa ukijulikana uliotangulia, atakaa humo, haswali wala hafungi, na zitamhusu hukumu za hedhi, na iliyobaki baada ya hapo itakuwa ni damu ya ugonjwa, hivyo zitamhusu hukumu za mwenye damu ya ugonjwa.

Mfano wake ni mwanamke ambaye ilikuwa kawaida yake anapata hedhi katika mwanzo wa kila mwezi kwa muda wa siku sita, kisha akapatwa na damu ya ugonjwa ikawa damu inaendelea kutoka mfululizo, basi hedhi yake ni siku sita za mwanzo wa kila mwezi, na kinachozidi hiyo ni damu ya ugonjwa. Kutoka kwa Aisha -radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake- yakwamba Fatuma bint Abii Hubaishi alisema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, hakika mimi napata hedhi na wala sitwahariki, je niache swala? Akasema: "Hapana, hakika huo ni upasukaji wa mshipa, lakini acha swala kwa kiasi cha siku ulizokuwa ukipata hedhi ndani yake, kisha oga na uswali." Imepokelewa na Bukhari59.

Na katika Sahihi Muslim, kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alimwambia Ummu Habiba bint Jahsh, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Kaa kiwango cha siku ambazo ilikuwa ikikuzuia hedhi yako, kisha oga na swali.60

Kwa msingi huo, mwenye damu ya ugonjwa ambaye ana hedhi inayojulikana atakaa kwa kiwango cha siku za hedhi yake pekee, kisha ataoga, na ataswali, wala asijali damu hiyo wakati huo.

Hali ya pili: Asiwe na hedhi yenye ada iliyojulikana kabla ya damu ya ugonjwa; yaani damu ya ugonjwa imeendelea kwake tangu mwanzo kabisa alipoanza kuona damu. Basi huyu atatumia utambuzi; hedhi yake itakuwa ni ile inayotambulika kwa rangi yake nyeusi au kwa uzito wake au kwa harufu yake, nayo itakuwa na hukumu za hedhi; na kilichobaki kitakuwa ni damu ya ugonjwa yenye hukumu za damu ya ugonjwa.

Mfano wa hilo ni: Mwanamke alipoona damu mara ya kwanza, ikaendelea damu kushuka kwake; lakini anaiona siku kumi ikiwa nyeusi, na siku zilizobaki za mwezi ikiwa nyekundu; au anaiona siku kumi ikiwa nzito, na siku zilizobaki za mwezi ikiwa nyepesi; au anaiona siku kumi ikiwa na harufu ya hedhi, na siku zilizobaki za mwezi bila harufu. Basi hedhi yake ni ile nyeusi katika mfano wa kwanza, na ile nzito katika mfano wa pili, na ile yenye harufu katika mfano wa tatu, na nyingine zote ni damu za ugonjwa. Kwa kauli ya Mtume -rehema na amani ziwe juu yake- kumwambia Fatma bint Abii Qubaishi: Ikiwa damu ya hedhi ni nyeusi inayotambulika, basi ikitokea hivyo acha swala; na ikiwa ni ile nyingine basi tawadha na swali; kwani hiyo ni damu ya mshipa. Ameipokea Abu Daud na An-Nasaai, na ameisahihisha Ibn Hibbaan na Al-Haakim61.

Na hadithi hii, ijapokuwa katika Isnad (wapokezi) wake na Matini yake kuna mjadala, basi wasomi -Mwenyezi Mungu awarehemu- wameifanyia kazi, na hilo ndilo lililo bora kuliko kuirejesha katika ada ya wanawake wengi.

Hali ya tatu: Asiwe na ada ya hedhi inayojulikana, wala asiwe na utofautishaji unaofaa kwa sifa za damu; yaani damu ya ugonjwa iendelee kushuka tangu alipoanza kuona damu, na damu yake sawa iwe ina sifa moja au ina sifa zisizo thabiti ambazo haziwezi kuwa hedhi, hivyo mwanamke huyu atafanya kwa kuzingatia desturi ya wanawake wengi; basi hedhi yake itakuwa siku sita au saba katika kila mwezi, ikianza tangu mwanzo wa kipindi alipoanza kuona damu, na kilichozidi hapo si hedhi bali ni damu ya ugonjwa wa kutokwa na damu.

Mfano wa hilo ni kwamba aone damu mara ya kwanza anapoiona katika siku ya tano ya Mwezi, nayo ikaendelea kumtoka bila kuwepo dalili ya kuitofautisha kuwa ni hedhi, si kwa rangi wala kwa kinginecho; hivyo hedhi yake katika kila Mwezi itakuwa siku sita au saba, ikianza kuanzia siku ya tano ya kila Mwezi; Kwa hadithi ya Hamna bint Jahshi -radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake- kwamba alisema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, hakika mimi napata damu ya ugonjwa nyingi tena nzito sana, unaonaje kuhusu hilo? Imekuwa imenizuia swala na saumu. Akasema Mtume -rehema na amani ziwe juu yake-: "Nitakuelezea namna ya kutumia (Kursuf) yaani; pamba: uiweke kwenye sehemu ya siri, kwani huizuia damu." Aisha akasema: Ni zaidi ya hizo. Na katika riwaya hiyo akasema: "Hakika huu ni mwendo wa shetani miongoni mwambio zake, basi kaa hedhi siku sita au saba, kwa elimu ya Mwenyezi Mungu Aliyetukuka, kisha oga, mpaka utakapoona kuwa umetwaharika na kuwa msafi kabisa, basi swali siku ishirini na nne au ishirini na tatu, na funga." Hadithi. [Imepokelewa na Ahmad, Abu Dawud na At-Tirmidhi, na At-Tirmidhi akaisahihisha62, na imenukuliwa kutoka kwa Ahmad kuwa aliisahihisha, na kutoka kwa Bukhari kuwa aliihukumia kuwa nzuri (Hasan)]63.

Na kauli ya Mtume – Rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake –: “siku sita au saba” si kwa hiari, bali ni kwa ajili ya ijtihadi; basi aangalie lililo karibu zaidi na hali yake miongoni mwa wanaofanana naye kimaumbile na waliokaribiana naye umri na undugu, na lililo karibu zaidi na hedhi kutokana na damu yake, na mambo mengineyo ya kuzingatiwa mfano wa hayo. Ikiwa jambo lililo karibu zaidi ni kuwa siku sita, basi atazifanya kuwa sita; na ikiwa jambo lililo karibu zaidi ni kuwa saba, atazifanya kuwa saba.

Hali ya anayefanana na mwenye damu ya ugonjwa (Istihadha):

Huenda mwanamke akapatwa na sababu inayosababisha kutokwa na damu nyingi kutoka katika tupu yake, kama vile upasuaji katika mfuko wa uzazi au katika sehemu zilizo chini yake; na hali hii ina aina mbili:

Aina ya kwanza: Ijulikane kuwa hawezi kupata hedhi baada ya upasuaji, kama vile kufanyiwa upasuaji wa kuondolewa mfuko wa uzazi kwa ukamilifu au kuzibwa kiasi kwamba damu haitoki humo. Basi mwanamke huyu hazimhusu hukumu za mwenye ugonjwa wa kutokwa na damu, bali hukumu yake ni hukumu ya yule anayeona rangi ya manjano au kahawia au unyevu baada ya kutwaharika: Hataziacha swala wala swaumu, wala haizuiliwi kuingiliwa na mume wake, na josho kubwa si wajibu kwa damu hii. Hata hivyo, inamlazimu wakati wa swala aioshe damu, na afunge kitambaa au mfano wake katika sehemu ya siri ili kuzuia kutoka kwa damu, kisha atatawadha kwa ajili ya swala, wala hatatawadha kwa ajili yake ila baada ya kuingia wakati wake iwapo ina wakati kama zile swala tano; na kama haina wakati, basi atatawadha anapotaka kuswali kama swala za sunna za jumla.

Aina ya pili: Isijulikane kuwa hedhi yake itakatika baada ya upasuaji, bali inawezekana apate hedhi; basi huyu hukumu yake ni hukumu ya mwenye damu ya ugonjwa. Na dalili ya yaliyotajwa ni kauli yake -rehema na amani ziwe juu yake- kwa Fatuma binti Abii Hubaishi: "Hakika hiyo ni damu ya mshipa tu, si damu ya hedhi; basi ikianza hedhi, acha swala."64

Kwa hakika kauli yake Mwenyezi Mungu: "Basi itakapokuja hedhi" Inabainisha kwamba hukumu ya mwenye damu ya ugonjwa ni kwa yule mwenye hedhi inayowezekana, inayokuja na kuondoka; ama yule asiye na hedhi inayowezekana, basi damu yake ni damu ya mshipa katika hali zote.

Hukumu za damu ya ugonjwa:

Tumekwisha kujua kutokana na yaliyotangulia ni lini damu huwa hedhi na ni lini huwa damu ya ugonjwa; basi inapokuwa hedhi, huthibiti kwake hukumu za hedhi, na inapokuwa damu ya ugonjwa, huthibiti kwake hukumu za damu ya ugonjwa.

Imeshatangulia kutajwa mambo muhimu miongoni mwa hukumu za hedhi.

Na kuhusu hukumu za istihaadha (damu ya ugonjwa), ni kama hukumu za twahara; basi hakuna tofauti kati ya mwenye istihaadha na wanawake waliotwaharika, isipokuwa katika haya yafuatayo:

La kwanza: Wajibu wa kushika udhu juu yake kwa kila Swala, Kwa kauli ya Mtume -rehema na amani ziwe juu yake- aliyoisema kumwambia Fatma bint Abii Qubaishi: "Kisha tawadha kwa kila swala." Imepokelewa na Bukhari katika mlango wa kuosha damu. Maana yake ni kwamba: Hatachukua udhu kwa ajili ya swala ya wakati maalumu ila baada ya kuingia wakati wake. Ama ikiwa swala hiyo si ya wakati maalumu, basi atatawadha kwa ajili yake pindi atakapotaka kuiswali.

Pili: Mwanamke akitaka kutawadha basi aoshe athari ya damu, na ajifunge juu ya sehemu ya siri kitambaa juu ya pamba ili damu idhibitiwe; kwa kauli ya Nabii, rehema na amani zimshukie, kwa Hamnah: "Ninakupendekezea pamba; kwani huzuia damu". Akasema: Kwa hakika damu ni nyingi kuliko hivyo. Akasema: "Basi vaa nguo (ya kuzuia damu)". Akasema: Ni nyingi zaidi kuliko hivyo. Akasema: "Basi jitie hatamu (yaani: Jifunge nguo kwa nguvu ili kuizuia damu)". Hadi mwisho wa Hadithi hii, Wala haitamdhuru chochote kitakachotoka baada ya hayo; kwa sababu ya kauli ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, aliyoisema kumwambia Fatma Bint ya Abi Hubaysh: "Acha swala siku za hedhi yako, kisha oga na tawadha kwa kila swala, kisha swali, hata kama damu ikidondoka juu ya mkeka." [Imepokelewa na Ahmad na Ibin Maajah]65.

Ya tatu: Kujamiiana. Wanazuoni wamekhitalifiana kuhusu kujuzu kwake ikiwa haogopi kuangukia dhiki ya kijinsia kwa kuacha kwake, na kauli sahihi ni kujuzu kwake kabisa; kwani wanawake wengi, hadi kufikia kumi au zaidi, walipatwa na damu ya istihadhi katika zama za Nabii - rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake - na Mwenyezi Mungu wala Mtume Wake hawakukataza kujamiiana nao. Bali katika kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

﴿...فَاعْتَزِلُواْ النِّسَاء فِي الْمَحِيضِ...﴾

"...jitengeni na wanawake wakati wa hedhi..." [Al-Baqara: 222] Ni dalili kwamba si wajibu kujitenga nao katika mengineyo; na kwa kuwa swala inajuzu kwake, basi jimai ni jambo lenye unafuu zaidi. Na kulinganisha kwa qiyasi (kupima) kujamiana naye na kujamiana na mwanamke mwenye hedhi si sahihi; kwa kuwa viwili hivyo havilingani hata kwa wale wanaosema kuwa ni haramu, na qiyasi haiwi sahihi penye tofauti ya msingi.

Sura ya sita: Kuhusu Nifasi na hukumu yake.

Nifasi: Ni Damu inayotoka kwa sababu ya kujifungua; inaweza kutoka pamoja na kujifungua, au baada yake, au siku mbili au tatu kabla yake ikiwa imeambatana na uchungu wa kujifungua.

Na amesema Sheikhul-Islaam Ibnu Taimiyya: "Damu atakayoiona mjamzito anapoanza uchungu wa kujifungua, basi hiyo ni damu ya Nifasi. Wala hakuiwekea mpaka wa siku mbili au tatu; na makusudio yake ni uchungu wa kujifungua unaofuatwa na kuzaa, la sivyo si damu ya Nifasi. Na wanazuoni wamehitilafiana: je, damu ya Nifasi ina mpaka katika uchache wake na wingi wake? Amesema Shaykh Taqiyyu-d-Din (Mwenyezi Mungu amrehemu) katika risala yake kuhusu majina ambayo Muweka Sheria amezihusisha nazo hukumu (uk. 37): “Na Nifasi haina mipaka ya uchache wala ya wingi wake. Hivyo ikikadiriwa kwamba mwanamke ameona damu zaidi ya siku arobaini au sitini au sabini kisha ikakatika, basi hiyo ni nifasi; lakini ikiwa itaendelea mfululizo (bila kukatika) basi hiyo ni damu ya ugonjwa (Istihadhwa). Na wakati huo, mpaka ni siku arobaini, kwani huo ndio mwisho wa kilichozoeleka, kama ilivyopokelewa katika athari.” Mwisho wa maneno yake.

Nikasema: Na kwa msingi huu, ikizidi damu ya nifasi yake siku arobaini, na ikiwa ana ada ya kukatika baada ya hapo, au zikaonekana alama za kukaribia kukatika, atasubiri mpaka ikatike; la sivyo ataoga josho kubwa anapokamilisha siku arobaini, kwa kuwa hilo ndilo la kawaida, isipokuwa ikipatana na muda wa hedhi yake basi atakaa mpaka uishe muda wa hedhi. Ikikatika baada ya hapo, inapaswa kuchukuliwa kuwa ndiyo ada yake, hivyo atatenda kwa mujibu wake katika siku za usoni; na ikiendelea basi atakuwa ni mwenye damu ya ugonjwa, na atarejea kwenye hukumu za mwenye damu ya ugonjwa zilizotangulia. Na pindi akitwaharika kwa kukatika ile damu kutoka kwake basi atakuwa twahara, hata kabla ya siku arobaini; basi ataoga josho kubwa, ataswali, atafunga, na ataingiliwa na mumewe; isipokuwa iwapo kukatika huko ni chini ya siku moja, basi kukatika huko hakuzingatiwa. Amesema hivyo katika Al-Mughni66.

Na haithibiti damu ya uzazi (nifasi) isipokuwa akizaa kilichobainika umbile la mwanadamu; hivyo akitoa mimba ndogo ambayo ndani yake halijabainika umbile la mwanadamu, basi damu yake si damu ya uzazi (nifasi), bali ni damu ya mshipa, na hukumu yake itakuwa hukumu ya mwenye istihada. Na muda mchache unaobainika umbile la mwanadamu ni siku themanini kuanzia mwanzo wa mimba, na mara nyingi ni siku tisini.

Amesema Al-Majd Ibn Taimiyyah: Basi pindi atakapoona damu siku moja pamoja na uchungu wa uzazi kabla ya kujifungua, asilitilie maanani hilo; na baada ya kujifungua hatoswali wala hatofunga. Kisha ikidhihiri baada ya kujifungua kuwa jambo liko kinyume na dhahiri, atarejea na kulipa. Na ikiwa halikudhihiri, basi hukumu ya dhahiri itaendelea, wala hakuna kulipa. Ameinukuu hivyo katika Sharh al-Iqna’67.

Hukumu za Nifasi:

Hukumu za Nifasi ni kama Hukumu za Hedhi sawa kwa sawa, isipokuwa katika haya yafuatayo:

Kwanza: Eda huhesabiwa kwa kuzingatia talaka wala si kwa nifasi; kwa sababu ikiwa talaka imetolewa kabla ya kujifungua, eda humalizika kwa kujifungua si kwa nifasi, na ikiwa talaka imetolewa baada ya kujifungua, atasubiri kurejea kwa hedhi kama ilivyotangulia.

Jambo la pili: Muda wa hedhi huhesabiwa ndani ya muda wa ilaa (kiapo cha kutomuingilia mwanamke), wala muda wa nifasi hauhesabiwi ndani yake.

Na Kujiapiza ni mume kuapa kuacha kumuingilia mkewe kabisa, au kwa muda unaozidi miezi minne. Basi akisha apa, na mkewe akamtaka kujamiiana, atapewa muda wa miezi minne katika kiapo chake kuanzia alipoapa. Muda huo ukikamilika, atalazimishwa kujamiiana au kuachana (talaka) kwa ombi la mke. Na ndani ya muda huu, mwanamke akipatwa na nifasi, haitahesabiwa juu ya mume, bali itaongezewa juu ya miezi minne kwa kadiri ya muda wake. Tofauti na hedhi, kwani muda wake unahesabiwa juu ya mume.

Ya tatu: Balehe hupatikana kwa hedhi na haipatikani kwa damu ya uzazi; kwa sababu mwanamke hawezi kupata ujauzito mpaka atokwe na manii, hivyo balehe hupatikana kwa kutokwa na manii kulikotangulia ujauzito.

La nne: Kwamba damu ya hedhi ikikatika, kisha ikarejea ndani ya ada yake ya kawaida, basi hiyo ni hedhi kwa yakini; mfano, ada yake ikiwa ni siku nane, akaona damu ya hedhi siku nne, kisha ikakatika siku mbili, kisha ikarejea siku ya saba na ya nane, basi hiyo iliyorejea ni hedhi kwa yakini na zinathibiti kwake hukumu za hedhi. Ama damu ya uzazi, ikikatika kabla ya siku arobaini kisha ikarudi ndani ya siku arobaini, basi damu hiyo ni ya shaka; hivyo itamlazimu aswali na afunge faradhi za wakati wake katika wakati wake, na itaharamika kwake yale yanayoharamika kwa mwenye hedhi isipokuwa yale ya wajibu. Na baada ya kutwaharika atalipa yale aliyoyafanya katika kipindi cha damu hii miongoni mwa yale ambayo humlazimu mwenye hedhi kulipa. Hili ndilo lililo mashuhuri kwa wanazuoni wa fiqhi wa madhehebu ya Hanbali68.

Kauli iliyo sahihi ni kwamba damu ikimrudia katika muda unaowezekana kuwa Nifasi, basi hiyo ni Nifasi; vinginevyo ni Hedhi, isipokuwa damu hiyo ikiendelea kumtoka bila kukoma, basi itakuwa damu ya ugonjwa.

Na hili liko karibu na alichokinukuu katika (Al-Mughni)69 kutoka kwa Imam Maliki, Mwenyezi Mungu amrehemu, ambapo alisema: Na Maliki akasema: Pindi mwanamke atakapoona damu baada ya siku mbili au tatu — yaani baada ya kukatika damu hiyo — basi damu hiyo ni damu ya uzazi (Nifasi), na sivyo hivyo basi ni hedhi. Na huo ndio muktadha wa uchaguzi wa Sheikhul-Islaam Ibnu Taimiyya, Mwenyezi Mungu amrehemu.

Si kwamba katika masuala ya damu kuna jambo la shaka kwa hali halisi; lakini shaka ni jambo linalotegemea hali, watu hutofautiana kwayo kulingana na elimu zao na ufahamu wao. Na Kitabu na Sunna vina ufafanuzi wa kila jambo. Na Mwenyezi Mungu hakumwajibisha yeyote afunge mara mbili, au afanye tawafu mara mbili, isipokuwa pale ambapo ya kwanza ilipata hitilafu isiyoweza kurekebishwa ila kwa kulipa. Ama pale mja anapotekeleza katika yale aliyobebeshwa kisheria kile anachoweza kulingana na uwezo wake, basi dhamana yake imeondoka, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu:

﴿لَا يُكَلِّفُ ٱللَّهُ نَفۡسًا إِلَّا وُسۡعَهَاۚ...﴾

"Mwenyezi Mungu haikalifishi nafsi yoyote ila kwa kadiri ya iwezavyo..." [Baqara: 286] Na alisema:

﴿فَٱتَّقُواْ ٱللَّهَ مَا ٱسۡتَطَعۡتُمۡ...﴾

"Basi mcheni Mwenyezi Mungu kadiri muwezavyo..." [At-Taghabun: 16].

Tofauti ya tano baina ya Hedhi na Nifasi: Katika Hedhi, ikiwa atatwaharika kabla ya ada yake ya hedhi inafaa kwa mume wake kumuingilia, na hilo si jambo linalochukiza; ama katika Nifasi, akitwaharika kabla ya siku arobaini, basi kumuingilia kunachukiza kwa mume wake kwa mujibu wa kauli mashuhuri katika madhehebu, na lililo sahihi ni kwamba haichukizi kwake kumuingilia. Na hiyo ndiyo kauli ya jopo la Wanazuoni; kwasababu kuchukiza ni hukumu ya kisheria inayohitaji dalili ya kisheria. Wala hakuna katika swala hili ila kile alichokitaja Imamu Ahmad kutoka kwa Othman bin Abil Aswi kwamba alimjia kabla ya arobaini, akasema: Usinikaribie70.

Hili halilazimishi kuwa ni jambo la kuchukiza (makruhu); kwa kuwa huenda ikawa ni kwa njia ya tahadhari kwa hofu ya kwamba hakuwa na uhakika wa kutwaharika, au kwamba damu inaweza kuanza kutoka kwa sababu ya kuingiliwa, au kwa sababu nyinginezo. Na Mwenyezi Mungu ndiye Mjuzi zaidi.

Sura ya saba: Katika matumizi ya yale yanayozuia hedhi au yanayoileta, na yanayozuia ujauzito au yanayosababisha mimba kutoka

Inajuzu kwa mwanamke kutumia kinachozuia hedhi yake kwa masharti mawili:

La kwanza: Kusiwe na hofu ya madhara juu yake; iwapo itahofiwa madhara juu yake kutokana na hilo, basi hairuhusiwi, kwa kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu:

﴿...وَلَا تُلۡقُواْ بِأَيۡدِيكُمۡ إِلَى ٱلتَّهۡلُكَةِ...﴾

"...wala msijitie kwa mikono yenu katika maangamizo..." [Al-Baqarah: 195]

﴿...وَلَا تَقۡتُلُوٓاْ أَنفُسَكُمۡۚ إِنَّ ٱللَّهَ كَانَ بِكُمۡ رَحِيمٗا﴾

"...Wala msijiuwe. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuwaoneahuruma" [An Nisaai: 29].

La pili: Liwe hilo kwa idhini ya mume, kama linamhusu; kama vile akiwa katika eda kutoka kwake kwa namna ambayo matumizi yake yanakuwa wajibu juu yake, kisha akatumia kinachozuia hedhi ili airefushe eda na matumizi yake yaongezeke juu yake. Basi hairuhusiwi kwake kutumia kinachozuia hedhi wakati huo isipokuwa kwa idhini yake. Vile vile, ikithibitika kwamba kuzuia hedhi kunazuia mimba, basi hapana budi ya ruhusa ya mume; na ikithibitika kuwa inafaa, lililo bora ni kutoitumia, isipokuwa kwa haja; kwasababu kuiacha hali ya asili kama ilivyo ni karibu zaidi na kutengamaa kwa afya, na pia usalama.

Ama kuhusu kutumia vitu vinavyoleta hedhi, inajuzu kwa masharti mawili pia:

Ya kwanza: Usifanye hila kwamatumizihayo ili kuangusha wajibu; kama vile kufanya hivyo panapokaribia Ramadhani kwa ajili ya kuvunja funga, au kuiondosha swala kwayo, na kadhalika.

Jambo la pili: Hilo liwe kwa idhini ya mume wake; kwa sababu kupatikana kwa hedhi humzuia kustarehe naye kikamilifu, hivyo hairuhusiwi kutumia chochote kinachozuia haki yake ila kwa ridhaa yake. Na hata akiwa amepewa talaka, basi katika hilo kuna kuharakisha kuondoka kwa haki ya mume ya kumrejea, ikiwa ana haki hiyo.

Na ama matumizi ya kile kinachozuia mimba, yako katika aina mbili:

Ya kwanza: Kuzuia uzazi kwa kudumu; hili hairuhusiwi, kwa sababu huzuia upatikaji wa mimba na hivyo hupunguza kizazi, nalo ni kinyume na lengo la Mwenyezi Mungu la kuzidisha umma wa Kiislamu; pia kwa kuwa hakuna uhakika kwamba watoto wake waliopo hawatafariki, akabaki mjane asiye na watoto.

Jambo la pili: Kuzuia mimba kwa muda tu; kama pale mwanamke anapokuwa ni wa kupata mimba mara kwa mara, na mimba humchosha, hivyo hupenda kupanga uzazi wake ili apate mimba mara moja kila baada ya miaka miwili, au mfano wake; basi hilo ni jambo linaloruhusiwa, kwa sharti kwamba mumewe akubalie hilo, na wala lisilete madhara kwake. Na dalili ya hilo ni kuwa Maswahaba — radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yao — walikuwa wakifanya al-azl na wake zao katika zama za Mtume – rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake – ili wake zao wasipate mimba71, wala hawakukatazwa hilo, na al-azl ni kuwa mtu afanye jimai na mkewe kisha ajitoe wakati wa kumwaga manii akayamwaga nje ya tupu.

Ama matumizi ya vitu vinavyoporomosha mimba, yako katika aina mbili:

Jambo la Kwanza: Akikusudia kwa kuishusha mimba kuiangamiza, basi ikiwa hilo ni baada ya kupuliziwa roho ndani yake; ni haramu, bila shaka; na hilo ni kuua nafsi iliyoharamishwa bila haki, na kuua nafsi iliyoharamishwa ni haramu kwa Kitabu na Sunna na kwa makubaliano ya Waislamu. Na ikiwa ni kabla ya roho kupulizwa ndani yake, basi wanazuoni wametofautiana kuhusu uhalali wa jambo hilo: Miongoni mwao wapo walioliruhusu, na miongoni mwao wapo waliolikataza, na miongoni mwao wapo waliosema: linaruhusiwa madamu halijawa pande la damu; yaani, madamu hazijapita juu yake siku arobaini; na miongoni mwao wapo waliosema: linaruhusiwa madamu bado halijadhihiri ndani yake umbile la mwanadamu.

Na lililo salama zaidi ni kuzuia kuiondoa mimba isipokuwa kwa haja, kama vile mama akiwa mgonjwa asiyestahamilia ujauzito au mfano wa hivyo; basi inajuzu kuiondoa wakati huo, isipokuwa ikiwa umepita muda ambao inawezekana kubainika umbile la mwanadamu, hapo inakatazwa, na Mwenyezi Mungu Ndiye Ajuaye zaidi.

La pili: Ni kwamba asikusudie kwa kumshusha mtoto aliye tumboni kumuangamiza; yaani jaribio la kumshusha liwe mwishoni mwa muda wa ujauzito na karibu na kujifungua; basi hili linajuzu, kwa sharti kwamba pasiwe na madhara kwa mama, wala kwa mtoto, na kwamba jambo hilo lisihitaji upasuaji; ikihitaji upasuaji, basi lina hali nne:

Ya kwanza: Mama awe hai na mimba iwe hai, basi haijuzu kufanywa upasuaji ila kwa dharura, ikiwa uzazi wake umekuwa mgumu akahitaji upasuaji; na hilo ni kwa sababu mwili ni amana kwa mja, hivyo asiuingilie kwa kitendo kinachohofiwa madhara yake isipokuwa kwa masilahi makubwa; na kwa kuwa huenda mja akadhani kuwa hakuna madhara katika upasuaji, kisha madhara yakatokea.

Aina ya pili: Ni kwamba mama awe amefariki, na mtoto awe amekufa; basi haijuzu kufanya upasuaji wa kumtoa, kwa kuwa hakuna faida.

Aina ya tatu: Ni kwamba mama awe hai na mimba iwe imekufa, basi inajuzu kufanywa upasuaji wa kuiondoa, isipokuwa ikiogopwa madhara kwa mama; kwa sababu inavyojulikana - na Mwenyezi Mungu anajua zaidi - kwamba mimba ikifa mara nyingi haitoki bila upasuaji, hivyo kuendelea kubaki kwake tumboni kunamzuia kupata ujauzito ujao, na humtaabisha, na huenda akabaki bila mume ikiwa yuko katika eda ya mume wa awali.

Ya nne: Mama awe amefariki na mtoto aliye tumboni yuko hai; basi ikiwa yeye hatarajiwi kuishi, si halali kufanya upasuaji.

Na ikiwa kunatarajiwa uhai wake, basi iwapo baadhi yake imeshatoka, tumbo la mama huchanwa ili kutoa kilichobaki; na iwapo hakuna chochote kilichotoka, basi wamesema wenzetu -Mwenyezi Mungu awarehemu-: Halitapasuliwa tumbo la mama ili kutoa mimba; kwa sababu hicho ni kitendo cha kudhalilisha na kuharibu mwili (muthla). Na kauli sahihi ni kwamba tumbo huchanwa endapo haiwezekani kumtoa bila kufanya hivyo. Na hili ndio chaguo la Ibn Hubaira; amesema katika Al-Insaaf72: na msimamo huo ndio wa kupewa kipaumbele.

Nikasema: Na hasa katika wakati wetu huu, kwa kuwa kufanya upasuaji si unyanyasaji wa mwili; kwa sababu tumbo huchanwa kisha hushonwa, na kwa sababu huruma ya aliye hai ni kubwa zaidi kuliko huruma ya maiti; na kwa kuwa kumuokoa aliyehifadhiwa kutokana na maangamizi ni wajibu, na mimba ni mwanadamu aliyehifadhiwa, basi ni wajibu kumuokoa. Na Mwenyezi Mungu ndiye ajuaye zaidi.

Tanbihi: Katika hali ambazo kutoa mimba kunaruhusiwa kama ilivyotangulia, haina budi ipatikane idhini ya mwenye haki juu ya mimba hiyo, kama mume.

 

Na mpaka hapa tumemaliza yale tuliyonuia kuyaandika katika mada hii muhimu, na tumejiegemeza humo tu kwenye misingi ya masuala na kanuni zake; vinginevyo, matawi yake na vipengele vyake vidogo, na yale yanayowatokea wanawake, na hilo, ni bahari isiyo na pwani. Lakini mwenye elimu anaweza kurudisha matawi kwenye misingi yake, na vipengele vidogo katika jumla zake na kanuni zake madhubuti, na akapima vitu kwa vinavyofanana navyo.

Na ajue mtoa fat'wa kwamba yeye ni kiunganishi kati ya Mwenyezi Mungu na viumbe wake katika kufikisha yale yaliyoletwa na Mitume wake na kuyabainisha kwa viumbe; na kwamba anawajibika na ataulizwa kuhusu yaliyomo katika Kitabu na Sunna, kwani hivyo viwili ndivyo vyanzo ambavyo mja amekalifishwa kuvielewa na kuvifanyia kazi. Na kila kilichopingana na Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Sunna ya Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, ni kosa; ni lazima lirejeshwe kwa msemaji wake, wala hauruhusiki kutenda kwa mujibu wake. Ijapokuwa msemaji wake anaweza kuwa na udhuru kwa kuwa ni mwenye jitihada, basi ataandikiwa thawabu kwa jitihada yake; lakini mwingine anayejua kosa hilo hauruhusiki kulikubali.

 

Ni wajibu kwa Mufti kutakasa nia kwa ajili ya Mwenyezi Mungu mtukufu, na aombe msaada Kwake katika kila tukio linalompata, na amuombe Yeye Aliyetukuka uthabiti na tawfiki ya kufikia lililo sahihi.

Na ni wajibu kwake kuwa anachokizingatia ni yale yaliyokuja katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu -Kutakasika na machafu ni kwake- na katika sunna za Mtume rehema na amani ziwe juu yake; kisha atazame na atafiti katika hayo, au arejee katika kauli za wanazuoni zinazosaidia kuyaelewa hayo mawili.

Na kwa hakika mara nyingi hutokea maswala miongoni mwa maswala, mtu akalifanyia utafiti katika yale anayoweza kuyafikia katika maneno ya wanazuoni, kisha asipate kile kitakachompa utulivu wa moyo kuhusu hukumu yake, na huenda asipate hata kutajwa kwake kabisa. Basi akirejea katika Qur'ani na sunna itabainika kwake hukumu yake upesi na waziwazi, na hilo ni kwa kadiri ya ikhlasi, elimu na ufahamu.

 

Ni wajibu kwa Mufti atulie katika kutoa hukumu panapokuwa na utata, wala asifanye pupa; kwani mara ngapi ameharakisha katika hukumu, kisha ikabainika kwake baada ya kutafakari kwa muda mfupi kuwa amekosea, akajutia hilo, na huenda asiweze kurekebisha alichokwisha kukitoa katika majibu (Fat-wa)!

Na mtoa majibu (Fat-wa) anapojulikana kwa watu kwa utulivu na uthabiti, huwa wanaiamini kauli yake na kumheshimu; na wakimuona ana pupa, na mwenye pupa ni mwingi wa makosa, hawatamuamini katika yale anayoyatoa katika majibu, basi kwa pupa yake na makosa yake huwa amejinyima mwenyewe na anawanyima wengine yale aliyonayo katika elimu na usahihi.

Tunamuomba Mwenyezi Mungu Mtukufu atuongoze sisi na ndugu zetu Waislamu katika njia yake iliyo nyoofu, na atutunze kwa uangalizi wake, na atuhifadhi kutokana na makosa kwa ulinzi wake. Hakika Yeye ni Mpaji, Mkarimu; na Rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu ya Nabii wetu Muhammad, na juu ya familia yake na maswahaba zake wote. Na kila sifa njema zinamstahiki Mwenyezi Mungu ambaye kwa neema yake matendo mema hutimia.

 

Kimetimia kwa uandishi wa Mhitaji kwa Mwenyezi Mungu

Muhammadi Swaleh Al-Uthaimin

Katika asubuhi ya siku ya Ijumaa

Tarehe 14 Shaban mwaka 1392 Hijria.

 

 

***

Yaliyomo

 

Sura ya Kwanza: Kuhusu maana ya Hedhi, na hekima yake. 5

Sura ya Pili: Kuhusu Muda wa Hedhi na Kipindi Chake. 6

Sura ya tatu: Kuhusu Matukio ya dharura yanayoathiri Hedhi 17

Sura ya nne: Kuhusu Hukumu za Hedhi 24

Sura ya tano: Katika Damu ya Ugonjwa, na hukumu zake. 46

Hali za damu ya ugonjwa: 48

Hali ya anayefanana na mwenye damu ya ugonjwa (Istihadha): 53

Hukumu za damu ya ugonjwa: 54

Sura ya sita: Kuhusu Nifasi na hukumu yake. 57

Hukumu za Nifasi: 59

Sura ya saba: Katika matumizi ya yale yanayozuia hedhi au yanayoileta, na yanayozuia ujauzito au yanayosababisha mimba kutoka 63

 

***

 


Ameipokea Bukhari katika kitabu cha Hedhi, mlango wa Mwenye hedhi hutekeleza ibada zote za Hija isipokuwa Tawafu ya Kaaba, nambari 305, na Muslim katika kitabu cha Hija, mlango wa Kubainisha namna za kuhirimia, nambari 1211.

Imepokelewa na Bukhari katika Kitabu cha Umra, mlango wa Thawabu za Umra kwa kadiri ya mashaka, nambari (1662), na Muslim katika Kitabu cha Hija, mlango wa Ufafanuzi wa Aina za Ihramu, nambari (1211).

Rejea: Rasaailul-Asmaa Allatii Allaqa sh-Shaariu Al-Ahkaam bihaa (Uk. 35).

Chanzo kilichotangulia ukurasa wa 36.

Chanzo kilichotangulia ukurasa wa 38.

Imepokelewa na Bukhari: Kitabu cha Imani, mlango wa "Dini ni wepesi", nambari (39), kutoka kwa Abu Hurairah, Mwenyezi Mungu amuwie radhi.

Ameipokea Bukhari katika kitabu cha Manaaqib, mlango wa Sifa ya Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, nambari (3560), na Muslim katika kitabu cha Al-Fadhail, mlango wa kujiepusha kwake, rehema na amani ziwe juu yake, na madhambi, nambari (77/2327).

Tazama: Majmu'ul Fataawa: Juzuu ya 19, uk. 238-239.

Al-Awsat (356/2).

Tazama: Al-Mughni (405/1).

Kitabu Al-Mudawwana, juzuu ya 1/155, Al-Nawadir wal-Ziyadat, juzuu ya 1/136.

Ikhtilaaf Al-fuqahaa (Al-marwaziy) (uk. 193), Al-Awsat (juzuu 2/239).

Tazama: Majmu'ul Fataawa: Juzuu ya 19, uk. 238-239.

Al-Umm (82/1).

Al-Mughni (396/1)

Imepokelewa na Abu Dawud: Kitabu cha Twahara, mlango kuhusu mwanamke anayeona rangi ya kahawia (al-kudrah) na ya njano (as-sufrah) baada ya twahara, nambari (307).

Imepokelewa na Bukhari: Kitabu cha Hedhi, mlango wa ute wa rangi ya manjano na kahawia katika siku zisizo za hedhi, nambari (326).

Fat-h Al-Baari", 1/426.

Sahihi Bukhari (1/ 71).

Ameitaja Bukhari kwa mu'allaq: Kitabu cha Hedhi, Mlango wa kuingia kwa hedhi na kutoka kwake, kabla ya hadithi nambari (320).

Al-Umm (1/ 83-84).

Imenukuliwa kutoka kwao katika Al-insaaf.

Al-Asl (19/2-20)

Al-Mughni (226/1)

Al-Mughni (257/1).

Ameipokea Bukhari katika kitabu cha Nyakati za swala, mlango wa Mwenye kuipata rakaa moja ya swala, kwa nambari 580, na Muslim katika kitabu cha Misikiti na sehemu za swala, mlango wa Mwenye kuipata rakaa moja ya swala basi amepata swala hiyo, kwa nambari 607, miongoni mwa hadithi za Abuu Huraira.

Ameipokea Bukhari katika kitabu cha Nyakati za swala, mlango wa Aliyepata rakaa moja ya Alfajiri, kwa nambari 579, na Muslim katika kitabu cha Misikiti na mahali pa kuswalia, mlango wa Aliyepata rakaa moja basi amepata hiyo swala, kwa nambari 608, miongoni mwa hadithi za Abuu Huraira.

Al-majmu' Sharh Al-muhadhdhab (juzuu ya 3/70).

Ameipokea Bukhari katika kitabu cha Hedhi, mlango wa kusoma kwa mwanaume akiwa pajani kwa mkewe naye akiwa katika hedhi, nambari (297), na Muslim katika kitabu cha Hedhi, mlango wa kuegemea kwa mwanaume pajani kwa mkewe naye akiwa katika hedhi na kusoma Qurani, nambari (301), katika hadithi ya Aisha, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake.

Ameipokea Bukhari katika kitabu cha Hedhi, mlango wa kuhudhuria wenye hedhi katika Iddi mbili na mwito kwa Waislamu, na wajitenge na mahala pa kuswalia, nambari 324, na Muslim katika kitabu cha Swala ya Iddi mbili, mlango wa kutaja kuruhusiwa kutoka kwa wanawake katika Iddi mbili kuelekea mahala pa tukio la swala ya iddi na kuhudhuria hotuba, wakiwa wametengana na wanaume, nambari 890.

Al-Majmu' (2/ 357).

Tazama: Sahihi Bukhari, Kitabu cha Hedhi, mlango wa mwenye hedhi hutekeleza ibada yote isipokuwa twawafu ya Kaaba, na Fathul Bari (1/ 407-408).

"Fat-h Al-Baari" (1/408).

Al-auswat (2/ 223).

Al-Majmuu' (2/356).

"Fat-h Al-Baari" (1/ 408).

Ameitaja Bukhari kwa ta'liq: Sahihi Bukhari, Kitabu cha Hedhi, mlango wa Mwenye hedhi hutekeleza ibada zote isipokuwa twawafu ya kuizunguka Kaaba, kabla ya hadithi namba (305).

Kaipokea At-Tirmidhiy: Milango ya Twahara, Mlango wa yaliyokuja kuhusu mwenye janaba na mwenye hedhi kwamba hawasomi Qur'ani, kwa nambari 131.

Tazama: Al-Ilal, cha At-Tirmidhi (69/ mpangilio wake), na As-Sunan al-Kubra, cha Al-Baihaqiy (1/ 309), na Al-Ahkam ash-Shar’iyyah, cha Ibn ‘Abd al-Haqq (1/ 504), na Nasb ar-Raayah, cha Az-Zayla’iy (1/ 195).

Tazama: Majmu'ul-Fataawa, uk. (26/191).

Imepokelewa na Bukhari katika Kitabu cha Hedhi, mlango wa Mwanamke mwenye hedhi halipi swala, nambari (321); na Muslim katika Kitabu cha Hedhi, mlango wa Wajibu wa kulipa Saumu kwa mwanamke mwenye hedhi bila kulipa swala, nambari (335); na tamko ni la Muslim.

Imepokelewa na Bukhari: Kitabu cha Elimu, mlango wa Haya katika Elimu, nambari (130). Na Muslim: Kitabu cha Hedhi, mlango wa Wajibu wa kuoga kwa mwanamke..., nambari (313).

Imepokelewa na Bukhari katika Kitabu cha Saumu, mlango wa Kuoga kwa mwenye kufunga, nambari (1931), na Muslim katika Kitabu cha Saumu, mlango wa Usahihi wa saumu ya aliyepambazukiwa na alfajiri naye yuko katika janaba, nambari (1109).

Ameipokea Bukhari katika kitabu cha Hedhi, mlango wa Mwenye hedhi kutekeleza manasiki (ibada) yote isipokuwa Tawafu ya Nyumba, nambari (305), na Muslim katika kitabu cha Hija, mlango wa Kubainisha namna za kuhirimia, nambari (1211).

Ameipokea Bukhari katika kitabu cha Hija, mlango wa Tawafu ya kuaga, nambari (1755), na Muslim katika kitabu cha Hija, mlango wa Tawafu ya kuaga na kuondolewa kwake kwa mwenye hedhi, nambari (1328).

Ameipokea Bukhari katika kitabu cha Hija, mlango wa mwanamke kupata hedhi baada ya kufanya Tawafu ya Ifadha, nambari 1757, na Muslim katika kitabu cha Hija, mlango wa Tawafu ya kuaga, nambari 1211.

Ameipokea Bukhari katika kitabu cha Hedhi, mlango wa kuhudhuria kwa mwenye hedhi Iddi mbili na wito wa Waislamu, na wajitenge na mahala pa kuswalia, nambari (324). Na Muslim katika kitabu cha Swala ya Iddi mbili, mlango wa kutaja uhalali wa kutoka kwa wanawake katika Iddi mbili kwenda kwenye mahala pa kuswalia na kuhudhuria hotuba, wakiwa wametengana na wanaume, nambari (890).

Ameitoa Muslim katika Kitabu cha Hedhi, mlango wa ruhusa ya mwanamke mwenye hedhi kuosha kichwa cha mume wake, nambari (302).

Ameipokea Bukhari katika kitabu cha Hedhi, mlango wa kumpapasa mwenye hedhi, nambari (301), na Muslim katika kitabu cha Hedhi, mlango wa kumpapasa mwenye hedhi juu ya izari, nambari (293).

Imepokelewa na Bukhari katika Kitabu cha Talaka, nambari (5251), na Muslim katika Kitabu cha Talaka, mlango wa Kuharamisha kumtaliki mwanamke mwenye hedhi bila ridhaa yake, na kwamba akikiuka hutokea talaka, na huamrishwa kumrudisha, nambari (1471), kutoka katika Hadithi ya bin Omari, Mwenyezi Mungu awawie radhi.

Imepokelewa na Bukhari: Kitabu cha Talaka, Mlango wa Khul’u na jinsi ya talaka humo, nambari (5273), kutoka katika Hadithi ya Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awawie radhi wote wawili.

Ameipokea Bukhari katika kitabu cha Hedhi, mlango wa kuanza kwa hedhi na kumalizika kwake, nambari 320, na Muslim katika kitabu cha Hedhi, mlango wa mwenye Istihadhah, josho lake na Swala yake, nambari 333, katika hadithi ya Aisha, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake.

Imepokelewa na Bukhari: Kitabu cha Hedhi, Mlango wa kuoga kwa mwenye hedhi, nambari (315), na Muslim: Kitabu cha Hedhi, Mlango wa kupendekezwa kwa aliyeoga kutokana na hedhi kutumia kipande cha misk katika mahali pa damu, nambari (332), kutoka katika Hadithi ya Aisha, Mwenyezi Mungu amuwie radhi.

Ameipokea Muslim katika kitabu cha Hedhi, mlango wa Hukumu ya misokoto ya nywele ya mwenye kuoga, nambari (330), kutoka kwa Ummu Salama, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake.

Ameipokea Bukhari katika kitabu cha Udhu, mlango wa kuosha damu, nambari (228), na Muslim katika kitabu cha Hedhi, mlango wa mwanamke mwenye damu ya istihadhwa na kuoga kwake na swala yake, nambari (333), katika hadithi ya Aisha, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake.

Ameipokea Ahmad 6/349, na Abuu Daud, kitabu cha Twahara, mlango wa aliyesema anapokuja hedhi aache swala, nambari 287, na Tirmidhi, milango ya Twahara, mlango wa kuhusu mwenye istihadha kwamba anakusanya baina ya swala mbili kwa uogaji wamara moja, nambari 128, katika hadithi ya Hamna bint Jahsh -radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake-.

Sunan At-Tirmidhiy: Milango ya Twahara, mlango unaohusu mwanamke mwenye istihadha kwamba anajumuisha baina ya Swala mbili kwa josho moja, baada ya Hadithi namba (128).

Imepokelewa na Bukhari: Kitabu cha Hedhi, Mlango wa Hedhi, na kusadikiwa kwa wanawake kuhusu hedhi na ujauzito, katika yanayowezekana katika hedhi, namba (325), kutoka kwa Aisha (Mwenyezi Mungu amridhie).

Imepokelewa na Muslim: Kitabu cha Hedhi, Mlango wa mwanamke mwenye damu ya istihadhah, kuoga kwake na Swala yake, nambari (334), kutoka katika Hadithi ya Aisha, Mwenyezi Mungu amuwie radhi.

Ameitoa Abu Dawud: Kitabu cha Twahara, Mlango wa yule aliyesema: Inapoingia hedhi aache swala, namba (286); na An-Nasai: Kitabu cha Twahara, Mlango wa yaliyokuja kuhusu mwenye damu ya ugonjwa ambaye amejua siku za hedhi zake za kawaida, kabla ya damu kuendelea kwake, namba (211); na Ibn Majah: Kitabu cha Twahara na Sunna zake, Mlango wa yaliyokuja kuhusu mwenye damu ya ugonjwa ambaye amejua siku za hedhi zake za kawaida, kabla ya damu kuendelea kwake, namba (620); na Ibn Hibban katika Sahihi yake (1348); na Al-Hakim katika Al-Mustadrak (618); kutoka kwa hadithi ya Aisha -radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake-.

Ameipokea Ahmad (6/439), na Abuu Daud katika kitabu cha Twahara, mlango wa aliyesema: anapokuja hedhi aache swala, nambari (287), na Tirmidhi katika milango ya Twahara, mlango kuhusu mwenye istihadhah kwamba anakusanya kati ya swala mbili kwa ghuslu moja, nambari (128), katika hadithi ya Hamna bint Jahsh -radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake-.

Sunanu Tirmidhiiy: Milango ya Twahara, mlango kuhusu mwanamke mwenye Istihadha kwamba anajumuisha baina ya Swala mbili kwa josho moja, baada ya Hadithi namba (128).

Imepokelewa na Bukhari katika Kitabu cha Udhu, mlango wa kuosha damu, nambari (228), na Muslim katika Kitabu cha Hedhi, mlango wa mwanamke mwenye istihadhah, kuoga kwake na swala yake, nambari (333), kutoka katika hadithi ya Aisha, Mwenyezi Mungu amuwie radhi.

Imepokelewa na Ahmad (6/204), na Ibn Majah, Kitabu cha Twahara na Sunna zake, Mlango: Yaliyoelezwa kuhusu mwenye Istihadhwa ambaye tayari amehesabu siku za hedhi zake, kabla ya damu kuendelea kwake, nambari (624), kutoka katika Hadithi ya Aisha, Mwenyezi Mungu amuwie radhi.

Al-Mughni (252/1-253).

Kashshaf al-Qinaa' (219/1)

Al-Mughni (253/1).

Al-Mughni (253/1).

Al-Mughni (2/252), na athari ya Uthman bin Abi al-'As imepokelewa na 'Abd ar-Razzaq katika Al-Musannaf (1202), na Ibn Abī Shaiba katika Al-Musannaf (17450), na Ad-Darimi katika As-Sunan (990), na Ibn al-Jarud katika Al-Muntaqa (118).

Imepokelewa na Bukhari: Kitabu cha Ndoa, Mlango wa 'Azl, nambari (5209), na Muslim: Kitabu cha Ndoa, Mlango wa Hukumu ya 'Azl, nambari (1440), kutoka kwa Jabir, Mwenyezi Mungu amuwie radhi.

Al-insaaf (juzuu 556/2).

Ahkaamu Al-Mutahayyirah fil-Haidh, cha Ad-Darmi (uk. 17).