إِقََامَةُ البَرَاهِينِ عَلَى
حُكْمِ مَنِ اسْتَغَاثَ بِغَيرِ اللهِ
KUSIMAMISHA USHAHIDI JUU YA HUKUMU YA MWENYE KUTAFUTA KUOKOLEWA NA ASIYEKUWA MWENYEZI MUNGU
لِسَمَاحَةِ الشَّيْخِ العَلَّامَةِ
عَبْدِ العَزِيزِ بْنِ عَبْدِ اللهِ بْنِ بَازٍ
رَحِمَهُ اللهُ
Mtunzi Mheshimiwa, Sheikh,
Abdulaziz bin Abdillah bin Baaz
بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَنِ الرَّحِيمِ
Makala ya Pili: Kuhusu hukumu ya kuomba kuokolewa kutoka kwa Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake.
Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, na rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu ya Mtume wa Mwenyezi Mungu, na watu wa familia yake, Maswahaba wake na wote wanaofuata uongofu wake.
Ama baada ya hayo: Gazeti la Al-Mujtama' Al-Kuwaiti katika toleo lake la kumi na tano, lililotokea tarehe 19/4/1390 Hijria, lilichapisha beti kwa anuani ya: (Katika Maadhimisho ya Kuzaliwa Mtume Mtukufu), ambazo zilijumuisha kuomba kuokolewa kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, na kutafuta nusura kutoka kwake kwamba auokoe Umma na kuunusuru na kuukomboa kutoka katika mgawanyiko na kutofautiana ambako uliingia ndani yake. Beti hizo zimetungwa na aliyejiita Amina. Na hizi ndizo beti zenyewe tulizoziashiria hapo juu:
Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, uokoe ulimwengu... unaowaka vita na kuungua kwa miale yake.
Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, uokoe Umma... kutoka katika giza la shaka, ambalo limekuwa refu sana
Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, uokoe Umma... uliopoteza maono yake katika michanganyiko ya huzuni
Mpaka aliposema:
Harakisha kuleta ushindi kama ulivyouharakisha... siku ya Badri ulipomuomba Mola Mlezi
Kwa hivyo, udhalili ukageuka kuwa ushindi wa ajabu... hakika Mwenyezi Mungu ana majeshi usiyoyaona
Hivi ndivyo mwandishi huyu anavyoelekeza wito na kuomba kwake kuokolewa kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake, akimuomba auokoe Umma kwa kuleta nusura haraka, huku akiwa amesahau au hajui kwamba nusura iko mikononi mwa Mwenyezi Mungu peke yake, si mikononi mwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, wala yeyote mwingine miongoni mwa viumbe, kama alivyoeleza Mwenyezi Mungu Mtukufu katika Kitabu chake kilicho wazi:
﴿...وَمَا النَّصْرُ إِلَّا مِنْ عِنْدِ اللَّهِ الْعَزِيزِ الْحَكِيمِ﴾
"Na msaada hautoki isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu, Aliyetukuka, Mwenye nguvu na Mwenye hekima." [Al-Imran: 126] Na akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿إِنْ يَنْصُرْكُمُ اللَّهُ فَلَا غَالِبَ لَكُمْ وَإِنْ يَخْذُلْكُمْ فَمَنْ ذَا الَّذِي يَنْصُرُكُمْ مِنْ بَعْدِهِ...﴾
"Akikunusuruni Mwenyezi Mungu, hapana wa kukushindeni. Na akikutupeni, ni nani basi baada yake Yeye atayekunusuruni?" [Al-Imran: 160]
Kitendo hiki cha kuomba dua na kutafuta kuokolewa ni kuelekeza aina ya ibada kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu. Na imeshajulikana kwa maandiko (ya Qur'ani na Sunna) na kwa makubaliano ya wanazuoni kwamba hilo haliruhusiwi, na kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu aliwaumba viumbe ili wamuabudu, na akatuma Mitume na kuteremsha Vitabu ili kufafanua ibada hiyo na kuwaita watu kwayo, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿وَمَا خَلَقْتُ الْجِنَّ وَالْإِنْسَ إِلَّا لِيَعْبُدُونِ56﴾
"Nami sikuwaumba majini na watu ila waniabudu Mimi." [Surat Adh-Dhariyaat: 56].
Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿وَلَقَدْ بَعَثْنَا فِي كُلِّ أُمَّةٍ رَسُولًا أَنِ اعْبُدُوا اللَّهَ وَاجْتَنِبُوا الطَّاغُوتَ...﴾
"Na kwa hakika, kwa kila umma tuliutumia Mtume kwamba: Muabuduni Mwenyezi Mungu, na muepukeni Twaghuut (Shetani na vyote vinavyoabudiwa kinyume na Mwenyezi Mungu." [Surat An-Nahl: 36]. Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿وَمَا أَرْسَلْنَا مِنْ قَبْلِكَ مِنْ رَسُولٍ إِلَّا نُوحِي إِلَيْهِ أَنَّهُ لَا إِلَهَ إِلَّا أَنَا فَاعْبُدُونِ 25﴾
"Na hatukumtuma kabla yako Mtume yeyote ila tulimfunulia ya kwamba hapana mungu isipokuwa Mimi. Basi niabuduni Mimi tu." [Surat Al-Anbiya: 25], Na akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿الر كِتَابٌ أُحْكِمَتْ آيَاتُهُ ثُمَّ فُصِّلَتْ مِنْ لَدُنْ حَكِيمٍ خَبِيرٍ1 أَلَّا تَعْبُدُوا إِلَّا اللَّهَ إِنَّنِي لَكُمْ مِنْهُ نَذِيرٌ وَبَشِيرٌ2﴾
"Alif Lam Raa. Hiki ni kitabu ambacho Aya zake zimewekwa wazi kisha zikapambanuliwa vizuri, kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mwenye hekima, Mwenye habari za kila kitu.
(Imefanywa hivyo) ili msiabudu isipokuwa Mwenyezi Mungu. Hakika mimi kwenu ni muonyaji na mbashiri nitokae kwake." [Surat Hud: 1-2]
Basi Mwenyezi Mungu Mtukufu akabainisha katika aya hizi zilizo wazi kwamba hakuwaumba wale viumbe wawili wazito (wanadamu na majini) isipokuwa wamu abudu Yeye peke yake, asiye na mshirika, na akaeleza kuwa alituma Mitume –rehema na amani ziwe juu yao- ili waamrishe ibada hii na kukataza kinyume chake, na akaeleza kuwa aliziweka wazi aya za Kitabu chake na kuzipambanua ili kisiabudiwe chochote kisichokuwa Yeye Mtukufu.
Inajulikana kuwa kuabudu maana yake ni kumpwekesha Mwenyezi Mungu na kumtii, kwa kutii maamrisho yake na kuacha makatazo yake. Mwenyezi Mungu ameyaamrisha hayo na kujulisha juu yake katika Aya nyingi, zikiwemo kauli yake aliyetakasika:
﴿وَمَا أُمِرُوا إِلَّا لِيَعْبُدُوا اللَّهَ مُخْلِصِينَ لَهُ الدِّينَ حُنَفَاءَ...﴾
"Nao hawakuamrishwa kitu ila wamuabudu Mwenyezi Mungu kwa kumtakasia Dini, wawe waongofu." [Surat Al-Bayyina: 5] Na kauli yake Mwenye nguvu, Mtukufu:
﴿وَقَضَى رَبُّكَ أَلَّا تَعْبُدُوا إِلَّا إِيَّاهُ...﴾
"Na Mola wako Mlezi ameamrisha kuwa msimuabudu yeyote ila Yeye tu." [Surat Al-Israai: 23] Na kauli yake Mtukufu:
﴿إِنَّآ أَنزَلۡنَآ إِلَيۡكَ ٱلۡكِتَٰبَ بِٱلۡحَقِّ فَٱعۡبُدِ ٱللَّهَ مُخۡلِصٗا لَّهُ ٱلدِّينَ2 أَلَا لِلَّهِ ٱلدِّينُ ٱلۡخَالِصُۚ وَٱلَّذِينَ ٱتَّخَذُواْ مِن دُونِهِۦٓ أَوۡلِيَآءَ مَا نَعۡبُدُهُمۡ إِلَّا لِيُقَرِّبُونَآ إِلَى ٱللَّهِ زُلۡفَىٰٓ إِنَّ ٱللَّهَ يَحۡكُمُ بَيۡنَهُمۡ فِي مَا هُمۡ فِيهِ يَخۡتَلِفُونَۗ إِنَّ ٱللَّهَ لَا يَهۡدِي مَنۡ هُوَ كَٰذِبٞ كَفَّارٞ3﴾
"Hakika Sisi tumekuteremshia Kitabu hiki kwa Haki. Basi muabudu Mwenyezi Mungu ukimsafia Dini Yeye tu." Sikilizeni. Hakika Dini Safi ni ya Mwenyezi Mungu tu. Na wale wanaowafanya wenginewe kuwa ni walinzi wakisema: Sisi hatuwaabudu ila wapate kutujongeza tu kumkaribia Mwenyezi Mungu - Hakika Mwenyezi Mungu atahukumu baina yao katika yale wanayohitilafiana. Hakika Mwenyezi Mungu hamuongoi aliye muongo kafiri." [Az-Zumar: 2-3].
Na aya zenye maana hii ni nyingi. Zote zinaonyesha ulazima wa kufanya ibada kwa ajili ya Mwenyezi Mungu peke yake, na kuacha kumuabudu mwingine yeyote, sawa sawa wawe ni Manabii au wengineo.
Hakuna shaka kwamba dua ni miongoni mwa aina ya ibada iliyo muhimu na kamili zaidi. Kwa hivyo, ni lazima kuifanya kwa ajili ya Mwenyezi Mungu peke yake, kama alivyosema Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Mtukufu:
﴿فَادْعُوا اللَّهَ مُخْلِصِينَ لَهُ الدِّينَ وَلَوْ كَرِهَ الْكَافِرُونَ14﴾
"Basi muombeni Mwenyezi Mungu mkimsafia Dini Yeye tu, hata kama watachukia makafiri." [Surat Ghafir: 14] Na akasema Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Mtukufu:
﴿وَأَنَّ الْمَسَاجِدَ لِلَّهِ فَلَا تَدْعُوا مَعَ اللَّهِ أَحَدًا18﴾
"Na kwamba kwa hakika misikiti ni ya Mwenyezi Mungu. Basi msimuabudu yeyote pamoja na Mwenyezi Mungu" [Surat Al-Jinn: 18] Agizo hili la kumpwekesha Mwenyezi Mungu katika dua, linawaenea viumbe wote, hata Manabii na wengineo. Na kauli yake:
﴿وَلَا تَدْعُ مِنْ دُونِ اللَّهِ مَا لَا يَنْفَعُكَ وَلَا يَضُرُّكَ فَإِن فَعَلۡتَ فَإِنَّكَ إِذٗا مِّنَ ٱلظَّٰلِمِينَ106﴾
"Na wala usiombe badala ya Mwenyezi Mungu wale ambao hawakufai kitu wala hawakudhuru. Na ukifanya hivyo, basi wewe hakika ni miongoni mwa madhalimu." [Surat Yunus: 106] Haya maneno anaambiwa Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na inajulikana kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu alimkinga kutokana na ushirikina, lakini lengo la haya ni kuwaonya wasiokuwa yeye. Kisha akasema Mwenyezi Mungu Mwenye utukufu mkubwa:
﴿وَلَا تَدۡعُ مِن دُونِ ٱللَّهِ مَا لَا يَنفَعُكَ وَلَا يَضُرُّكَ فَإِنْ فَعَلْتَ فَإِنَّكَ إِذًا مِنَ الظَّالِمِينَ106﴾
"Na wala usiombe badala ya Mwenyezi Mungu wale ambao hawakufai kitu wala hawakudhuru. Na ukifanya hivyo, basi wewe hakika ni miongoni mwa madhalimu." [Surat Yunus: 106] Maneno haya anaambiwa Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na kinachokusudiwa kwayo ni kuwaonya wengineo. Kwa sababu inajulikana kuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu alimlinda Mtume wake kutokana na ushirikina. Kisha Mwenyezi Mungu Mtukufu akawa mkali katika kukataza na kuonya. Akasema:
﴿...فَإِنْ فَعَلْتَ فَإِنَّكَ إِذًا مِنَ الظَّالِمِينَ﴾
"Ukifanya hivyo, basi hakika utakuwa miongoni mwa waliodhulumu." Wakati neno dhuluma linatumika kwa maneno ya ujumla, huwa linamaanisha ushirikina mkubwa, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿...وَالْكَافِرُونَ هُمُ الظَّالِمُونَ﴾
"Na makafiri ndio madhalimu." [Al-Baqara: 254]. Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿...إِنَّ الشِّرْكَ لَظُلْمٌ عَظِيمٌ﴾
"Kwani hakika ushirikina bila ya shaka ni dhuluma kubwa." [Luqman: 13]. Lau bwana wa watoto wa Adam, Muhammad, rehema na amani ziwe juu yake, angemuomba asiyekuwa Mwenyezi Mungu, angekuwa miongoni mwa madhalimu, basi itakuwa vipi kuhusu mwingine?!
Ikajulikana kutokana na aya hizi na nyinginezo kwamba kumuomba asiyekuwa Mwenyezi Mungu miongoni mwa wafu, miti, masanamu na vinginevyo ni kumshirikisha Mwenyezi Mungu Mtukufu, na kunapingana na kumpwekesha Mwenyezi Mungu katika ibada, ambayo ndiyo makusudio ya Mwenyezi Mungu kuumba vitu viwili vikubwa (majini na watu), kutuma Mitume, na kuteremsha Vitabu, na kunapingana na maana ya: Hakuna mungu ila Mwenyezi Mungu. Ambayo hukanusha kuabudiwa kwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu, na kumthibitishia Mwenyezi Mungu peke yake ibada, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿ذَٰلِكَ بِأَنَّ ٱللَّهَ هُوَ ٱلۡحَقُّ وَأَنَّ مَا يَدۡعُونَ مِن دُونِهِۦ هُوَ ٱلۡبَٰطِلُ وَأَنَّ ٱللَّهَ هُوَ ٱلۡعَلِيُّ ٱلۡكَبِيرُ62﴾
"Hayo ni kwa kuwa Mwenyezi Mungu ndiye wa Kweli, na kwamba wale wanaowaomba badala yake, ni batili, na kwamba hakika Mwenyezi Mungu ndiye Aliye Juu na ndiye Mkubwa" [Al-Hajj: 62].
Na huu ndio msingi wa dini na mila ya Kiislamu, na wala ibada haziwezi kuwa sahihi isipokuwa baada ya asili hii kuwa sahihi, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿وَلَقَدْ أُوحِيَ إِلَيْكَ وَإِلَى الَّذِينَ مِنْ قَبْلِكَ لَئِنْ أَشْرَكْتَ لَيَحْبَطَنَّ عَمَلُكَ وَلَتَكُونَنَّ مِنَ الْخَاسِرِينَ65﴾
"Na kwa yakini yamefunuliwa kwako na kwa wale waliokuwa kabla yako: Bila ya shaka ukimshirikisha Mwenyezi Mungu, matendo yako yataanguka, na lazima utakuwa miongoni mwa wenye kupata hasara." [Surat Az-Zumar: 65] Na amesema Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kutukuka:
﴿...وَلَوْ أَشْرَكُوا لَحَبِطَ عَنْهُمْ مَا كَانُوا يَعْمَلُونَ﴾
"Na lau wangelimshirikisha, yangeliwaharibikia yale waliyokuwa wakiyatenda." [Surat Al-An'am: 88].
Kutokana na yaliyotangulia hapo juu, inadhihirika kuwa Dini ya Uislamu na kushuhudia kwamba: (Hakuna mungu ila Mwenyezi Mungu) vina misingi miwili mikuu:
Wa kwanza: Asiabudiwe ila Mwenyezi Mungu peke yake, asiye na mshirika. Kwa hivyo, mwenye kuwaomba wafu miongoni mwa Manabii na wengineo, au akawaomba masanamu, au miti, au mawe, au viumbe vingine, au akaomba kuokolewa nao, au akajikurubisha kwao kwa kuchinja na kuwawekea nadhiri, au akaswali kwa ajili yao, au akasujudu kwa ajili yao; basi hakika atakuwa amewafanya waola badala ya Mwenyezi Mungu, na akawafanya sawa na Mwenyezi Mungu Mtukufu, na akapinga na akakanusha maana ya hakuna mungu ila Mwenyezi Mungu.
Wa pili: Mwenyezi Mungu Mtukufu hapaswi kuabudiwa isipokuwa kwa mujibu wa sheria ya Nabii na Mtume wake, rehema na amani ziwe juu yake. Kwa hivyo, mwenye kuzua katika Dini yale ambayo Mwenyezi Mungu hakuruhusu, basi hatakuwa ametekeleza maana ya kushuhudia kwamba Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, na matendo yake hayatamnufaisha wala hayakubaliwa kutoka kwake. Amesema Mwenyezi Mungu Mwenye utukufu mkubwa:
﴿وَقَدِمْنَا إِلَى مَا عَمِلُوا مِنْ عَمَلٍ فَجَعَلْنَاهُ هَبَاءً مَنْثُورًا23﴾
"Na tutayaendea yale waliyoyatenda katika vitendo vyao, tuvifanye kama mavumbi yaliyotawanywa." [Surat Al-Furqaan: 23].
Kilichokusudiwa na matendo yaliyotajwa katika aya hii ni matendo ya mtu aliyekufa huku bado anamshirikisha Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Mtukufu.
Pia yanaingia katika hilo matendo yaliyobuniwa ambayo Mwenyezi Mungu hakuyaidhinisha. Hayo yatakuwa siku ya Kiyama kama mavumbi yaliyotawanywa, kwa sababu hayakulingana na sheria yake iliyotakaswa. Kama alivyosema Mtume rehema na amani ziwe juu yake: "Yeyote atakayezua (kitu) katika jambo letu hili (dini) ambalo si miongoni mwake, basi hilo litakataliwa." Wanachuoni wamekubaliana kwamba hadithi hii ni sahihi.
Na muhtasari wa maneno ni kwamba mwandishi huyu ameelekeza kuomba kwake kuokolewa na dua yake kwa Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na akampuuza Mola Mlezi wa walimwengu wote, ambaye nusura, madhara na manufaa, vyote viko mikononi mwake, na hakuna chochote katika hivi kilicho katika mikono ya asiyekuwa Yeye.
Hakuna shaka kwamba jambo hili ni dhuluma kubwa na yenye matokeo mabaya sana. Na Mwenyezi Mungu Mwenye nguvu, Mtukufu aliamuru watu wamuombe Yeye peke yake, akawaahidi wenye kumuomba kwamba atawaitikia dua yao, na akawaonya wale wanaojivuna kufanya hivyo kwamba wataingia Jahannam, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mwenye nguvu, Mtukufu:
﴿وَقَالَ رَبُّكُمُ ادْعُونِي أَسْتَجِبْ لَكُمْ إِنَّ الَّذِينَ يَسْتَكْبِرُونَ عَنْ عِبَادَتِي سَيَدْخُلُونَ جَهَنَّمَ دَاخِرِينَ 60﴾
"Na Mola wenu Mlezi amesema: Niombeni, nita kuitikieni. Kwa hakika wale wanaojivuna kuniabudu Mimi, wataingia Jahannamu wadhalilike." [Surat Ghafir: 60] Yaani, watakuwa duni na wadhalilifu. Basi aya hii tukufu ikaonyesha kwamba dua ni ibada, na kwamba yeyote atakayejivuna kumuomba Mwenyezi Mungu, basi makazi yake yatakuwa Jahannam. Kwa hivyo, ikiwa hali ya anayejivuna kumuomba Mwenyezi Mungu ni hivyo, basi itakuwaje hali ya yule anayeomba asiyekuwa Yeye na akapuuza kumuomba Mwenyezi Mungu, ambaye Yeye – Mtukufu – ndiye wa karibu zaidi, Mwenye kumiliki kila kitu, na Mwenye uwezo juu ya kila kitu, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿وَإِذَا سَأَلَكَ عِبَادِي عَنِّي فَإِنِّي قَرِيبٌ أُجِيبُ دَعْوَةَ الدَّاعِ إِذَا دَعَانِ فَلْيَسْتَجِيبُوا لِي وَلْيُؤْمِنُوا بِي لَعَلَّهُمْ يَرْشُدُونَ 186﴾
"Na waja wangu watakapokuuliza habari zangu, basi Mimi niko karibu. Naitikia maombi ya muombaji anaponiomba. Basi na waniitikie Mimi, na waniamini Mimi, ili wapate kuongoka." [Surat Al-Baqara: 186], Na Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake alieleza katika hadithi sahihi kwamba dua ndiyo ibada, na akamwambia mpwa wake, Abdullah bin Abbas - radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yao wawili: "Muhifadhi Mwenyezi Mungu, atakuhifadhi. Muhifadhi Mwenyezi Mungu, utamkuta mbele yako. Unapoomba, basi muombe Mwenyezi Mungu. Na unapotaka msaada, basi taka msaada kwa Mwenyezi Mungu." Imesimuliwa na Tirmidhii na wengineo.
Alisema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Yeyote atakayekufa huku ana muomba mwenza pamoja na Mwenyezi Mungu, ataingia Motoni." Imesimuliwa na Bukhari. Na imesimuliwa katika vitabu viwili (Sahihi Bukhari na Sahihi Muslim), kwamba Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake aliulizwa: Ni dhambi ipi kubwa zaidi? Akasema: "Kumfanyia Mwenyezi Mungu mwenza (mshirika) ilhali Yeye ndiye aliyekuumba." Kwa hivyo, kila anayemuomba mwingine asiyekuwa Mwenyezi Mungu, au akaomba msaada kwa hicho, au akakiwekea nadhiri, au akakichijia, au akakifanyia ibada ya namna yoyote ile kando na hizi zilizotajwa, basi bila shaka atakuwa amekifanya kuwa mwenza wa Mwenyezi Mungu, sawa awe Nabii, au mtu mtakatifu, au Malaika, au jini, au sanamu, au kiumbe chochote kinginecho.
Hapa mtu anaweza kusema: Ni ipi hukumu ya kumuuliza mtu aliye hai kwa kile anachoweza kufanya, na kutafuta kuokolewa naye katika mambo ya kihisia anayoweza kuyafanya? Jibu ni kwamba hilo sio ushirikina, bali ni jambo la kawaida linaloruhusiwa miongoni mwa Waislamu, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu katika kisa cha Musa:
﴿...فَاسْتَغَاثَهُ الَّذِي مِنْ شِيعَتِهِ عَلَى الَّذِي مِنْ عَدُوِّهِ...﴾
"Basi yule mwenzake akamtaka msaada kumpiga adui yake." [Al-Qasas: 15] Na kama alivyosemwa Mwenyezi Mungu Mtukufu katika kisa cha Musa pia:
﴿فَخَرَجَ مِنْهَا خَائِفًا يَتَرَقَّبُ...﴾
"Basi akatoka humo naye ana hofu, akiangalia huku na huku." [Al-Qaswas: 21] Na kama vile mtu anavyotafuta kuokolewa kutoka kwa marafiki zake katika vita na mambo mengine yanayowatokea watu na ambayo wanahitajiana ndani yake.
Mwenyezi Mungu alimwamrisha Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kuujulisha umma wake kwamba yeye hana uwezo wa kumnufaisha wala kumdhuru yeyote. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿قُلْ إِنَّمَا أَدْعُو رَبِّي وَلَا أُشْرِكُ بِهِ أَحَدًا21 قُلْ إِنِّي لَا أَمْلِكُ لَكُمْ ضَرًّا وَلَا رَشَدًا22﴾
"Sema: 'Hakika mimi ninamuomba Mola wangu Mlezi, wala simshirikishi Yeye na yeyote.' Sema: 'Hakika mimi sina mamlaka ya kukudhuruni wala kukuongozeni.'"
Sema: Mimi sina mamlaka ya kukudhuruni wala kukuongozeni. [Surat Al-Jinn: 21-22] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿قُلْ لَا أَمْلِكُ لِنَفْسِي نَفْعًا وَلَا ضَرًّا إِلَّا مَا شَاءَ اللَّهُ وَلَوْ كُنْتُ أَعْلَمُ الْغَيْبَ لَاسْتَكْثَرْتُ مِنَ الْخَيْرِ وَمَا مَسَّنِيَ السُّوءُ إِنْ أَنَا إِلَّا نَذِيرٌ وَبَشِيرٌ لِقَوْمٍ يُؤْمِنُونَ188﴾
"Sema: Siimilikii nafsi yangu manufaa wala madhara, ila apendavyo Mwenyezi Mungu. Na lau kuwa ninayajua ya ghaibu, ningejizidishia mema mengi, wala ovu lisingenigusa. Mimi si chochote ila ni muonyaji na mbashiri kwa watu wanaoamini." [Surat Al-A'raaf: 188] Na aya zenye maana hii ni nyingi sana.
Na inavyojulikana ni kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, haombi isipokuwa Mola wake Mlezi, kama ilivyothibiti kutoka kwake kwamba siku ya Badri alikuwa anaomba aokolewe na Mwenyezi Mungu na kumuomba nusura dhidi ya maadui zake, na alikuwa akisisitiza juu ya hilo na kusema: “Ewe Mola Mlezi! Nitimizie yale uliyoniahidi." mpaka yule mwenye kusadikisha mkubwa zaidi, Abubakari, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, akasema: "Imetosha ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, kwani hakika Mwenyezi Mungu atakutimizia yale aliyokuahidi." Kisha Mwenyezi Mungu Mtukufu akateremsha kauli hii kuhusiana na hilo:
﴿إِذۡ تَسۡتَغِيثُونَ رَبَّكُمۡ فَٱسۡتَجَابَ لَكُمۡ أَنِّي مُمِدُّكُم بِأَلۡفٖ مِّنَ ٱلۡمَلَٰٓئِكَةِ مُرۡدِفِينَ9﴾
"Mlipokuwa mkimuomba msaada Mola wenu Mlezi, naye akakujibuni kuwa: Kwa yakini Mimi nitakusaidieni kwa Malaika elfu (moja) wanaofuatana mfululizo." [Surat Al-Anfaal: 9] Basi, Yeye aliyetakasika, akawa kumbusha katika Aya hizi kuomba kwao kuokolewa, na akawaambia kuwa aliwaitikia na akawasaidia kwa Malaika; ili wapate habari njema ya ushindi na utulivu, na Yeye - utukufu ni wake - akabainisha kuwa ushindi hautokani na Malaika, bali ushindi hutoka kwake. Akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿وَمَا النَّصْرُ إِلَّا مِنْ عِنْدِ اللَّهِ...﴾
"Na msaada hautoki isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu." [Al-Imran: 126] Na akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿وَلَقَدْ نَصَرَكُمُ اللَّهُ بِبَدْرٍ وَأَنْتُمْ أَذِلَّةٌ فَاتَّقُوا اللَّهَ لَعَلَّكُمْ تَشْكُرُونَ123﴾
"Na hakika Mwenyezi Mungu alikwishakunusuruni katika Badri nanyi mlikuwa wanyonge. Basi mcheni Mwenyezi Mungu ili mpate kushukuru." [Al-Imran: 123]. Basi Yeye Mtukufu akabainisha katika Aya hii kwamba Yeye ndiye aliyewapa nusura Siku ya Badri. Kwa hivyo, ikajulikana kwa hilo kwamba alichowapa cha silaha na nguvu, na Malaika aliowateremshia ili wawasaidie, hivyo vyote ni visababu vya ushindi, habari njema na utulivu, lakini ushindi huo haukutokana na hayo, bali ulitoka kwa Mwenyezi Mungu peke yake. Basi ni vipi anafanya ujasiri mwandishi huyu - au mtu mwingine yeyote - kuelekeza kilio chake cha kuomba kuokolewa na kuomba kwake ushindi kwa Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na kumuacha Mola Mlezi wa walimwengu wote, Mmiliki wa kila kitu na Muweza wa kila kitu?!
Hapana shaka kwamba hili ni miongoni mwa ujinga mbaya zaidi, bali ni katika ushirikina mkubwa zaidi. Basi la wajibu kwa mwandishi huyu ni atubu kwa Mwenyezi Mungu aliyetakasika, kwa toba ya kweli. Na toba ya kweli ni ile inayohusisha mambo kadhaa, ambayo ni: Kwanza: Kujutia yale aliyofanya. Pili: Kuachana na aliyoyafanya. Tatu: Kuazimia kutorejea katika aliyofanya; ili kumpa Mwenyezi Mungu taadhima na kumkusudia Yeye peke yake, kufuata amri yake, na kutahadhari yale aliyokataza. Hii ndiyo toba ya kweli. Na kuna jambo la nne mahsusi iwapo kosa lake hilo linahusiana na haki za viumbe, basi naarudishe haki hiyo kwa mwenyewe, au amuombe amuondolee haki hiyo. Hili ndilo sharti la nne.
Mwenyezi Mungu amewaamrisha waja wake kufanya toba na akaahidi kuikubali, kama alivyosema Mtukufu:
﴿وَتُوبُوا إِلَى اللَّهِ جَمِيعًا أَيُّهَ الْمُؤْمِنُونَ لَعَلَّكُمْ تُفْلِحُونَ31﴾
"Na tubuni nyote kwa Mwenyezi Mungu, enyi Waumini, ili mpate kufanikiwa." [Surat An-Nur: 31] Na alisema kuhusu Wakristo:
﴿أَفَلَا يَتُوبُونَ إِلَى اللَّهِ وَيَسْتَغْفِرُونَهُ وَاللَّهُ غَفُورٌ رَحِيمٌ74﴾
"Je, hawatubu kwa Mwenyezi Mungu na waka muomba msamaha? Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye maghufira (msamaha) na Mwenye kurehemu" [Al-Maaida: 74] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿وَالَّذِينَ لَا يَدْعُونَ مَعَ اللَّهِ إِلَهًا آخَرَ وَلَا يَقْتُلُونَ النَّفْسَ الَّتِي حَرَّمَ اللَّهُ إِلَّا بِالْحَقِّ وَلَا يَزْنُونَ وَمَنْ يَفْعَلْ ذَلِكَ يَلْقَ أَثَامًا68 يُضَاعَفْ لَهُ الْعَذَابُ يَوْمَ الْقِيَامَةِ وَيَخْلُدْ فِيهِ مُهَانًا69 إِلَّا مَنْ تَابَ وَآمَنَ وَعَمِلَ عَمَلًا صَالِحًا فَأُولَئِكَ يُبَدِّلُ اللَّهُ سَيِّئَاتِهِمْ حَسَنَاتٍ وَكَانَ اللَّهُ غَفُورًا رَحِيمًا70﴾
"Na wale wasiomuomba mungu mwingine pamoja na Mwenyezi Mungu, wala hawaui nafsi aliyoiharamisha Mwenyezi Mungu isipokuwa kwa haki, wala hawazini. Na atakayefanya hayo, atapata madhara.
Atazidishiwa adhabu Siku ya Kiyama, na atadumu humo akifedheheshwa.
Isipokuwa atakayetubu, na akaamini, na akatenda vitendo vyema. Basi hao Mwenyezi Mungu atayabadilisha maovu yao yawe mema. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu." [Al-Furqaan: 68-70] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿وَهُوَ الَّذِي يَقْبَلُ التَّوْبَةَ عَنْ عِبَادِهِ وَيَعْفُو عَنِ السَّيِّئَاتِ وَيَعْلَمُ مَا تَفْعَلُونَ25﴾
"Naye ndiye anayepokea toba kwa waja wake, na anasamehe makosa, na anayajua mnayoyatenda." [Ash-Shuura: 25]
Ilithibiti kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake kwamba alisema: "Uislamu unabomoa yale yaliyokuwa kabla yake, na toba inafuta yale yaliyokuwa kabla yake."
Nimeyaandika maneno haya mafupi kwa sababu ya hatari kubwa ya ushirikina, na kwa sababu ndio dhambi kubwa zaidi, na kwa sababu ya hofu ya watu kudanganywa na yale yaliyoandikwa na mwandishi huyu, na kwa sababu ya ulazima wa kunasihi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na kuwanasihi waja wake. Na ninamuomba Mwenyezi Mungu mwenye utukufu mkubwa atunufaishe kwayo, aziboreshe hali zetu na hali za Waislamu wote, atujaalie sisi sote ufahamu wa dini na kuwa imara juu yake, na atulinde sisi na Waislamu wote kutokana na shari za nafsi zetu na ubaya wa matendo yetu. Kwani, Yeye ndiye Msimamizi wa hayo na Mwenye uwezo wa kuyafanya.
Na rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu ya mja wa Mwenyezi Mungu na Mtume wake, Nabii wetu Muhammad, na familia yake na Maswahaba wake.
***
بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَنِ الرَّحِيمِ
Makala ya Tatu
Kuhusu hukumu ya kutafuta msaada kutoka kwa majini na mashetani, na kuweka nadhiri kwa ajili yao.
Kutoka kwa Abdul-Aziz bin Abdullah bin Baaz kwenda kwa yeyote anayeuona (ujumbe huu) miongoni mwa Waislamu, Mwenyezi Mungu aniwezeshe mimi na wao tushikamane na dini yake na kubaki imara juu yake, aamiin.
Assalaam alaikum Warahmatullaahi Wabarakaatuh
Ama baada ya hayo: Baadhi ya ndugu zangu waliniuliza kuhusu kile ambacho baadhi ya watu wajinga hufanya cha kumuomba asiyekuwa Mwenyezi Mungu, na kutafuta msaada wake katika mambo mazito muhimu; kama vile kuwaomba dua majini, kuwataka kuokolewa, kuwawekea nadhiri na kuchinja kwa ajili yao. Na katika hayo pia ni kauli ya baadhi yao: "Enyi saba", na saba ni katika viongozi wa majini, "mchukueni", "mvunjeni mifupa yake", na "kunyweni damu yake", "mkatakateni vipande", "enyi saba, mfanyieni fulani hivi." Au kauli ya baadhi yao: “Mchukueni, enyi majini wa mchana, enyi pepo wa Alasiri.” Haya mara nyingi hupatikana katika baadhi ya maeneo ya kusini (mwa nchi hii). Na mengine yanayohusiana na jambo hili ni kuwaomba dua wafu, wakiwemo Manabii, watu wema na wengineo, na kuwaomba dua Malaika na kuwataka wawaokoe. Yote haya na yanayofanana nayo yanatokea kwa wengi miongoni mwa wale wanaojinasibisha na Uislamu, kwa kutojua na kuwaiga wale waliokuwa kabla yao, na pengine baadhi yao hurahisisha hilo sana na kutumia hoja ya kusema: 'Hili ni jambo linalopita tu juu ya ulimi, na hatulikusudii wala hatuliitakidi.'
Vile vile, akaniuliza kuhusu hukumu ya kuolewa na mtu anayejulikana kwa vitendo hivi, na vichinjwa vyao, na kuwaswalia, na kuswali nyuma yao, na kuhusu kuwasadikisha wachawi na wapiga ramli. Kama mtu anayedai kujua ugonjwa fulani na sababu zake kwa kuangalia tu kitu kilichougusa mwili wa mgonjwa; kama vile kilemba, suruali, kitambaa na mfano wa hivyo.
Jibu: Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu peke yake, na rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie yule ambaye hakuna Nabii baada yake, na juu ya jamaa zake na Maswahaba wake na wote walioongoka kupitia wao mpaka Siku ya Kiyama.
Ama baada ya hayo: Hakika Mwenyezi Mungu Aliyetakasika na kutukuka, aliumba viumbe viwili vizito (majini na wanadamu) ili wamuabudu, na sio kitu kingine chochote, na ili wamuombe Yeye pekee na kumtaka msaada, na kumchinjia, na kumuwekea nadhiri na ibada nyingine zote. Aliwatuma Mitume kuyaleta haya, na akawaamrisha kufanya hivyo, na akateremsha vitabu vya mbinguni, ambavyo kikubwa chake kabisa ni Qur’ani Tukufu, ili kueleza hayo, na kulingania kwayo, na kuwaonya watu dhidi ya kumshirikisha Mwenyezi Mungu na kuabudu asiyekuwa Yeye. Hii ndiyo asili ya asili zote na msingi wa dini na mila ya Kiislamu, na ndiyo maana ya kushuhudia kwamba hakuna mungu ila Mwenyezi Mungu, na uhakika wa hakuna apasaye kuabudiwa kwa haki ila Mwenyezi Mungu. Kwani, inakanusha asifanyiwe uungu na ibada yeyote asiyekuwa Mwenyezi Mungu, na inamthibitishia - yaani ibada - Mwenyezi Mungu peke yake, mbali na chochote miongoni mwa viumbe. Ushahidi wa hayo kutoka katika Kitabu cha Mwenyezi Mungu na Sunnah za Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, ni mwingi sana, ikiwa ni pamoja na: Maneno ya Mwenyezi Mungu Mwenye utukufu mkubwa:
﴿وَمَا خَلَقْتُ الْجِنَّ وَالْإِنْسَ إِلَّا لِيَعْبُدُونِ56﴾
"Nami sikuwaumba majini na watu ila waniabudu Mimi." [Surat Adh-Dhariyaat: 56]. Na kauli yake Mtukufu:
﴿وَقَضَى رَبُّكَ أَلَّا تَعْبُدُوا إِلَّا إِيَّاهُ...﴾
"Na Mola wako Mlezi ameamrisha kuwa msimuabudu yeyote ila Yeye tu." [Surat Al-Israai: 23] Na kauli yake Mtukufu:
﴿وَمَا أُمِرُوا إِلَّا لِيَعْبُدُوا اللَّهَ مُخْلِصِينَ لَهُ الدِّينَ حُنَفَاءَ...﴾
"Nao hawakuamrishwa kitu ila wamuabudu Mwenyezi Mungu kwa kumtakasia Dini, wawe waongofu." [Surat Al-Bayyina: 5] Na kauli yake Mtukufu:
﴿وَقَالَ رَبُّكُمُ ادْعُونِي أَسْتَجِبْ لَكُمْ إِنَّ الَّذِينَ يَسْتَكْبِرُونَ عَنْ عِبَادَتِي سَيَدْخُلُونَ جَهَنَّمَ دَاخِرِينَ60﴾
"Na Mola wenu Mlezi amesema: Niombeni, nitakuitikieni. Kwa hakika wale wanaojivuna kuniabudu Mimi, wataingia Jahannamu wadhalilike." [Surat Ghafir: 60] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿وَإِذَا سَأَلَكَ عِبَادِي عَنِّي فَإِنِّي قَرِيبٌ أُجِيبُ دَعْوَةَ الدَّاعِ إِذَا دَعَانِ...﴾
"Na waja wangu watakapokuuliza kuhusu Mimi, basi Mimi nipo karibu. Naitika maombi ya muombaji anaponiomba." [Al-Baqarah: 186].
Basi Yeye aliyetakasika akabainisha katika Aya hizi kwamba aliumba vitu viwili vizito (majini na watu) ili vimwabudu, na kwamba aliamuru na kuusia waja wake katika Qur’ani iliyo wazi, na kwa ulimi wa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, kwamba asiabudiwe isipokuwa Mola wao Mlezi.
Mwenyezi Mungu Mtukufu alibainisha kuwa dua ni ibada kubwa, na mwenye kutakabari akaiacha, ataingia Motoni. Na akawaamrisha waja wake kumuomba dua Yeye peke yake, na akaeleza kuwa yuko karibu na anajibu dua zao. Basi ikawa ni wajibu kwa waja wote kumkusudia Mola wao Mlezi tu katika dua. Kwa sababu hiyo ni aina ya ibada ambayo wameumbwa kwa ajili yake na wakaamrishwa kuifanya, na akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿قُلْ إِنَّ صَلَاتِي وَنُسُكِي وَمَحْيَايَ وَمَمَاتِي لِلَّهِ رَبِّ الْعَالَمِينَ162 لَا شَرِيكَ لَهُ وَبِذَلِكَ أُمِرْتُ وَأَنَا أَوَّلُ الْمُسْلِمِينَ163﴾
"Sema: 'Hakika Sala yangu, na ibada zangu, na uhai wangu, na kufa kwangu, ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa viumbe vyote.'"
Hana mshirika yeyote. Na hayo ndiyo niliyoamrishwa, na mimi ni wa kwanza wa Waislamu." [Al-An'am: 162-163]
Kwa hivyo, Mwenyezi Mungu akamuamrisha Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kuwajulisha watu kwamba sala yake na ibada zake za kuchinja, na uhai wake na kifo chake ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote, asiye na mshirika. Na kwa mujibu wa hayo, mwenye kuchinja kwa ajili ya asiyekuwa Mwenyezi Mungu, atakuwa amemshirikisha Mwenyezi Mungu, kama vile akiswali kwa ajili ya asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Kwa sababu Mwenyezi Mungu -aliyetakasika- aliifanya swala na kuchinja kuwa vitu viwili vinavyo kwenda kwa pamoja, na akajulisha kwamba viwili hivyo ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu peke yake, asiye na mshirika yeyote. Kwa hivyo, mwenye kuchinja kwa ajili ya asiyekuwa Mwenyezi Mungu, kama vile majini, Malaika, wafu na wengineo kwa kutaka kujiweka karibu nao kwa kufanya hivyo, basi ni sawa na anayeswali kwa ajili ya asiyekuwa Mwenyezi Mungu. Imekuja katika Hadithi sahihi kwamba Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, alisema: "Mwenyezi Mungu amemlaani mwenye kuchinja kwa ajili ya asiyekuwa Mwenyezi Mungu." Na amesimulia Imaam Ahmad kwa Isnadi Hasan (mlolongo mzuri wa wasimulizi) kutoka kwa Twariq bin Shihab, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kutoka kwa Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba alisema: "Wanaume wawili walipita karibu na watu waliokuwa na sanamu ambalo hakuna mtu angeweza kupita hapo mpaka alitolee kitu. Mmoja wao akaambiwa: Toa kitu kwa ajili yake. Akasema: Sina kitu cha kulitolea. Wakasema: Toa hata kama ni nzi. Kwa hivyo, akalitolea nzi, basi wakamwachilia aende zake na akaingia Motoni. Kisha wakamwambia mwenzake: Litolee kitu. Akasema: Siwezi kumtolea kitu yeyote (kwa njia ya ibada) ila Mwenyezi Mungu Mtukufu. Kwa hivyo wakampiga shingo yake (akafa), na akaingia Peponi."
Hivyo basi, ikiwa mwenye kufanya ibada ya kujiweka karibu na sanamu na mfano wake kwa kutoa nzi au mfano wake ni mshirikina anayestahiki kuingia Motoni, basi atakuwa vipi mwenye kuwaomba majini, Malaika na watu wema? Na atakuwa vipi mwenye kuwaomba wamuokoe, akawawekea nadhiri na akajisogeza karibu nao kwa vichinjwa, kwa kutaraji kuhifadhi mali yake kwa kufanya hivyo, au kumponya mgonjwa wake, au kuwafanya wanyama wake na mazao yake kuwa salama? Na atakuwa vipi mwenye kufanya hivyo kwa kuhofu shari za majini, au kitu kama hicho?! Hakuna shaka kwamba mwenye kufanya hivyo na wengine kama yeye, wanastahiki zaidi kuwa washirikina, wanaostahiki kuingia Motoni kuliko mtu huyu aliyelipa sanamu nzi kwa njia ya ibada.
Miongoni mwa yaliyokuja katika suala hili - pia - ni kauli ya Mola Mtukufu:
﴿إِنَّآ أَنزَلۡنَآ إِلَيۡكَ ٱلۡكِتَٰبَ بِٱلۡحَقِّ فَٱعۡبُدِ ٱللَّهَ مُخۡلِصٗا لَّهُ ٱلدِّينَ2 أَلَا لِلَّهِ ٱلدِّينُ ٱلۡخَالِصُۚ وَٱلَّذِينَ ٱتَّخَذُواْ مِن دُونِهِۦٓ أَوۡلِيَآءَ مَا نَعۡبُدُهُمۡ إِلَّا لِيُقَرِّبُونَآ إِلَى ٱللَّهِ زُلۡفَىٰٓ إِنَّ ٱللَّهَ يَحۡكُمُ بَيۡنَهُمۡ فِي مَا هُمۡ فِيهِ يَخۡتَلِفُونَۗ إِنَّ ٱللَّهَ لَا يَهۡدِي مَنۡ هُوَ كَٰذِبٞ كَفَّارٞ3﴾
"Hakika Sisi tumekuteremshia Kitabu hiki kwa Haki. Basi muabudu Mwenyezi Mungu ukimsafia Dini Yeye tu."
Sikilizeni. Hakika Dini Safi ni ya Mwenyezi Mungu tu. Na wale wanaowafanya wenginewe kuwa ni walinzi wakisema: Sisi hatuwaabudu ila wapate kutujongeza tu kumkaribia Mwenyezi Mungu - Hakika Mwenyezi Mungu atahukumu baina yao katika yale wanayohitilafiana. Hakika Mwenyezi Mungu hamuongoi aliye muongo kafiri." [Az-zumar: 1-3] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿وَيَعْبُدُونَ مِنْ دُونِ اللَّهِ مَا لَا يَضُرُّهُمْ وَلَا يَنْفَعُهُمْ وَيَقُولُونَ هَؤُلَاءِ شُفَعَاؤُنَا عِنْدَ اللَّهِ قُلْ أَتُنَبِّئُونَ اللَّهَ بِمَا لَا يَعْلَمُ فِي السَّمَاوَاتِ وَلَا فِي الْأَرْضِ سُبْحَانَهُ وَتَعَالَى عَمَّا يُشْرِكُونَ18﴾
"Nao, badala ya Mwenyezi Mungu, wanaabudu wasiowadhuru wala kuwanufaisha, na wanasema: Hawa ndio waombezi wetu kwa Mwenyezi Mungu! Sema: Je, mnamwambia Mwenyezi Mungu asiyoyajua yaliyoko katika mbingu wala katika ardhi? Sub-hanahu wa Taala (Ametakasika na ametukuka) mbali na hao wanaomshirikisha naye." [Yunus: 18]
Basi Mwenyezi Mungu Mtukufu akajulisha katika Aya hizi mbili kwamba washirikina walichukua kinyume na Mwenyezi Mungu walinzi miongoni mwa viumbe, wakiwaabudu pamoja naye kwa kuwahofu, kuwatumaini, kuwachinjia, kuwawekea nadhiri, kuwaomba dua na mfano wa hayo, wakidai kuwa walinzi hao wanawaweka wale wanaowaabudu karibu na Mwenyezi Mungu na wanawafanyia uombezi kwake. Basi Mwenyezi Mungu aliyetakasika akawakadhibisha na akabainisha batili zao hizo, na akawaita waongo, makafiri na washirikina, na akajitakasa mbali na ushirikina wao huo.
Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿...سُبْحَانَهُ وَتَعَالَى عَمَّا يُشْرِكُونَ﴾
"Ametakasika na ametukuka mbali na hao wanao mshirikisha naye." [An-Nahli: 1]. Basi ikajulikana kutokana na hayo kwamba mwenye kumchukua Malaika, au Nabii, au jini, au mti au jiwe na akaviomba pamoja na Mwenyezi Mungu, na akavitaka msaada, na akajikurubisha kwavyo kwa nadhiri na kuchinja kwa kutaraji uombezi wake kwa Mwenyezi Mungu, na kumjongeza kwake, au kutaraji kuponya wagonjwa, au kuhifadhi mali, au usalama wa asiyekuwapo, au mengineyo, basi hakika atakuwa ameanguka katika ushirikina huu mkubwa na balaa la kutisha, ambalo Mwenyezi Mungu alisema juu yake:
﴿إِنَّ اللَّهَ لَا يَغْفِرُ أَنْ يُشْرَكَ بِهِ وَيَغْفِرُ مَا دُونَ ذَلِكَ لِمَنْ يَشَاءُ وَمَنْ يُشْرِكْ بِاللَّهِ فَقَدِ افْتَرَى إِثْمًا عَظِيمًا48﴾
"Hakika Mwenyezi Mungu hasamehe kushirikishwa, na husamehe yaliyo chini ya hilo kwa amtakaye. Na anayemshirikisha Mwenyezi Mungu, basi hakika amezua dhambi kubwa." [An-Nisaa: 48]. Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿إِنَّهُ مَنْ يُشْرِكْ بِاللَّهِ فَقَدْ حَرَّمَ اللَّهُ عَلَيْهِ الْجَنَّةَ وَمَأْوَاهُ النَّارُ وَمَا لِلظَّالِمِينَ مِنْ أَنْصَارٍ72﴾
"Kwani anayemshirikisha Mwenyezi Mungu, hakika Mwenyezi Mungu atamharamishia Pepo, na mahala pake ni Motoni. Na waliodhulumu hawatakuwa na wa kuwanusuru." [Al-Ma’idah: 72].
Uombezi Siku ya Kiyama utatolewa tu kwa ajili ya watu wa tauhidi na ikhlasi, si kwa watu wa ushirikina, kama alivyosema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alipoulizwa: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu! Ni nani kati ya watu wote atakaye furahia uombezi wako? Akasema: "Atakayesema: 'Laa ilaaha illa llaahu (Hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu)' likiwa limetoka moyoni mwake kwa utakasifu kabisa." Alisema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Kila Nabii ana dua inayojibiwa. Basi kila Nabii akaharakisha kuomba dua yake. Nami nimeihifadhi dua yangu iwe ni uombezi kwa ajili ya umma wangu Siku ya Kiyama, nayo itampata -Mwenyezi Mungu akipenda- kila atakayekufa katika umma wangu huku hamshirikishi Mwenyezi Mungu na chochote."
Washirikina wa mwanzo walikuwa wakiamini kuwa Mwenyezi Mungu ndiye Mola wao Mlezi, Muumba na Mruzuku wao. Walitegemea tu Mitume, na watu wema, na Malaika, na miti, na mawe na mfano wa hivyo wakitarajia uombezi wao kwa Mwenyezi Mungu na kuwakurubisha kwake, kama ilivyotajwa hapo awali kwenye aya mbali mbali. Kwa hivyo, Mwenyezi Mungu hakuwapa udhuru kwa hilo. Bali aliwakanusha katika hilo kwenye Kitabu chake kitukufu, na akawaita makafiri na washirikina, na akawakadhibisha katika kudai kwao kwamba miungu hao wanawaombea na kuwakurubisha kwa Mwenyezi Mungu wawe karibu zaidi. Pia Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake hakuwapa udhuru. Bali aliwapiga vita juu ya ushirikina huu mpaka wamfanyie Mwenyezi Mungu peke yake ibada, na kwa mujibu wa kauli ya Mwenyezi Mungu aliyetakasika:
﴿وَقَاتِلُوهُمْ حَتَّى لَا تَكُونَ فِتْنَةٌ وَيَكُونَ الدِّينُ لِلَّهِ...﴾
"Na piganeni nao mpaka pasiwepo fitina, na Dini iwe ya Mwenyezi Mungu tu." [Al-Baqara: 193]. Na amesema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Nimeamrishwa nipigane vita na watu mpaka washuhudie kuwa hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu na kuwa Muhammadi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu, na wadumishe swala, na watoe zaka. Basi pindi watakapofanya hivyo, watakuwa wamezikinga kutokana nami damu zao na mali zao isipokuwa kwa haki ya Uislamu, na hesabu yao itakuwa juu ya Mwenyezi Mungu Mtukufu." Maana ya kauli ya Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Mpaka washuhudie kuwa hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu"
Yaani: Mpaka wamkusudie Mwenyezi Mungu peke yake katika ibada, pasina kila kitu kisichokuwa Yeye.
Washirikina walikuwa wakiwaogopa majini na wana jikinga kwao. Basi Mwenyezi Mungu Mtukufu akateremsha maneno yake haya kuhusu hilo:
﴿وَأَنَّهُ كَانَ رِجَالٌ مِنَ الْإِنْسِ يَعُوذُونَ بِرِجَالٍ مِنَ الْجِنِّ فَزَادُوهُمْ رَهَقًا6﴾
"Na hakika walikuwako wanaume katika watu waliokuwa wakitafuta kujikinga kwa wanaume wa kijini; kwa hivyo wakawazidishia madhambi." [Al-Jin: 6]. Wafasiri walisema kuhusu Aya hii tukufu: Maana ya kauli yake:
﴿...فَزَادُوهُمْ رَهَقًا﴾
"Kwa hivyo wakawazidishia madhambi." Yaani: Uoga na hofu; kwa sababu majini hujiona wakubwa na wanatakabari wanapowaona watu wanakimbilia kwao, na hapo wanawaongezea hofu na uoga ili wawaabudu kwa wingi na kutafuta kimbilio kwao.
Na Mwenyezi Mungu aliwageuzia Waislamu badala ya hilo kutafuta kimbilio kwake Yeye aliyetakasika, na kwa maneno yake makamilifu, na akateremsha kuhusiana na hilo kauli yake Mtukufu:
﴿وَإِمَّا يَنْزَغَنَّكَ مِنَ الشَّيْطَانِ نَزْغٌ فَاسْتَعِذْ بِاللَّهِ إِنَّهُ سَمِيعٌ عَلِيمٌ200﴾
"Na uchochezi wa Shetani ukikuchochea, basi omba ulinzi wa Mwenyezi Mungu. Hakika Yeye ni Msikivu, Mjuzi." [Al-A'araf: 200]. Na kauli yake Mtukufu:
﴿قُلْ أَعُوذُ بِرَبِّ الْفَلَقِ1﴾
"Sema: Ninajikinga kwa Mola Mlezi wa mapambazuko" Na imepokelewa kwa njia sahihi kwamba Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie, alisema: "Atakayeshuka mahala popote kisha akasema: 'A'udhu bikalimaati-llaahit-taammaati min sharri maa khalaqa: Tafsiri: Najilinda kwa maneno ya Mwenyezi Mungu yaliyotimia, kutokana na uovu wa vile alivyo viumba, hakitomdhuru chochote mpaka atakapoondoka mahala pake hapo."
Kutokana na Aya na Hadithi zilizotangulia, mtafutaji wa uokovu, na mwenye kutaka kuihifadhi dini yake na kusalimika kutokana na ushirikina uliofichikana na ulio wazi atajua kwamba kujifungamanisha na wafu, Malaika, na majini na viumbe wengineo, na kuwaomba dua, na kujikinga kwao na mengineyo, ni miongoni mwa matendo ya washirikina wa enzi ya ujahilia (ujinga), na ni miongoni mwa aina mbaya kabisa za kumshirikisha Mwenyezi Mungu Mtukufu. Kwa hivyo, la wajibu ni kuyaacha, kujihadhari nayo, na watu kuusiana kuyaacha na kumkemea yeyote anayeyafanya.
Na ama anayejulikana miongoni mwa watu kwa vitendo hivi vya kishirikina, basi hairuhusiwi kumuoa, wala kula kichinjwa chake, wala kumswalia, wala kuswali nyuma yake, mpaka atangaze toba kutokana na hayo kwa Mwenyezi Mungu aliyetakasika, na amkusudie Mwenyezi Mungu peke yake katika dua na ibada. Kwani dua ndiyo ibada, bali ndio kiini chake, kama alivyosema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Dua ndiyo ibada." Na imepokelewa kutoka kwake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, katika maneno mengine kwamba alisema: "Dua ndiyo kiini cha ibada." Ama kuwaowa washirikina, amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿وَلَا تَنْكِحُوا الْمُشْرِكَاتِ حَتَّى يُؤْمِنَّ وَلَأَمَةٌ مُؤْمِنَةٌ خَيْرٌ مِنْ مُشْرِكَةٍ وَلَوْ أَعْجَبَتْكُمْ وَلَا تُنْكِحُوا الْمُشْرِكِينَ حَتَّى يُؤْمِنُوا وَلَعَبْدٌ مُؤْمِنٌ خَيْرٌ مِنْ مُشْرِكٍ وَلَوْ أَعْجَبَكُمْ أُولَئِكَ يَدْعُونَ إِلَى النَّارِ وَاللَّهُ يَدْعُو إِلَى الْجَنَّةِ وَالْمَغْفِرَةِ بِإِذْنِهِ وَيُبَيِّنُ آيَاتِهِ لِلنَّاسِ لَعَلَّهُمْ يَتَذَكَّرُونَ221﴾
"Wala msiwaoe wanawake washirikina mpaka waamini. Na mjakazi Muumini ni bora kuliko mshirikina hata akikupendezeni. Wala msiwaoze (binti zenu) wanaume washirikina mpaka waamini. Na mtumwa mwanamume Muumini ni bora kuliko mshirikina hata akikupendezeni. Hao wanaitia kwenye Moto, na Mwenyezi Mungu anaitia kwenye Pepo na maghufira (msamaha) kwa idhini yake. Naye huzibainisha Aya zake kwa watu ili wapate kukumbuka." [Al-Baqarah: 221]. Hapa, Mwenyezi Mungu Mtukufu amekataza Waislamu kuoa wanawake washirikina, wanoabudu masanamu, majini, Malaika na vinginevyo, mpaka waamini kwa kumkusudia Mwenyezi Mungu pekee katika ibada, na kumsadikisha Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, katika yale aliyokuja nayo na kufuata njia yake. Na pia akakataza kuwaozesha wanaume washirikina wanawake wa Kiislamu, mpaka waamini kwa kumkusudia Mwenyezi Mungu pekee katika ibada, na kumsadikisha Mtume, rehema na amani ziwe juu yake na kufuata njia yake.
Na Mwenyezi Mungu Mtukufu alieleza kuwa mjakazi Muumini ni bora kuliko mwanamke mshirikina aliye huru, hata kama atampendeza anayemtazama na kusikia maneno yake kwa urembo wake na uzuri wa maneno yake, na kwamba mtumwa Muumini ni bora kuliko mwanamume mshirikina aliye huru, hata kama atampendeza msikilizaji na mtazamaji wake kwa uzuri wake, ufasaha wake na ujasiri na mambo mengine. Kisha akaeleza sababu za ubora huu kwa kauli yake aliyetakasika:
﴿...أُولَئِكَ يَدْعُونَ إِلَى النَّارِ...﴾
"Hao wanaitia kwenye Moto." [Al-Baqara: 221]. Akimaanisha washirikina wanaume na wanawake. Kwa sababu wao ni walinganizi wa kwenda Motoni kwa kauli zao, vitendo vyao, mwenendo wao na maadili yao. Ama Waumini wanaume na Waumini wanawake, hao ni katika walinganizi wa kwenda Peponi kwa maadili yao, matendo yao na mwenendo wao. Basi vipi hawa na hao watakuwa sawa?
Na ama kuhusu kuwaswalia washirikina, Mwenyezi Mungu Mwenye utukufu mkubwa amesema kuhusu wanafiki:
﴿وَلَا تُصَلِّ عَلَى أَحَدٍ مِنْهُمْ مَاتَ أَبَدًا وَلَا تَقُمْ عَلَى قَبْرِهِ إِنَّهُمْ كَفَرُوا بِاللَّهِ وَرَسُولِهِ وَمَاتُوا وَهُمْ فَاسِقُونَ84﴾
"Wala usimsalie kabisa yeyote katika wao akifa, wala usisimame kaburini kwake. Hakika hao wamemkataa Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na wakafa na hali ni wapotofu." [At-Tauba: 84] Kwa hivyo Yeye Mtukufu akabainisha katika Aya hii tukufu kwamba mnafiki na kafiri hawafai kuswaliwa. Kwa sababu wamemkataa Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Basi vile vile haifai kuswali nyuma yao, wala wasifanywe viongozi wa Waislamu. Kwa sababu ya ukafiri wao na kukosa kwao uaminifu, na kwa sababu ya uadui mkubwa ulio baina yao na Waislamu, na kwa sababu wao si katika watu wa kuswali na kuabudu. Kwa sababu hakuna tendo linalosalia pamoja na ukafiri na ushirikina. Tunamuomba Mwenyezi Mungu atusalimishe kutokana na hayo. Na ama kuhusu kula vichinjo vya washirikina, Mwenyezi Mungu Mtukufu Mwenye utukufu mkubwa alisema, akieleza kuharamishwa kwa wanyama waliokufa wenyewe na vichinjo vya washirikina:
﴿وَلَا تَأْكُلُوا مِمَّا لَمْ يُذْكَرِ اسْمُ اللَّهِ عَلَيْهِ وَإِنَّهُ لَفِسْقٌ وَإِنَّ الشَّيَاطِينَ لَيُوحُونَ إِلَى أَوْلِيَائِهِمْ لِيُجَادِلُوكُمْ وَإِنْ أَطَعْتُمُوهُمْ إِنَّكُمْ لَمُشْرِكُونَ121﴾
"Wala msile katika wale ambao hawakusomewa jina la Mwenyezi Mungu. Kwani huo ni upotofu. Na kwa yakini mashetani wanawafunza marafiki zao kubishana nanyi. Na mkiwafuata, basi hapana shaka nyinyi mtakuwa washirikina." [Al-An'am: 121]. Basi Mwenyezi Mungu Mtukufu aliwakataza Waislamu kula wanyama waliokufa bila ya kuchinjwa kisheria na vichinjo vya washirikina. Kwa sababu hivyo ni najisi, kwani vichinjo vyao vina hukumu ya wanyama waliokufa bila ya kuchinjwa kisheria hata kama jina la Mwenyezi Mungu litatajwa juu yake. Kwa sababu kuwatajia jina la Mwenyezi Mungu ni batili na halina athari yoyote juu yake. Kwa sababu hii ni ibada, na ushirikina unavunjilia mbali na kubatilisha ibada, mpaka mshirikina atubie kwa Mwenyezi Mungu aliyetakasika. Mwenyezi Mungu Mtukufu ameruhusu tu chakula cha Watu wa Kitabu katika kauli yake:
﴿...وَطَعَامُ الَّذِينَ أُوتُوا الْكِتَابَ حِلٌّ لَكُمْ وَطَعَامُكُمْ حِلٌّ لَهُمْ...﴾
"Na chakula cha wale waliopewa Kitabu ni halali kwenu, na chakula chenu ni halali kwao." [Al-Maidah: 5] Kwa sababu wanajinasibisha na dini ya mbinguni, na wanadai kuwa wao ni wafuasi wa Musa na Isa, ijapokuwa wanasema uongo katika hilo. Mwenyezi Mungu aliifuta dini yao na kuibatilisha kwa kumtuma Muhammad, rehema na amani ziwe juu yake kwa watu wote, lakini Mwenyezi Mungu Mtukufu, alituhalalishia chakula na wanawake wa Watu wa Kitabu kwa sababu ya hekima ya kina, na siri zilizozingatiwa, ambazo wanazuoni wamezieleza, tofauti na washirikina wanaoabudu masanamu na wafu miongoni mwa manabii na mawalii na wengineo. Kwa sababu dini yao haina msingi, wala hata shaka juu yake. Bali ni ya batili tokea msingi wake. Ndiyo maana vichinjwa vya watu wake ni nyamafu na hairuhusiwi kuvila.
Ama mtu kumwambia mwingine: "Jini amekusibu" “Jini amekuchukua”, “Shetani amepeperuka nawe” na mfano wake, hayo ni aina ya matusi na hayaruhusiwi kati ya Waislamu, kama aina nyingine zote za matusi. Hayo hayazingatiwi kuwa ni ushirikina, isipokuwa ikiwa mwenye kusema hivi anaamini kwamba majini wana watawala watu bila ya idhini ya Mwenyezi Mungu na mapenzi yake, kwa hivyo, mwenye kuamini haya kuhusu majini au viumbe wengineo, anakuwa kafiri kwa sababu ya imani hii. Kwa sababu Mwenyezi Mungu aliyetakasika ndiye Mwenye kumiliki kila kitu, na Muweza wa kila kitu, na Yeye ndiye mwenye kunufaisha na kudhuru, na hakuna kitu kinachoweza kupatikana isipokuwa kwa idhini yake, na kwa kutaka kwake, na mipango yake iliyotangulia, kama alivyosema Mtukufu akimuamrisha Mtume wake, rehema na amani ziwe juu yake kwamba awaambie watu juu ya msingi huu mkuu:
﴿قُلْ لَا أَمْلِكُ لِنَفْسِي نَفْعًا وَلَا ضَرًّا إِلَّا مَا شَاءَ اللَّهُ وَلَوْ كُنْتُ أَعْلَمُ الْغَيْبَ لَاسْتَكْثَرْتُ مِنَ الْخَيْرِ وَمَا مَسَّنِيَ السُّوءُ إِنْ أَنَا إِلَّا نَذِيرٌ وَبَشِيرٌ لِقَوْمٍ يُؤْمِنُونَ188﴾
"Sema: Siimilikii nafsi yangu manufaa wala madhara, ila apendavyo Mwenyezi Mungu. Na lau kuwa ninayajua ya ghaibu, ningejizidishia mema mengi, wala ovu lisingenigusa. Mimi si chochote ila ni muonyaji na mbashiri kwa watu wanaoamini." [Al-A'araf: 188] Kwa hivyo, ikiwa bwana wa viumbe na mbora wao -rehema na amani ziwe juu yake- hajimilikii manufaa wala madhara isipokuwa apendavyo Mwenyezi Mungu, basi itakuwa vipi kuhusu viumbe vingineo? Na kuna aya nyingi katika maana hii.
Ama kuwauliza wapiga ramli, na wachawi, na wanajimu, na mfano wao miongoni mwa wale wanao shughulika na habari za ghaibu, huu ni uovu na wala hauruhusiwi, na tena kuwasadikisha ni kubaya zaidi na ni uovu mno. Bali ni katika matawi ya ukafiri; kama alivyosema Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Atakayemuendea mpiga ramli na akamuuliza kuhusu lolote, basi hatakubaliwa swala yoyote siku arobaini." Imepokelewa na Imamu Muslim katika Sahihi yake. Na katika Sahihi yake – pia – kutoka kwa Muawia bin Al-Hakam As-Sulami, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi kwamba: "Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie, alikataza kumwendea mpiga ramli na kumuuliza kitu."
Watu wa vitabu vya Sunna wamepokea kutoka kwa Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake kwamba alisema: "Atakayemuendea kuhani na akamsadikisha kwa yale anayoyasema, basi hakika atakuwa amekufuru yale yaliyoteremshwa kwa Muhammad rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake." Na kuna hadithi nyingi zenye maana hii. Kwa hivyo ni wajibu kwa Waislamu kutahadhari kuwauliza makuhani na wapiga ramli, na wachawi na wengineo wote ambao wanashughulika na kusimulia mambo ya ghaibu na ya kuwahadaa na kuwachanganya Waislamu, sawa iwe kwa jina la utabibu au mengineyo, kwa sababu ya yale yaliyotangulia kutajwa kuhusu katazo la Mtume rehema na amani ziwe juu yake juu ya hayo na onyo lake dhidi yake. Na yanaingia katika hayo yale wanayodai baadhi ya watu kwa jina la utabibu miongoni mwa mambo ya ghaibu anaponusa harufu ya kilemba cha mgonjwa, au kitambaa cha mgonjwa, au kitu kama hicho, anasema: 'Mgonjwa huyu wa kiume au wa kike alifanya hivi na vile', akitaja mambo ya ghaibu ambayo hakuna ushahidi wake katika kilemba cha mgonjwa huyo. Bali makusudio ya hayo ni kuwahadaa na kuuchanganya umma, ili waseme kuwa yeye ni mjuzi wa matibabu na aina za maradhi na sababu zake, na pengine akawapa baadhi ya madawa, na huenda kwa bahati wakaponywa kwa mapenzi ya Mwenyezi Mungu, basi wakadhani kuwa ni kwa sababu ya dawa zake hizo. Na huenda maradhi hayo yakawa yamesababishwa na baadhi ya majini na mashetani wanaomtumikia mdai huyo katika utabibu wake na wanamwambia baadhi ya mambo ya ghaibu wanayoyajua, basi yeye akategemea hayo na akawaridhisha majini hao na mashetani kwa yale yanayowafaa katika ibada, hivyo basi wakamuondoka mgonjwa huyo na kuachana na madhara waliyomfanyia, na hili ni jambo linalojulikana kuhusu majini na mashetani na wale wanaowatumia.
Hivyo basi, la wajibu pia kwa Waislamu ni kujihadhari na jambo hili, na kuusiana kuachana nalo, na kumtegemea Mwenyezi Mungu Mtukufu katika mambo yote. Na hakuna ubaya kutumia ruqya ya kisheria na dawa zinazozuhusika na kutafuta tiba kwa madaktari ambao humchunguza mgonjwa na kuthibitisha maradhi yake kwa kutumia njia zinazoonekana na za kihisia za kueleweka. Imepokelewa kwa usahihi kwamba Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie, alisema: "Mwenyezi Mungu hakuteremsha ugonjwa isipokuwa aliuteremshia tiba yake. Aliijua aliyeijua na akakosa kuijia yule aliyekosa kuijua." Na alisema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Kila ugonjwa una dawa. Kwa hivyo, ikiwa ugonjwa utapatwa na dawa, basi utapona kwa idhini ya Mwenyezi Mungu." Na alisema Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake: "Enyi waja wa Mwenyezi Mungu, tafuteni matibabu, lakini msitafute matibabu kwa yale yaliyoharamishwa." Na kuna hadithi nyingi zenye maana hii.
Tunamuomba Mwenyezi Mungu Mtukufu aziboreshe hali za Waislamu wote, aziponye nyoyo na miili yao kutokana na maovu yote, awaunganishe juu ya uongofu, na atuepushe sisi na wao kutokana na majaribu ya kupotosha na kumtii Shetani na wafuasi wake. Hakika Yeye ni Muweza wa kila kitu, na hakuna uwezo wala nguvu ila kwa Mwenyezi Mungu aliye juu, Mtukufu.
Na rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu ya mja wa Mwenyezi Mungu na Mtume wake, Nabii wetu Muhammad, na familia yake na Maswahaba wake.
***
بِسْمِ اللَّهِ الرَّحْمَنِ الرَّحِيمِ
Makala ya Nne:
Kuhusu hukumu ya kuabudu kwa kutumia nyiradi za kiuzushi na za kishirikina
Kutoka kwa Abdul-Aziz bin Abdullah bin Baaz kwenda kwa ndugu yetu mtukufu (.....), Mwenyezi Mungu amuwezeshe kufikia kila la heri, Amin.
Assalaam alaikum Warahmatullahi Wabarakaatuh.
Sasa basi: Imenifikia barua yako tukufu, Mwenyezi Mungu akuongoze, na habari zilizomo ndani yake kwamba wako watu katika nchi yako wanaoshikamana na nyiradi ambazo Mwenyezi Mungu hakuziteremshia uthibitisho wowote, baadhi yake ni za kizushi na baadhi yake ni za kishirikina, na wananasibisha hilo kwa amiri wa waumini Ali bin Abi Twalib, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, na wengineo. Dua hizo wanazisoma katika mikusanyiko ya dhikiri, au misikitini baada ya swala ya Magharibi, wakidai kuwa ni kitendo cha kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu, kama vile kusema: Kwa haki ya Mwenyezi Mungu, enyi watu wa Mwenyezi Mungu, tusaidieni kwa msaada wa Mwenyezi Mungu, na kuweni wasaidizi wetu kupitia kwa Mwenyezi Mungu. Na kama wasemavyo: Enyi miti mitukufu, enyi mabwana, itikieni enyi mlio na usaidizi miongoni mwetu, na muombeeni kwa Mwenyezi Mungu, huyu ni mja wenu amesimama, na amejitolea kukaa mlangoni kwenu, na anaogopa mapungufu yake, tusaidie ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, na mimi sina wa kwenda kwake asiyekuwa nyinyi, na kutoka kwenu maombi yanapatikana, na nyinyi ni watu wa Mwenyezi Mungu, kupitia kwa Hamza, bwana wa mashahidi, na ni nani asiyekuwa nyinyi anayeweza kutunusuru sisi, tusaidie ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu. Na kama wanavyosema: Ewe Mwenyezi Mungu mpe rehema yule uliyemfanya kuwa sababu ya kugawanyika kwa siri zako kuu na kufichuka kwa nuru zako za rehema, hivyo akawa mwakilishi wa uwepo wa Mola Mlezi, na mrithi wa siri zako za dhati.
Na kutaka kwenu kubainishiwa ni yapi ya uzushi na yapi ni ya ushirikina, na je ni sahihi kuswalia nyuma ya imamu anayeomba dua hii, ikiwa hayo yote yanajulikana?
Jibu: Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu peke yake, na rehema na amani zimshukie yule ambaye hakuna Nabii baada yake, na juu ya jamaa zake na Maswahaba wake, na wanaofuata uongofu wake mpaka Siku ya Kiyama.
Ama baada ya hayo: Basi jua -Mwenyezi Mungu akuongoze- kwamba Mwenyezi Mungu aliyetakasika aliumba viumbe na akatuma Mitume -rehema na amani ziwe juu yao- ili Yeye peke yake aabudiwe, bila ya mshirika mbali na chochote kisichokuwa Yeye, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿وَمَا خَلَقْتُ الْجِنَّ وَالْإِنْسَ إِلَّا لِيَعْبُدُونِ56﴾
"Nami sikuwaumba majini na watu ila waniabudu Mimi." [Dhariyat: 56].
Na ibada kama ilivyotangulia kubainishwa ni kumtii Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kumtii Mtume wake Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwa kufanya yale aliyoyaamrisha Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na kuyaacha aliyoyakataza Mwenyezi Mungu na Mtume wake, kwa sababu ya kumuamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na kumtakasia Mwenyezi Mungu vitendo, pamoja na kumpenda sana Mwenyezi Mungu, na kujidhalilisha kikamilifu kwake peke yake. Kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿وَقَضَى رَبُّكَ أَلَّا تَعْبُدُوا إِلَّا إِيَّاهُ...﴾
"Na Mola wako Mlezi ameamrisha kuwa msimuabudu yeyote ila Yeye tu." [Al-Israa: 23]. Yaani aliamrisha na kuusia kwamba aabudiwe Yeye peke yake tu. Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿الْحَمْدُ لِلَّهِ رَبِّ الْعَالَمِينَ2 الرَّحْمَنِ الرَّحِيمِ3 مَالِكِ يَوْمِ الدِّينِ4 إِيَّاكَ نَعْبُدُ وَإِيَّاكَ نَسْتَعِينُ5﴾
"Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote.
Mwingi wa rehema, Mwingi wa kurehemu.
Mwenye kumiliki Siku ya Malipo."
5. Ni Wewe tu tunayekuabudu na ni Wewe tu tunayekuomba msaada." [Al-Fatiha 2-5] Kwa hivyo, Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kutukuka akaweka wazi katika aya hizi kwamba Yeye pekee ndiye anayestahiki kuabudiwa na kuombwa msaada. Na akasema Mwenyezi Mungu Mwenye utukufu mkubwa:
﴿إِنَّآ أَنزَلۡنَآ إِلَيۡكَ ٱلۡكِتَٰبَ بِٱلۡحَقِّ فَٱعۡبُدِ ٱللَّهَ مُخۡلِصٗا لَّهُ ٱلدِّينَ2 أَلَا لِلَّهِ ٱلدِّينُ ٱلۡخَالِصُۚ...﴾
"Hakika Sisi tumekuteremshia Kitabu hiki kwa Haki. Basi muabudu Mwenyezi Mungu ukimsafia Dini Yeye tu. Hakika Dini Safi ni ya Mwenyezi Mungu tu."
Hakika Dini Safi ni ya Mwenyezi Mungu tu... [Az-Zumar: 2-3]. Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿فَادْعُوا اللَّهَ مُخْلِصِينَ لَهُ الدِّينَ وَلَوْ كَرِهَ الْكَافِرُونَ14﴾
"Basi muombeni Mwenyezi Mungu mkimsafia Dini Yeye tu, hata kama watachukia makafiri." [Surat Ghafir: 14] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿وَأَنَّ الْمَسَاجِدَ لِلَّهِ فَلَا تَدْعُوا مَعَ اللَّهِ أَحَدًا18﴾
"Na kwamba kwa hakika misikiti ni ya Mwenyezi Mungu. Basi msimuabudu yeyote pamoja na Mwenyezi Mungu." [Surat Al-Jinn: 18]
Kuna aya nyingi katika maana hii, na zote zinaonyesha ulazima wa kumpwekesha Mwenyezi Mungu katika ibada.
Inajulikana kuwa dua kwa aina zake zote ni ibada, na hairuhusiwi kwa mtu yeyote kumuomba yeyote isipokuwa Mola wake Mlezi, wala kuomba msaada na kuokolewa kwa yeyote isipokuwa kutoka kwake, kwa kufanyia kazi Aya hizi tukufu na yale yaliyokuja na maana hii hii. Haya ni kuhusiana na mambo ya kawaida na sababu za kihisia ambazo kiumbe kilicho hai, kilichopo sasa kinayaweza, kwa kuwa hizo si katika ibada. Bali inajuzu kwa maandiko na makubaliano ya wanazuoni kwamba mtu anaweza kutafuta msaada kutoka kwa mtu aliye hai, mwenye uwezo, katika mambo ya kawaida ambayo ana uwezo nayo. Kama vile kutafuta msaada wake ili kuepusha maovu ya mwanawe, au mtumishi, au mbwa, au mfano wa hayo. Na pia kama vile mtu kutafuta msaada kutoka kwa mtu aliye hai, aliyepo, mwenye uwezo, au mtu asiyekuwepo, kupitia njia za kihisia kama vile kuandikiana na mfano wake, katika kujenga nyumba yake, au kutengeneza gari lake au mambo kama hayo. Na katika hayo ni mtu kutafuta kuokolewa kutoka kwa ndugu zake katika jihadi, vita na mfano wa hayo. Na pia katika mlango huu, ni kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu katika kisa cha Musa, rehema na amani ziwe juu yake:
﴿...فَاسْتَغَاثَهُ الَّذِي مِنْ شِيعَتِهِ عَلَى الَّذِي مِنْ عَدُوِّهِ...﴾
"Basi yule mwenzake akamtaka msaada kumpiga adui yake." [Al-Qasas: 15].
Ama kutafuta kuokolewa na wafu, majini, Malaika, miti na mawe, haya ni katika ushirikina mkubwa, na ni aina moja na matendo waliyokuwa washirikina wa mwanzo wakiwafanyia miungu wao, kama vile al-Uzza, al-Lata na wengineo. Na vile vile kutafuta kuokolewa na kusaidiwa na wale anaoamini kwamba wana ulinzi kati ya walio hai, katika mambo ambayo Mwenyezi Mungu pekee ndiye mwenye uwezo juu yake kama vile kuponya wagonjwa, kuongoa nyoyo, kuingia Peponi, kuokoka na Moto na mfano wa hayo.
Aya zilizotangulia na Aya na Hadithi zilizokuja na maana zinazofanana nazo, zote zinaashiria ulazima wa kuelekeza nyoyo kwa Mwenyezi Mungu katika mambo yote, na kumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake. Kwa sababu waja wameumbwa kwa ajili ya hili, na waliamrishwa kufanya hivyo, kama ilivyotajwa hapo awali katika Aya mbalimbali, na kama vile katika kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿وَاعْبُدُوا اللَّهَ وَلَا تُشْرِكُوا بِهِ شَيْئًا...﴾
"Na muabuduni Mwenyezi Mungu na msimshirikishe na chochote." [An-Nisaai: 36] Na kauli yake Mtukufu:
﴿وَمَا أُمِرُوا إِلَّا لِيَعْبُدُوا اللَّهَ مُخْلِصِينَ لَهُ الدِّينَ...﴾
"Nao hawakuamrishwa kitu ila wamuabudu Mwenyezi Mungu kwa kumtakasia Dini." [Surat Al-Bayyina: 5] Na maneno ya Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake katika hadithi ya Muadhi Mwenyezi Mungu amuwiye radhi: “Haki ya Mwenyezi Mungu juu ya waja wake ni kwamba wamuabudu wala wasimshirikishe na chochote.” Wanachuoni wamekubaliana kwamba hadithi hii ni sahihi. Na kauli yake Mtume rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, katika hadithi ya bin Masudi, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi: "Yeyote atakayekufa huku anamuomba mwenza pamoja na Mwenyezi Mungu, ataingia Motoni." Imepokelewa na Bukhari. Katika Sahihi mbili, kutoka kwa bin Abbas, Mwenyezi Mungu awawie radhi wote wawili, ya kwamba Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alipomtuma Muadhi kwenda Yemen, alimwambia: “Hakika wewe unawajia watu wa Kitabu, basi na liwe la kwanza utakalowalingania ni kushuhudia kwamba hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu." Na katika tamko lingine: “Waite katika kushuhudia kwamba hapana mungu ila Mwenyezi Mungu, na kwamba hakika mimi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu." Na katika mapokezi ya Bukhari: "Basi na liwe jambo la kwanza unalowalingania ni kumpwekesha Mwenyezi Mungu." Na katika Sahihi Muslim, kutoka kwa Tariq bin Ushaim Al-Ashja’i, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, ya kwamba Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisema: "Atakayesema: Laa ilaaha illa llaah, na akakufuru vyote vinavyoabudiwa kinyume na Mwenyezi Mungu, itakuwa haramu mali yake na damu yake, na hesabu yake itakuwa juu ya Mwenyezi Mungu, Mwenye utukufu mkubwa." Na kuna hadithi nyingi zenye maana hii.
Tauhidi hii ndiyo chimbuko la Dini ya Uislamu, nayo ndiyo msingi wa mila hii, na ndiyo kichwa cha jambo hili, na ndiyo wajibu muhimu zaidi, nayo ndiyo hekima katika kuumbwa kwa vizito viwili (wanadamu na majini), na ndiyo hekima ya kuwatuma Mitume wote, rehema na amani ziwe juu yao, kama ilivyotangulia katika aya zilizoonyesha hayo. Miongoni mwake ni maneno ya Mola Mtukufu:
﴿وَمَا خَلَقْتُ الْجِنَّ وَالْإِنْسَ إِلَّا لِيَعْبُدُونِ56﴾
"Nami sikuwaumba majini na watu ila waniabudu Mimi." [Surat Adh-Dhariyaat: 56]. Na miongoni mwa ushahidi wa hayo ni kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿وَلَقَدْ بَعَثْنَا فِي كُلِّ أُمَّةٍ رَسُولًا أَنِ ااعْبُدُوا اللَّهَ وَاجْتَنِبُوا الطَّاغُوتَ...﴾
"Na kwa hakika, kwa kila umma tuliutumia Mtume kwamba: Muabuduni Mwenyezi Mungu, na muepukeni Twaghuut (Shetani na vyote vinavyoabudiwa kando na Mwenyezi Mungu." [Surat An-Nahl: 36]. Na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿وَمَا أَرْسَلْنَا مِنْ قَبْلِكَ مِنْ رَسُولٍ إِلَّا نُوحِي إِلَيْهِ أَنَّهُ لَا إِلَهَ إِلَّا أَنَا فَاعْبُدُونِ25﴾
"Na hatukumtuma kabla yako Mtume yeyote ila tulimfunulia ya kwamba hapana mungu isipokuwa Mimi. Basi niabuduni Mimi tu." [Al-Anbiya: 25]. Na Mwenyezi Mungu Mwenye utukufu mkubwa amesema kuhusu Nuhu, Hud, Saleh na Shuaib -rehema na amani ziwe juu yao- kwamba waliwaambia watu wao:
﴿...اعْبُدُوا اللَّهَ مَا لَكُمْ مِنْ إِلَهٍ غَيْرُهُ...﴾
"Muabuduni Mwenyezi Mungu. Nyinyi hamna Mungu ila Yeye." [Al-A'araf: 59]. Na huu ndio wito wa Mitume wote, kama ilivyoashiriwa na zile Aya mbili zilizotangulia. Na maadui wa Mitume walikiri kwamba Mitume waliwaamrisha kumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake na kuwakataa waungu wanaoabudiwa badala yake, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mwenye utukufu mkubwa katika kisa cha 'Adi, kwamba walimwambia Hudi, rehema na amani ziwe juu yake:
﴿...أَجِئْتَنَا لِنَعْبُدَ اللَّهَ وَحْدَهُ وَنَذَرَ مَا كَانَ يَعْبُدُ آبَاؤُنَا...﴾
"Je, umetujia ili tumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake, na tuyaache waliyo kuwa wakiyaabudu baba zetu?" [Al-A'araf: 70], Na alisema Mwenyezi Mungu Mtukufu kuhusu Makuraishi pale Mtume wetu Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alipowalingania kumuabudu Mwenyezi Mungu peke yake na kuyaacha waliyokuwa wakiyaabudu badala yake miongoni mwa Malaika, watakatifu, masanamu, miti na vinginevyo:
﴿أَجَعَلَ الْآلِهَةَ إِلَهًا وَاحِدًا إِنَّ هَذَا لَشَيْءٌ عُجَابٌ5﴾
"Amewafanya miungu wote kuwa ni Mungu Mmoja tu? Hakika hili ni jambo la ajabu sana." [Swad: 5] Na amesema Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kutukuka kuhusu wao:
﴿إِنَّهُمْ كَانُوا إِذَا قِيلَ لَهُمْ لَا إِلَهَ إِلَّا اللَّهُ يَسْتَكْبِرُونَ35 وَيَقُولُونَ أَئِنَّا لَتَارِكُوٓاْ ءَالِهَتِنَا لِشَاعِرٖ مَّجۡنُونِۭ36﴾
"Hakika wao walikuwa wanapoambiwa: 'Laa ilaaha illallahu (Hapana mungu ila Mwenyezi Mungu tu)', wanajivuna."
Na wanasema: Hivyo sisi tuiache miungu yetu kwa ajili ya huyu mtunga mashairi mwendawazimu?" [As-Saffat: 35, 36]. Na kuna aya nyingi zinazoonyesha maana hii.
Kutokana na Aya na hadithi tulizozitaja, inakubainikia -Mwenyezi Mungu aniwezeshe mimi na wewe kuifahamu dini na kutambua sawasawa haki ya Mola Mlezi wa walimwengu wote - kwamba dua hizi na aina mbalimbali za kutafuta kuokolewa ulizozitaja katika swali lako, zote ni katika aina za ushirikina mkubwa. Kwa sababu ni kuabudu asiyekuwa Mwenyezi Mungu, na kuomba mambo asiyoweza kuyafanya asiyekuwa Yeye, kutoka kwa wafu na wasiokuwepo, na hilo linachukiza zaidi kuliko ushirikina wa watu wa mwanzo; Kwa sababu wale wa mwanzo walikuwa wakishirikisha tu wakati wa raha na mafanikio. Ama katika nyakati za magumu, walikuwa wakimsafia Mwenyezi Mungu ibada. Kwa sababu walijua kwamba Yeye Mtukufu ndiye Muweza wa kuwaepusha mbali na dhiki, na si mwingine, kama alivyosema Mwenyezi Mungu katika kitabu chake kilicho wazi kuhusu washirikina hao.
﴿فَإِذَا رَكِبُواْ فِي ٱلۡفُلۡكِ دَعَوُاْ ٱللَّهَ مُخۡلِصِينَ لَهُ ٱلدِّينَ فَلَمَّا نَجَّىٰهُمۡ إِلَى ٱلۡبَرِّ إِذَا هُمۡ يُشۡرِكُونَ65﴾
"Na wanapopanda katika merikebu, humuomba Mwenyezi Mungu kwa kumsafia utiifu. Lakini anapo wavusha wakafika nchi kavu, mara wanamshirikisha." [Al-Ankabut: 65] Na Mwenyezi Mungu Mtukufu akasema akiwaongelesha katika Aya nyingine:
﴿وَإِذَا مَسَّكُمُ ٱلضُّرُّ فِي ٱلۡبَحۡرِ ضَلَّ مَن تَدۡعُونَ إِلَّآ إِيَّاهُۖ فَلَمَّا نَجَّىٰكُمۡ إِلَى ٱلۡبَرِّ أَعۡرَضۡتُمۡۚ وَكَانَ ٱلۡإِنسَٰنُ كَفُورًا67﴾
"Na inapokufikieni tabu katika bahari, hao mnao waomba wanapotea, isipokuwa Yeye tu. Na anapo kuvusheni mkafika nchi kavu, mnageuka. Ama (kweli) mwanadamu ni mwingi wa kukufuru." [Al-Israa: 67].
Iwapo mwenye kusema katika washirikina hawa wa nyuma atasema: 'Hakika sisi hatumaanishi kwamba hao wanaweza kufaidi wenyewe, au wanaponya wagonjwa wetu wenyewe, au wanaweza kutunufaisha wenyewe au kutudhuru wenyewe. Bali tunamaanisha (na kutafuta) uombezi wao kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu katika hayo?'
Jibu ni aambiwe: Hakika hili ndilo lengo na makusudio ya makafiri wa mwanzo, na hawakumaanisha ya kwamba miungu yao inaumba au kutoa riziki, au inanufaisha au inadhuru yenyewe. Kwa sababu, hayo yanabatilika kwa yale aliyoyataja Mwenyezi Mungu kuwahusu ndani ya Qur'ani, na kwamba walikusudia uombezi wao na heshima yao, na kuwakurubisha kwa Mwenyezi Mungu wawe karibu zaidi, kama alivyosema Mwenyezi Mungu aliyetakasika na kutukuka:
﴿وَيَعۡبُدُونَ مِن دُونِ ٱللَّهِ مَا لَا يَضُرُّهُمۡ وَلَا يَنفَعُهُمۡ وَيَقُولُونَ هَٰٓؤُلَآءِ شُفَعَٰٓؤُنَا عِندَ ٱللَّهِ...﴾
"Nao, badala ya Mwenyezi Mungu, wanaabudu wasiowadhuru wala kuwanufaisha, na wanasema: 'Hawa ndio waombezi wetu kwa Mwenyezi Mungu!" [Yunus: 18] Mwenyezi Mungu akawapinga katika hilo kwa kauli yake:
﴿...قُلۡ أَتُنَبِّـُٔونَ ٱللَّهَ بِمَا لَا يَعۡلَمُ فِي ٱلسَّمَٰوَٰتِ وَلَا فِي ٱلۡأَرۡضِۚ سُبۡحَٰنَهُۥ وَتَعَٰلَىٰ عَمَّا يُشۡرِكُونَ﴾
"Sema: Je, mnamwambia Mwenyezi Mungu asiyoyajua yaliyoko katika mbingu wala katika ardhi? Sub-hanahu wa Taa'la (ametakasika na ametukuka) mbali na hao wanaomshirikisha naye." [Yunus: 18] Basi, Yeye aliyetakasika akabainisha kuwa hamjui muombezi yeyote mbele yake mbinguni au ardhini kwa namna iliyokusudiwa na washirikina. Na kile ambacho Mwenyezi Mungu hajui uwepo wake, basi hicho hakipo. Kwa sababu Yeye aliyetakasika hakuna kinachofichikana kwake. Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿تَنزِيلُ ٱلۡكِتَٰبِ مِنَ ٱللَّهِ ٱلۡعَزِيزِ ٱلۡحَكِيمِ 1 إِنَّآ أَنزَلۡنَآ إِلَيۡكَ ٱلۡكِتَٰبَ بِٱلۡحَقِّ فَٱعۡبُدِ ٱللَّهَ مُخۡلِصٗا لَّهُ ٱلدِّينَ2 أَلَا لِلَّهِ ٱلدِّينُ ٱلۡخَالِصُۚ وَٱلَّذِينَ ٱتَّخَذُواْ مِن دُونِهِۦٓ أَوۡلِيَآءَ مَا نَعۡبُدُهُمۡ إِلَّا لِيُقَرِّبُونَآ إِلَى ٱللَّهِ زُلۡفَىٰٓ إِنَّ ٱللَّهَ يَحۡكُمُ بَيۡنَهُمۡ فِي مَا هُمۡ فِيهِ يَخۡتَلِفُونَۗ إِنَّ ٱللَّهَ لَا يَهۡدِي مَنۡ هُوَ كَٰذِبٞ كَفَّارٞ3﴾
"Uteremsho wa Kitabu hiki umetokana na Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Mwenye hekima.
Hakika Sisi tumekuteremshia Kitabu hiki kwa Haki. Basi muabudu Mwenyezi Mungu ukimsafia Dini Yeye tu.
Sikilizeni. Hakika Dini Safi ni ya Mwenyezi Mungu tu. Na wale wanaowafanya wenginewe kuwa ni walinzi wakisema: 'Sisi hatuwaabudu ila wapate kutujongeza tu kumkaribia Mwenyezi Mungu', hakika Mwenyezi Mungu atahukumu baina yao katika yale wanayohitilafiana. Hakika Mwenyezi Mungu hamuongoi aliye muongo kafiri." [Az-Zumar: 1-3]
Maana ya dini hapa ni ibada. Nayo ni kumtii Mwenyezi Mungu na kumtii Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kama ilivyotangulia kutajwa. Na inaingia ndani yake dua, kuomba kuokolewa, hofu, matumaini, kuchinja na nadhiri. Pia inaingia ndani yake swala, saumu na mengineyo aliyoamrisha Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Kwa hivyo, Yeye aliyetakasika akabainisha kwamba ibada ni yake peke yake, na kwamba ni wajibu kwa waja kumkusudia Yeye Mwenye utukufu mkubwa pekee ndani yake. Kwa sababu kumuamrisha kwake Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kumkusudia Yeye tu katika ibada pia ni kuwaamrisha wana wote wa umma huu.
Kisha Mwenyezi Mungu Mwenye utukufu mkubwa akaeleza baada ya hayo kuhusu makafiri. Akasema:
﴿وَٱلَّذِينَ ٱتَّخَذُواْ مِن دُونِهِۦٓ أَوۡلِيَآءَ مَا نَعۡبُدُهُمۡ إِلَّا لِيُقَرِّبُونَآ إِلَى ٱللَّهِ زُلۡفَىٰٓ﴾
"Na wale wanaowafanya wenginewe kuwa ni walinzi wakisema: Sisi hatuwaabudu ila wapate kutujongeza tu kumkaribia Mwenyezi Mungu." [Az-Zumar: 3]. Mwenyezi Mungu aliyetakasika akawajibu kwa kusema:
﴿...إِنَّ ٱللَّهَ يَحۡكُمُ بَيۡنَهُمۡ فِي مَا هُمۡ فِيهِ يَخۡتَلِفُونَۗ إِنَّ ٱللَّهَ لَا يَهۡدِي مَنۡ هُوَ كَٰذِبٞ كَفَّارٞ﴾
"Hakika Mwenyezi Mungu atahukumu baina yao katika yale wanayohitilafiana. Hakika Mwenyezi Mungu hamuongoi aliye muongo kafiri." [Az-Zumar: 3]. Basi Yeye Mtukufu, akabainisha katika Aya hii tukufu ya kwamba makafiri hawakuwaabudu mawalii badala yake isipokuwa ili kuwakurubisha kwa Mwenyezi Mungu, wawe karibu zaidi. Na haya ndiyo makusudio ya makafiri wa zamani na wa sasa, na Mwenyezi Mungu alilibatilisha hilo kwa kusema:
﴿...إِنَّ ٱللَّهَ يَحۡكُمُ بَيۡنَهُمۡ فِي مَا هُمۡ فِيهِ يَخۡتَلِفُونَۗ إِنَّ ٱللَّهَ لَا يَهۡدِي مَنۡ هُوَ كَٰذِبٞ كَفَّارٞ﴾
"Hakika Mwenyezi Mungu atahukumu baina yao katika yale wanayohitilafiana. Hakika Mwenyezi Mungu hamuongoi aliye muongo kafiri." [Az-Zumar: 3]. Basi Mwenyezi Mungu aliyetakasika akauweka wazi uongo wao katika madai yao ya kwamba miungu yao inawakurubisha kwa Mwenyezi Mungu, wakawa karibu zaidi, na kufuru yao kwa sababu ya ibada walizofanya kwa ajili yao. Basi kwa hilo, kila mwenye utambuzi hata mdogo tu atajua kwamba makafiri wa mwanzo ulikuwa ukafiri wao ni kuwachukua Mitume, mawalii, miti, mawe na viumbe vingine kuwa waombezi baina yao na Mwenyezi Mungu. Waliitakidi kwamba wanaweza kutimiza haja zao bila idhini Yake Mtukufu na kuridhia kwake, sawa na vile mawaziri wanavyofanya uombezi mbele ya wafalme. Hapo wakawa wamempima Yeye Mtukufu na wafalme na viongozi. Wakasema: Kama vile mtu ambaye ana haja kwa mfalme au kiongozi anafanyiwa uombezi kwake kupitia wasiri wake na mawaziri wake, basi ndivyo tunavyojikurubisha kwa Mwenyezi Mungu kwa kuwaabudu Manabii wake na mawalii wake. Hili ni katika batili kubwa zaidi. Kwa sababu Yeye Mtukufu, hana wa kufanana naye na wala halinganishwi na viumbe vyake, na hakuna awezaye kufanya uombezi kwake isipokuwa kwa idhini yake, na Yeye hawapi idhini isipokuwa watu wa Tauhidi tu. Yeye aliyetakasika na kutukuka ni Muweza wa kila kitu, na ni Mjuzi wa kila kitu, na Yeye ni Mwingi wa kurehemu kuliko wote wanaorehemu, wala hamuogopi yeyote, wala hamhofu. Kwa sababu Yeye Mtukufu, ni Mshindi juu ya waja wake, na huwaendesha apendavyo. Mwenyezi Mungu ni tofauti na wafalme na viongozi. Wao hawana uwezo wa kufanya kila kitu, ndiyo maana wanahitaji mtu wa kuwasaidia katika yale ambayo hawawezi kuyafanya, kama mawaziri wao, na wasiri wao na askari wao, kama vile wanavyo hitaji kujulishwa mahitaji ya wale ambao hawayajui mahitaji yao, kwa hivyo wanahitaji mtu miongoni mwa mawaziri wao na wasiri wao wa kuwafanyia huruma na kuwaridhisha. Ama Mola Mlezi Mwenye utukufu mkubwa, Yeye aliyetakasika ni Mkwasi asiyewahitaji viumbe wake wote, na ni mwenye huruma kwao sana kuliko mama zao, ndiye hakimu muadilifu, anayeweka vitu mahali pake kulingana na hekima yake, elimu yake na uwezo wake. Kwa hivyo hairuhusiwi kumlinganisha na viumbe wake kwa njia yoyote ile. Ndiyo maana, Yeye aliyetakasika akabainisha katika Kitabu chake kwamba washirikina walikiri kwamba Yeye ndiye Muumba, Mwenye kuruzuku na Mwendeshaji mambo, na kwamba Yeye ndiye Mwenye kujibu wenye dhiki kubwa, anayeondoa maovu, anayehuisha na anayefisha na mengineyo miongoni mwa vitendo vyake Yeye aliyetakasika. Mzozo baina ya washirikina na Mitume ulikuwa juu ya kumkusudia Mwenyezi Mungu peke yake katika ibada, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mwenye utukufu mkubwa:
﴿َوَلَئِن سَأَلۡتَهُم مَّنۡ خَلَقَهُمۡ لَيَقُولُنَّ ٱللَّهُ...﴾
"Na ukiwauliza ni nani aliyewaumba? Bila ya shaka watasema: Mwenyezi Mungu!" [Az-Zukhruf: 87] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿قُلۡ مَن يَرۡزُقُكُم مِّنَ ٱلسَّمَآءِ وَٱلۡأَرۡضِ أَمَّن يَمۡلِكُ ٱلسَّمۡعَ وَٱلۡأَبۡصَٰرَ وَمَن يُخۡرِجُ ٱلۡحَيَّ مِنَ ٱلۡمَيِّتِ وَيُخۡرِجُ ٱلۡمَيِّتَ مِنَ ٱلۡحَيِّ وَمَن يُدَبِّرُ ٱلۡأَمۡرَۚ فَسَيَقُولُونَ ٱللَّهُۚ فَقُلۡ أَفَلَا تَتَّقُونَ31﴾
"Sema: Ni nani anayekuruzukuni kutoka mbinguni na kwenye ardhi? Au ni nani anayemiliki kusikia na kuona? Na ni nani amtoaye hai kutoka kwenye maiti, na akamtoa maiti kutoka kwa aliye hai? Na ni nani anayeyaendesha mambo yote? Watasema: Allah (Mwenyezi Mungu). Basi sema: Je, hamumchi?" [Yunus: 31] Na aya zenye maana hii ni nyingi sana.
Zilishatangulia kutajwa Aya zinazoonyesha kwamba mzozo uliokuwa baina ya Mitume na umma wao ni juu ya kumkusudia Mwenyezi Mungu pekee katika ibada, kama vile kauli yake Mtukufu:
﴿وَلَقَدۡ بَعَثۡنَا فِي كُلِّ أُمَّةٖ رَّسُولًا أَنِ ٱعۡبُدُواْ ٱللَّهَ وَٱجۡتَنِبُواْ ٱلطَّٰغُوتَ...﴾
"Na kwa hakika, kwa kila umma tuliutumia Mtume kwamba: Muabuduni Mwenyezi Mungu, na muepukeni Twaghuut (Shetani na vyote vinavyoabudiwa kinyume na Mwenyezi Mungu." [Surat An-Nahl: 36]. Na kuna aya nyingi sana zilizokuja katika maana hii. Na Yeye aliyetakasika ameeleza katika sehemu nyingi katika Kitabu chake kitukufu suala la uombezi. Akasema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿َ...مَن ذَا ٱلَّذِي يَشۡفَعُ عِندَهُۥٓ إِلَّا بِإِذۡنِهِ...﴾
"Ni nani huyo awezaye kuombea mbele yake isipokuwa kwa idhini yake?" [Al-Baqara: 255]. Na akasema Mwenyezi Mungu, Mwenye nguvu, Mtukufu:
﴿وَكَم مِّن مَّلَكٖ فِي ٱلسَّمَٰوَٰتِ لَا تُغۡنِي شَفَٰعَتُهُمۡ شَيۡـًٔا إِلَّا مِنۢ بَعۡدِ أَن يَأۡذَنَ ٱللَّهُ لِمَن يَشَآءُ وَيَرۡضَىٰٓ26﴾
"Na wako Malaika wangapi mbinguni, ambao uombezi wao hautafaa chochote isipokuwa baada ya Mwenyezi Mungu kutoa idhini kwa amtakaye na kumridhia." [An-Najm: 26].
Na akasema katika kuwaelezea Malaika:
﴿...وَلَا يَشۡفَعُونَ إِلَّا لِمَنِ ٱرۡتَضَىٰ وَهُم مِّنۡ خَشۡيَتِهِۦ مُشۡفِقُونَ﴾
"Wala hawamuombei yeyote ila yule anayemridhia Yeye, nao kwa sababu ya kumuogopa wananyenyekea." [Al-Anbiya: 28].
Na akajulisha kuwa haridhii ukafiri kutoka kwa waja wake. Bali anaridhia shukurani kutoka kwao. Nayo shukurani ni kumpwekesha na kufanya matendo ya kumtii. Amesema Mtukufu:
﴿إِن تَكۡفُرُواْ فَإِنَّ ٱللَّهَ غَنِيٌّ عَنكُمۡۖ وَلَا يَرۡضَىٰ لِعِبَادِهِ ٱلۡكُفۡرَۖ وَإِن تَشۡكُرُواْ يَرۡضَهُ لَكُمۡ...﴾
"Mkikufuru, basi Mwenyezi Mungu si mwenye haja nanyi, lakini hafurahii kufuru kwa waja wake. Na mkishukuru, Yeye hufurahika nanyi." [Az-Zumar: 7]
Na imepokelewa na Bukhari katika Sahihi yake kutoka kwa Abuu Huraira, radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, kwamba alisema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, ni nani mwenye furaha zaidi ya kupata uombezi wako?" Akasema: "Atakayesema: 'Laa ilaaha illa llaahu (Hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu) likiwa limetoka moyoni mwake kwa utakasifu kabisa." Au alisema: "Kutoka katika nafsi yake."
Na katika Sahihi tena, kutoka kwa Anas, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kutoka kwa Mtume, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisema: "Kila Nabii ana dua inayojibiwa. Basi kila Nabii akaharakisha kuomba dua yake. Nami nimeihifadhi dua yangu iwe ni uombezi kwa ajili ya umma wangu Siku ya Kiyama, nayo itampata - Mwenyezi Mungu akipenda - kila atakayekufa katika umma wangu huku hamshirikishi Mwenyezi Mungu na chochote." Na kuna hadithi nyingi zenye maana hii.
Aya na hadithi zote tulizozitaja zinaashiria kuwa ibada ni haki ya Mwenyezi Mungu peke yake, na kwamba hairuhusiwi kufanya chochote miongoni mwake kwa ajili ya asiyekuwa Mwenyezi Mungu, si kwa ajili ya Manabii wala wengineo, na kwamba uombezi ni miliki ya Mwenyezi Mungu, kama alivyosema Mtukufu:
﴿قُل لِّلَّهِ ٱلشَّفَٰعَةُ جَمِيعٗا...﴾
"Sema: Uombezi wote uko kwa Mwenyezi Mungu." [Az-Zumar: 44] Hakuna anayeustahiki uombezi isipokuwa baada kumpa muombezi idhini na kumridhia yule anayefanyiwa uombezi. Naye aliyetakasika haridhii chochote isipokuwa kumpwekesha Yeye, kama ilivyotajwa hapo awali. Basi kwa mujibu wa hayo, washirikina hawana fungu lolote katika uombezi, na Mwenyezi Mungu alikwishabainisha haya katika kauli yake Mtukufu:
﴿فَمَا تَنفَعُهُمۡ شَفَٰعَةُ ٱلشَّٰفِعِينَ 48﴾
"Basi hautawafaa kitu uombezi wa waombezi." [Al-Muddaththir: 48] Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿...مَا لِلظَّٰلِمِينَ مِنۡ حَمِيمٖ وَلَا شَفِيعٖ يُطَاعُ 18﴾
"Madhalimu hawatakuwa na rafiki, wala muombezi wa kuitikiwa." [Ghaafir: 18].
Inajulikana kuwa dhuluma kwa ujumla ni kumshirikisha Mwenyezi Mungu, kama alivyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿...وَٱلۡكَٰفِرُونَ هُمُ ٱلظَّٰلِمُونَ﴾
"Na makafiri ndio madhalimu." [Al-Baqara: 254], Na amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿...إِنَّ ٱلشِّرۡكَ لَظُلۡمٌ عَظِيمٞ﴾
"Kwani hakika ushirikina bila ya shaka ni dhuluma kubwa." [Luqman: 13].
Ama uliyoyataja katika swali lako katika kauli za baadhi ya Masufi misikitini na kwingineko: "Ewe Mwenyezi Mungu, mrehemu yule uliyemfanya sababu ya kugawanyika kwa siri zako kuu, na kuzuka kwa nuru zako za rehema, basi akawa ni mwakilishi wa uwepo wa Mola Mlezi, na mrithi wa siri zako za ndani ... n.k.
Jibu ni kwamba: Maneno haya na kauli zinazofanana nayo ni katika kujisumbua bure na kuwa na msimamo mkali ambao Mtume wetu Muhammad, rehema na amani zimshukie, alionya dhidi yake katika yale aliyoyasimulia Muslim ndani ya Sahihi yake kutoka kwa Abdullah bin Masudi, Mwenyezi Mungu amuwie radhi, kuwa alisema kwamba: Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani zimshukie, alisema: "Watu wenye msimamo mkali wameangamia," aliyasema mara tatu.
Amesema Imam Khattwabi, Mwenyezi Mungu amrehemu: Mwenye msimamo mkali ni yule anayezama katika jambo fulani na kujisumbua kulipekua akifuata njia ya watu wa theolojia (wana falsafa), wanaoingia katika yale yasiyowahusu, wanaozama katika yale ambayo akili zao haziwezi kuyafikia.
Na alisema Abuu Sa'adaat binil-Athiir: Hao ndio wanaozama na kuingia ndani katika mazungumzo, ambao huzungumza kwa mapafu yao (Yaani: Kwa kujikalifisha wasiyoyaweza).
Na kwa yale waliyoyataja maimamu hawa wawili miongoni mwa maimamu wa lugha, inakudhihirikia wewe na kila mwenye ufahamu hata mdogo kwamba namna hii ya kumuombea rehema na amani Nabii wetu na Mtume wetu na bwana wetu, Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, ni miongoni mwa kujisumbua na kushika msimamo mkali ambako kulikatazwa. Katika mlango huu, Muislamu anafaa kutafuta njia iliyothibiti ya kumuombea rehema na amani Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, na hiyo itamtoshelezaa asihitaji njia nyingine yoyote.
Katika hizo ni ile iliyopokelewa na Bukhari na Muslim katika Sahihi zao mbili, kutoka kwa Ka'ab bin Ujrah, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kwamba Maswahaba, Mwenyezi Mungu awawie radhi walisema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu alituamrisha kukuombea rehema, basi tunakuombea vipi rehema?" Akasema: Semeni: Ewe Mwenyezi Mungu, shusha rehema juu ya Muhammad na aali zake Muhammad, kama ulivyoshusha rehema juu ya Ibrahim na aali za Ibrahim. Hakika Wewe ni Msifiwa mno, Mtukufu. Na shusha baraka juu ya Muhammad na aali za Muhammad, kama ulivyoshusha baraka juu ya Ibrahim na aali za Ibrahim. Hakika Wewe ni Msifiwa mno, Mtukufu.
Na katika Sahihi mbili, kutoka kwa Abuu Humaidi As-Sa’idi, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, kwamba walisema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, tuna kuombea vipi rehema?" Akasema: “Semeni: Ewe Mwenyezi Mungu, shusha rehema juu ya Muhammad na wake zake na dhuriya wake, kama ulivyoshusha rehema juu ya aali za Ibrahim. Na mbariki Muhammad na wake zake na dhuriya wake, kama ulivyowabariki aali za Ibrahimu. Hakika Wewe ni Msifiwa mno, Mtukufu.”
Na katika Sahihi Muslim, kutoka kwa Abuu Masud Al-Ansari, Mwenyezi Mungu amuwiye radhi, alisema: Bashir bin Sa'ad alisema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu ametuamrisha kukuombea rehema, basi tunakuombea vipi rehema?" Akanyamaza, kisha akasema: “Semeni: 'Ewe Mwenyezi Mungu, shusha rehema juu ya Muhammad na aali za Muhammad, kama ulivyoshusha rehema juu ya aali za Ibrahimu. Na mbariki Muhammad na aali za Muhammad kama ulivyowabariki aali za Ibrahim. Hakika wewe katika walimwengu ni Msifiwa, Mtukufu.' Na kutoa salamu ni kama mlivyokwishajua."
Maneno haya na maneno yanayofanana na hayo miongoni mwa yale yaliyothibiti kutoka kwa Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, ndiyo mambo ambayo Muislamu anapaswa kuyatumia katika kumuombea rehema na amani Mtume wa Mwenyezi Mungu, rehema na amani ziwe juu yake. Kwa sababu Mtume, rehema na amani ziwe juu yake, ndiye mjuzi zaidi kuliko watu wote kuhusu yale yanayostahiki kutumika kuhusiana naye, kama vile yeye ndiye mjuzi zaidi kuliko watu wote kuhusu maneno yanayofaa kutumika kuhusiana na Mola wake Mlezi.
Ama maneno yaliyotungwa tu na ya kizushi, na maneno yanayoweza kuwa na maana isiyo sahihi; kama maneno yaliyotajwa katika swali lako, hayo hayapaswi kutumiwa. Kwa sababu ni ya kujisumbua tu, na kwa sababu yanaweza kufasiriwa kwa maana batili, pamoja na kwamba hayo ni kinyume na maneno aliyoyachagua Mtume wa Mwenyezi Mungu rehema na amani ziwe juu yake na akauongoza umma wake kuyatumia, naye ndiye mjuzi zaidi ya viumbe vyote na anayewanasihi zaidi na aliye mbali zaidi ya mambo ya kujisumbua bure, rehema na amani bora zaidi ziwe juu yake kutoka kwa Mola wake Mlezi.
Ni hayo tu, na ninatumai kwamba kuna utoshelevu na manufaa kwa mwenye kutafuta haki katika yale tuliyoyataja ya ushahidi wa kueleza uhakika wa Tauhidi, uhakika wa ushirikina, na tofauti baina ya walivyokuwa wakifanya washirikina wa mwanzo na washirikina wa baadaye katika suala hili, na katika kueleza jinsi ya kumuombea Mtume rehema kwa njia ya kisheria. Ama yule asiyetaka kujua haki, basi huyo anafuata tu matamanio yake. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu:
﴿فَإِن لَّمۡ يَسۡتَجِيبُواْ لَكَ فَٱعۡلَمۡ أَنَّمَا يَتَّبِعُونَ أَهۡوَآءَهُمۡۚ وَمَنۡ أَضَلُّ مِمَّنِ ٱتَّبَعَ هَوَىٰهُ بِغَيۡرِ هُدٗى مِّنَ ٱللَّهِۚ إِنَّ ٱللَّهَ لَا يَهۡدِي ٱلۡقَوۡمَ ٱلظَّٰلِمِينَ50﴾
"Na ikiwa hawakuitikii, basi jua kuwa wanafuata pumbao lao tu. Na ni nani aliyepotea zaidi kumshinda anayefuata pumbao lake bila ya uongofu utokao kwa Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu hawaongoi watu wenye kudhulumu." [Al-Qasas: 50]
Basi Yeye Mtukufu, akabainisha katika Aya hii tukufu kwamba; watu kuhusiana na yale ambayo Mwenyezi Mungu aliyomtuma nayo Mtume wake Muhammad, rehema na amani za Mwenyezi Mungu zimshukie ya uongofu na Dini ya haki wako aina mbili:
Ya kwanza: Mwenye kumuitikia Mwenyezi Mungu na Mtume wake.
Ya pili: Mwenye kufuata matamanio yake, kisha Yeye Mtukufu akaeleza kuwa hakuna mpotevu zaidi kuliko yule anayefuata matamanio yake bila ya uongofu utokao kwa Mwenyezi Mungu.
Tunamuomba Mwenyezi Mungu -Aliyetukuka- atujaalie salama kutokana na kufuata matamanio, na kwamba atujaalie sisi na nyinyi na ndugu zetu wote miongoni mwa wale wenye kumuitikia Mwenyezi Mungu na Mtume wake, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, wale wanaoiheshimu sheria yake na wanaojitahadhari dhidi ya kila kitu kinachokwenda kinyume na sheria yake, kama uzushi na matamanio. Kwani Yeye ndiye Mpaji, Mkarimu zaidi.
Na rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu ya mja wake na Mtume wake, Nabii wetu Muhammad, na aali zake, Maswahaba wake na wafuasi wake wanaomfuata kwa wema mpaka Siku ya Malipo.
***